Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na kwa kuanza tu ninataka nikushukuru kwa kutukumbusha kuzingatia misimamo ya nchi yetu na sera za chama chetu ambazo zimeainishwa kwenye Ilani ya Uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nilipokuwa nimejipanga kuchangia nikaenda kuangalia sera zetu za mambo ya nje, nisije nikasema jambo ambalo liko kinyume na sera za chama kuhusu mambo ya nje, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa imani yangu mimi nchi yetu imepata hifadhi kubwa sana ambayo haitoki kwa mtu mwingine yeyote wala Taifa lingine lolote, inatoka kwa Mungu mwenyewe kutokana na namna ambavyo sisi kama Taifa tumeji-address siku zote kwamba ni Taifa linalosimamia haki na linaloheshimu utu na haki za binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hilo ni toka Taifa letu lilipoasisiwa na Mzee wetu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Abeid Aman Karume. Tumeji-address hivyo, duniani kote wanatufahamu kwamba Tanzania ni nchi ambayo inaheshimu haki za binadamu na inatetea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwenzangu ametoka kusema muda mfupi uliopita juu ya msimamo wetu kama Taifa kuhusu hali inayoendelea Mashariki ya Kati, na ukisoma kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, hakuligusia. Amegusia diplomasia ya uchumi, Mashariki ya Kati tunauza nyama Qatar, Oman, Kuwait; ni jambo jema, lakini ninachotaka kusema ni kwamba tusirudi nyuma, wala tusione woga, wala tusione aibu kusema sisi kama Taifa jambo hili hatulioni sawa, tunawaomba wakubwa kaeni muone jinsi ya kutatua matatizo haya. Si jambo baya wala si dhambi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa ninakumbuka maneno ya Askofu Desmond Tutu wakati wa harakati za ukombozi Kusini mwa Afrika; alisema hivi; If you are neutral in situations of injustice, you have chosen the side of the oppressor. Kama unakaa kimya katika jambo ambalo wengine wanakandamizwa, maana yake wewe umechagua upande wa wale wakandamizaji ndiyo upande wako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi hatuwezi kuwa upande wa wakandamizaji, tunataka Mungu aendelee kutoa baraka kwenye Taifa hili. Msimamo wetu toka wakati wa Mwalimu na mpaka leo haujabadilika, ni kwamba Wapalestina wamefika mahali wamekaliwa katika ardhi yao na kwamba ni lazima waachiwe ardhi yao. Huo ni msimamo ambao tumekuwa nao na hatujawahi kurudi nyuma katika msimamo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawaomba hao wakubwa huko watafute namna ya kufanya mambo huko Mashariki ya Kati yaende vizuri badala ya kushuhudia dunia watu wanakufa kwa maelfu halafu sisi tunasema tunakaa kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, tulikuwa na msimamo mkali hata juu ya Morocco ambayo ilikuwa inaikalia Sahara ya Magharibi, na huo msimamo wetu hatujawahi mahali popote kuuondoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachotaka kusema ni kwamba katika jambo hili lazima tupaze sauti na tusione vibaya kama Taifa kusema kwamba hili hatuoni vizuri. Hatumshutumu yeyote, hatukai upande wowote, lakini hatuoni vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze sasa kuzungumzia hasa masuala yanayohusu diplomasia ya uchumi. Katika ukurasa wa 23 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia ushirikiano wa Tanzania na nchi za Afrika, na akaeleza kwa mtiririko; Kenya, Burundi, Msumbiji na nchi nyingine amezitaja nyingi. Lakini kwa bahati mbaya sikuona DRC Kongo ikiwa imetajwa, inawezekana zipo sababu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nilichotaka kusema mimi natoka Kigoma Mjini, sisi jirani zetu pale ni watu wa DRC na hawa watu wa DRC wamechangia sana mzunguko wa fedha katika Mkoa wa Kigomana hii inatokana na nanii, inatokana na ukweli kwamba watu wa DRC hasa Mkoa wa Kivu ambao tunapakana nao, huduma nyingi wanazipata kutoka nchini kwetu. Na hili ni eneo na fursa kubwa sana kwa sababu Mkoa wa Kivu una population ya watu karibu milioni sita, lakini umbali kutoka Mkoa wa Kivu kwenda Kinshasa ni zaidi ya kilometa 1,900 maana yake unatokana Kigoma, unapita Mtwara unaingia mpaka Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya nchi ile bado haijawa mizuri sana, kwa hiyo huduma nyingi bado wanazitegemea katika nchi yetu, fursa hii tumeipoteza kwa sababu ya kutokutengeneza mazingira mazuri ya kibiashara ya sisi na DRC. Na hapa ningependa Mheshimiwa Waziri unisikilize vizuri, moja ya jambo ambalo limekuwa likilalamikiwa ni pamoja na visa kubwa kwa wafanyabiashara wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna visa ya dola 50 ambazo ni hela nyingi kwa mfanyabiashara mdogo anayetoka DRC Kongo kuja kufuata bidhaa ambazo anajua atazipata kutoka Kigoma, lakini sasa hivi kimeongezeka tena kitu kingine mbali na hiyo visa kila Mkongo anayeingia anatakiwa apimwe covid na kupimwa covid dola 25 sisi ndiyo tuna kiwango kikubwa cha kupima covid kuliko Kenya, kuliko Uganda, kuliko DRC yenyewe. Wenzetu wengine ni dola tano sisi dola 25 halafu tunasema tunataka tuvutie uhusiano wa kibiashara, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachotaka Mheshimiwa Waziri utakapofika mahala unafanya majumuisho unisaidie, nini mkakati wenu katika soko kubwa hili la watu karibu milioni sita ambalo tunalitegemea, nini, mkakati wenu wa kupunguza gharama ya visa ili tuweze kufanya nao biashara vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hilo nilitaka kuzungumzia tumekuwa sisi ni mafundi wa kuanzisha uhusiano, nilitaka kuuliza hivi uhusiano wa sisi na Msumbiji tukaanzisha mpaka ile TAMOFA imekwenda wapi? imekufa au ipo na hawa Msumbiji ni ndugu zetu naweza nikasema ni ndugu zetu wa damu, tukishirikiana nao tunakuwa tuna uhakika tupo katika mikono salama, uhusiano huu umekwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuzungumzia diaspora na uraia pacha; ibara ya 132 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi imezungumza namna ambavyo tutawashirikisha diaspora katika kusaidia suala la diplomasia ya uchumi na kusaidia uwekezaji katika nchi yetu, tumeeleza, siwezi kunukuu hapa nitachukua muda mrefu, lakini ipo kwenye ibara ya 132.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati tunazungumza kuwashirikisha sijui tunapata kigugumizi wapi cha uraia pacha na katika hili nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja kufanya majumuisho unisaidie nini kigugumizi cha uraia pacha? Tuna ndugu zetu, tena hawa mbali na kuwa na wana mitaji kama alivyosema dada yangu hapa Mheshimiwa Ng’wasi muda mfupi, wengine wana-technology, wana maarifa, wakiyaleta hapa nchini tutanufaika, kigugumizi kinatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba sana, sana wakati tunazungumza diplomasia ya uchumi tuone jinsi ya kuwatumia diaspora kutusaidia katika suala la uwekezaji na maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, narudia kukushukuru, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)