Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nianze kwanza kwa kuipongeza Wizara, hasa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, kwa kazi nzuri ambayo mmeendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipomshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo amejitoa sana kwenye sekta hii. Na kazi nzuri aliyoifanya tunaona hivi sasa; vijiji takribani 10,312 vimeshafikiwa. Na ninaamini kabisa azma ile ya kufikia vijiji vyote itafikiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, hapa Mkoa wa Dodoma ametuletea watendaji wazuri kwa TANESCO. Alikuwepo meneja wetu hapa Frank Chambua, amefanya kazi nzuri, umem-promote amekuwa Meneja wa Kanda. Lakini hivi sasa ametuletea Boimanda, na yeye anafanya kazi nzuri sana; tunamshukuru sana kwa kuona umuhimu wa kuwaleta watendaji hawa katika Mkoa wetu wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nianze kuzungumzia masuala ya utekelezaji wa miradi ya nishati ya umeme katika Jimbo la Dodoma Mjini, na hasa katika miradi hii mikubwa miwili ya densification na peri urban. Mheshimiwa Waziri, nataka nikushukuru sana na niishukuru sana Serikali kwa kutenga zaidi ya shilingi bilioni 100 ya utekelezaji wa miradi ya umeme katika Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii tafsiri yake ni kwamba itakwenda kuiwasha Dodoma nzima, na hapo sasa tutakuwa tumefikia malengo ya kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu ya kweli ya Nchi ambayo umeme utawaka maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kwenye mradi densification tunashukuru kwamba mkandarasi aliyepo anafanya kazi yake vizuri sana, ameyafikia maeneo mengi yale ambayo yalikuwa hayajafikiwa na umeme. Na nimpongeze sana kwa kweli Mkandarasi Derm Electrics kwa kazi nzuri ambayo anaifanya, na hivi sasa karibia maeneo yote ambayo yalirukwa kwenye umeme wa REA Awamu ya Kwanza na ya Pili, yanatekelezewa mradi huu wa densification. Kwa imani yangu ni kwamba yatakamilika yote na Dodoma yote itaendelea kuwaka.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, jana nimepigiwa simu na nimekutana na mkandarasi wa CILEX ambaye ndiyo atakwenda kutekeleza mradi wa peri urban ambao kwa mara ya kwanza utakwenda kuwasha umeme kwenye Kata za Chihanga na Mbalawala ambazo hazijawahi kuona nguzo hata moja tangu kuumbwa kwa ulimwengu huu. Lakini pia utafika mpaka maeneo ya Mkoyo. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ombi langu; hivi sasa Jiji la Dodoma linakua kwa kasi sana, maeneo ni mengi sana ambayo yanaendelezwa. Niwaombe watendaji wako waongeze kasi na hasa katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, tuna maeneo yametengwa kwa ajili ya viwanda; eneo la Nala na eneo la Mpunguzi. Wawekezaji wengi wanashindwa kuja kuanza kuwekeza kwa sababu hakuna miundombinu ya nishati ya umeme.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, ulitoa msisitizo mkubwa sana kwa mkuu wa mkoa na mkuu wa mkoa amelibeba suala la kiwanda cha mbolea pale Nala. Walishindwa kuanza kwa sababu hakukuwa na miundombinu ya umeme. Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Anthony Mtaka, ameshinda pale Nala siku mbili na watu wa TANESCO na Jumamosi umeme unawaka na mwekezaji ataanza kujenga kiwanda kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Wizara, Dodoma maeneo haya mawili yanafahamika, ya Mpunguzi na Nala; nikuombe Mheshimiwa Waziri, twendeni tukawekeze kule tuweke miundombinu ili wawekezaji wengi zaidi waje. Kwa sababu hivi sasa tunamtegemea mwekezaji mkubwa wa SBL na TBL lakini wao wakifika itakuwa pia kichocheo kwa wawekezaji wengi kuja kuwekeza Dodoma.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, nikuombe katika mipango yako angalia sana maeneo ya industrial park ili tukaweke umeme kuwavutia wawekezaji wengi zaidi. Akija TBL hapa Dodoma, akija SBL, atawavutia wawekezaji wengine na viwanda vingi vitajengwa. Hivyo nikuombe Mheshimiwa Waziri uliangalie hili kwa macho mawili.

Mheshimiwa Spika, suala la mradi wa bomba la mafuta (EACOP); kwanza kabisa nataka nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo ameharakisha na ameshiriki katika mchakato wa kusaini mikataba hii muhimu sana kwa ajili ya bomba hili.

Mheshimiwa Spika, bomba hili lina urefu wa kilometa 1,443. Bomba hili ni refu sana na eneo kubwa liko eneo la Tanzania. Inapotoka kule Kabahale, Hoima, mpaka Chongoleani, maana yake ni kwamba katikati kote hapa bomba hili litaacha athari chanya.

