Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kutujalia jioni hii ya leo uzima na afya kuweza kuzungumza machache kuhusu Wizara yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mama Samia, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchagua safu makini katika Wizara hii ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kwa kweli Mheshimiwa Balozi Mulamula na Mheshimiwa Balozi Mbarouk, hawa ni watu wabobezi ambao wanajua diplomasia ya kidunia. Kwa hiyo, ni jambo la kumshukuru Mwenyezi Mungu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo, mimi mchango wangu utakuwa mfupi tu ambao sanasana utakumbusha ziara ambayo imewahi kuandaliwa kama sikosei, mwaka 2019. Ubalozi wetu ulioko kule Abu Dhabi ukishirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje uliandaa ziara ambayo aliyekuwa Rais wa Zanzibar wa Awamu ya Saba, Dkt. Ali Mohamed Shein, alifanya ziara katika nchi zile za Falme za Kiarabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na miongoni mwa matunda ambayo yamepatikana katika ziara ile ni kupatikana kwa ahadi ya msaada kwa Zanzibar, msaada wa dola za Kimarekani zisizopungua milioni kumi ambazo zingesaidia wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wadogo wa Zanzibar kwa ujumla. Dola Kimarekani milioni kumi si pesa ndogo kwa nchi kama ya Zanzibar, ni pesa ambazo zingeweza kuzunguka na zikasaidia pato la nchi na uchumi wa nchi kwa ujumla; kwa hiyo hili lilikuwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, katika Mfuko wa Abu Dhabi (Abu Dhabi Fund) nao uliahidi kutoa dola milioni kumi hivyo hivyo kwa ajili ya Hospitali ya Wete iliyoko katika Mkoa wa Kaskazini Pemba. Yaani kuifanyia ukarabati mkubwa hospitali ile, lakini pia kuifanyia mambo makubwa, pamoja na kuleta vifaa tiba pamoja na dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo ninachokumbusha ni kwamba msaada ule kila kitu mwaka 2019 walishakuweka saini ule mkataba, kilichobakia ilikuwa maafisa wale wajumbe wa mifuko ile wa Khalifa Fund pamoja na Abu Dhabi, waje Tanzania Zanzibar ili kukagua miundombinu na namna gani zile pesa watakazozileta zitatumika vipi, lakini kwa sababu ya mlipuko wa Covid duniani, basi mpaka leo hawakuweza kuja katika nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokumbusha ni kwamba Ubalozi wetu wa Abu Dhabi ukitiwa hima na Wizara yetu hii basi waweze kuhimiza, kukumbusha na kuwaambia Tanzania sasa iko salama kwa Covid-19. Kwa hiyo, waje wakague ili baadaye watupatie pesa hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba katika Bunge lililopita tulikuwa na mvutano kidogo hapa wa nani anahusika kuweka saini katika msaada fulani wa kujenga barabara iliyoko Pemba vilevile; kutoka Wete – Piki – Melitano – Chakechake. Tuliambiwa watu wa ADB pamoja na Saudi Fund walikuwa tayari watoe msaada wa kujenga barabara ile ambayo ni muhimu sana katika maendeleo ya uchumi wa Pemba kwa mazao ya biashara pamoja na mazao ya chakula. Lakini mpaka leo tunasikia danadana, hatujui msaada ule umekwama wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninamuomba Mheshimiwa Waziri akija hapa aki-summarize basi atueleze nini position ya msaada ule wa kuijenga barabara hii ya Wete, wanaita barabara ya Njia Kongwe kufika Melitano mpaka Chakechake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kadhalika pia tumeona katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri akizungumza kwamba China wako tayari kusaidia ujenzi wa barabara kuu za Zanzibar, kilometa 148. Lakini hakukuwa na ufafanuzi. Kwa hiyo, tunamuomba Waziri pia akija hapa atueleze ni barabara zipi hizo ambazo China watatusaidia na lini tunategemea kuanza kazi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, mimi nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia kwa kuwateua majembe mawili makubwa haya. Tunasema kama Wizara hii ni upele basi upele umepata mkunaji. Kwa hiyo tunawatia moyo, waendelee kuchapa kazi ili maendeleo ya nchi hii kupitia Wizara hii yapatikane. Ahsante sana (Makofi)