Mheshimiwa Spika, sasa mchango wangu ni kuomba Serikali kwamba pamoja na uwepo wa bomba hili, lakini bomba hili lazima lilete manufaa kwa wananchi wetu wa Tanzania na hasa jumuiya ya wafanyabiashara na wajasiriamali katika Nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba kwenye bomba hili ajira takribani 15,000 zitatengenezwa. Lakini nawaomba Wizara kupitia EWURA najua mmewasajili wale watoa huduma takribani 570, lakini twende mbele zaidi. Uganda kwenye bomba hili hili Mheshimiwa Waziri, wame- ring fence baadhi ya categories ambazo lazima zifanywe na wazawa. Mheshimiwa Waziri, na hapa Tanzania mme-ring fence categories nyingi sana ambazo zitafanywa na wazawa isipokuwa hamjazitangaza. Mheshimiwa Waziri, tunaomba msiwa-take by surprise business community; mtangaze tujue maeneo gani Watanzania watafanya. Mkiwa-take by surprise watashindwa kujiandaa vizuri, watakuja wageni watazichukua hizi nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kama tayari tunafahamu maeneo gani ambako huduma zitatolewa na bidhaa zitahitajika, naomba mtangaze mapema ili watu wajiandae. Kwa hivi sasa hamjatoa tangazo lolote Mheshimiwa Waziri, watu wanajua tu kwamba kuna fursa lakini hawajui fursa gani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeomba EWURA, kama mmeshawasajili hawa watoa huduma toeni matangazo kila mtu ajue ili kama kuna masuala ya mafundi wa kuchomelea watu wajue, kama kuna masuala ya kuleta crane watu wajue; hayo yote lazima yaainishwe na Watanzania wajiandae katika hilo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, lakini kwenye Watanzania kujiandaa katika hili, naomba pia msiwasahau wajasiriamali wadogowadogo. Nimeona Wizara mmejielekeza sana kwa wafanyabiashara wakubwa wenye makampuni, lakini tunawasahau wale wajasiriamali wadogowadogo ambako bomba hili linapita.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba upitie kufanya vikao pamoja na mikoa yote ambako bomba hili linapita ili tuwaandae akinamama, vijana na watu wenye ulemavu pia kushiriki kwenye mradi huu mkubwa. Najua mama lishe watahitajika, najua vijana nguvukazi itahitajika, lakini tuwaandae mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho katika hili niiombe Wizara ya Fedha, Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Nishati na Madini mkae pamoja muwasaidie wafanyabiashara ambao wamekuwa listed pale EWURA ili waweze kufanya kazi hii vizuri. Kwa sababu najua moja kati ya changamoto kubwa ni changamoto ya mitaji.

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara hawa ambao watashiriki kwenye bomba la mafuta wakienda kwa aina ya mikopo ya asilimia 21 katika commercial rate, hakuna mtu ataweza kufanya. Lakini Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Baraza la Taifa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Wizara ya Nishati pamoja na Wizara ya Fedha, naomba mkae na taasisi za benki, taasisi za kifedha, mkubaliane kwamba kwa sababu bomba hili mahitaji yake yanafahamika, wale wote ambao wamekuwa listed, yale makampuni 570, wakienda kuomba mkopo basi riba yao iwe tofauti na riba iliyoko hivi sasa katika soko la biashara ya kibenki kwa sababu asilimia 21 hawataweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Wachina wanafanikiwa sana kwa sababu Serikali yao inaingia katikati na mikopo yao ni asilimia tatu mpaka nne. Asilimia 21 hakuna Mtanzania ataweza kufanya kazi hiyo, lakini mnao uwezo wa kukaa pamoja na benki.

Mheshimiwa Spika, hoja ya benki ni kwamba wakitoa mikopo mingi risk yake ni kubwa kwenye repayment. Lakini mkikaa nao kwa pamoja uko mfumo unaitwa contract cash flow discounting; unachukua mkataba aliyopewa huyu mtoa huduma unaupeleka benki, benki anafungua akaunti ya huyu mtoa huduma, mtoa huduma huyu akilipwa malipo yapitie katika benki iliyomkopesha, benki wakate hela yake iwe sehemu ya malipo ya deni halafui naye abaki na kile cha ziada. Tukifanya hivyo tutakuwa tumewasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa trend ambayo tunakwenda nayo hivi sasa, asilimia kubwa ya Watanzania hawataweza, watashindwa kwa sababu mikopo yetu iko juu sana.

Mheshimiwa Spika, niiombe Wizara ya Fedha; mnaweza mkaenda mpaka ikafikia asilimia nane katika riba. Hili linawezekana sana kwa sababu benki atakuwa na uhakika wa repayment ya mkopo wake. Lakini vinginevyo wazawa, wafanyabiashara wa Kitanzania wataishia kuuona mradi huu kwa mbali, watakuja Wachina na Wazungu hapa watachukua shughuli zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tutafurahi tukiona Watanzania wananeemeka na huu mradi, lakini Serikali lazima muweke mkono wenu. Muwawezeshe kama ambavyo mataifa mengine yanafanya. Mkiwaacha waende wenyewe blindly tu, naona hatari kwamba mwisho wa siku Watanzania wengi hawatanufaika.

Mheshimiwa Spika, hivyo, niwaombe Wizara ya Fedha, mnao uwezo wa kukaa pamoja na hizi taasisi za kifedha mkaweka huu utaratibu mzuri. Riba ishuke kutoka asilimia 21 iende asilimia nane mpaka kwenda chini huko ili Watanzania wengi zaidi waweze kushiriki kwenye mradi huu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)