Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami naomba nishukuru kwa kupata fursa hii ya kuchangia Wizara hii muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kujikita kwenye habari baadaye nitakwenda kwenye michezo na kama muda utaniruhusu, nitamalizia kwenye utamaduni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa habari naomba niongelee hili Shirika letu la Utangazaji la Taifa - TBC. Maeneo mengi ya Mkoa wetu wa Tanga hayana usikivu, kwa mfano kwa maeneo kama vile ya Mkinga, Mlalo na Bumbuli wanasikiliza sana redio za Kenya kuliko za Tanzania. Kwa hiyo hali hii ni ya hatari sana, wale watu wanakosa mawasiliano kabisa na kama tunavyojua, mawasiliano ni jambo muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la TBC kwa maeneo hayo walifunga minara yao kwa Kata za Mnyuzi na Kwemshai maeneo ya Korogwe na Lushoto. Lakini sasa maeneo ya Mlalo na Bumbuli yako nyuma ya mlima, kwa hiyo hayapati mawimbi hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mawaziri waliopita walikwenda mara kadhaa wakaahidi kushughulikia suala hilo lakini mpaka sasa halijashughulikiwa. Kwa hiyo, niiombe Wizara itukumbuke watu wa Mkoa wa Tanga kwa maeneo hayo ambayo hatuna usikivu waende wakarekebishe mitambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia cha kushangaza ni kwamba hapo awali maeneo hayo yalikuwa yanakamata lakini baada ya kutoka kwenye mfumo ule wa analogue kwenda kwenye mfumo wa digital wa fm ndiyo yamepoteza usikivu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapo nashindwa kuelewa, kwa nchi nyingine wakitoka kwenye mifumo ya zamani wakiwa wanaboresha mifumo yao kwenda kwenye mifumo mipya ndiyo wanafanya vizuri zaidi. Lakini sasa ni tofauti sisi kwa nchi yetu, yaani tulivyokuwa kwenye analogue maeneo yale yalikuwa yana usikivu na tulikuwa tunakamata vizuri hizo redio. Lakini baada ya kufanya marekebisho yale kutoka kwenye hizo short waves kwenda kwenye fm, maeneo yale yamepoteza usikivu. Kwa hiyo niiombe Wizara iende katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo kwenye Shirika letu hili la Utangazaji la TBC, naona kama bado vifaa vyao vingi si vya kisasa; naomba wapatiwe vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, waandishi wetu wa habari naona maslahi yao bado ni madogo mno, tuangalie namna ya kuongeza maslahi ya waandishi wa habari. Wanafanya kazi kubwa na ni kazi ngumu mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona hata tunapokuwa kwenye misafara ya viongozi, wakati viongozi wanakimbia na zile V8 nao wanakimbia na magari yao na wanatakiwa kuwahi pale tukio likitokea, kila kituo mnachohama yaani unaona wanavyopata taabu na wanavyoomba lift kwenye magari ya viongozi. Kwa hiyo, naomba sana pia waandishi wa habari waangaliwe kwa upande wa maslahi na upande wa vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye michezo. Michezo ni ajira, michezo ni afya na michezo ni uwekezaji pia. Lakini nimesikiliza vizuri hotuba ya Wizara hapo asubuhi, hoja yao moja kubwa, walisema mkakati mmoja wapo wa Wizara ni kuongeza ushiriki wa michezo kwenye ngazi za shule na jamii. Nafikiri ndiyo mkakati wao mmoja mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sasa kuongeza ushiriki tu peke yake haitatosha kama Wizara haitashirikiana na Wizara nyingine kama vile TAMISEMI na Wizara ya Elimu. Kwa sababu samaki mkunje angalia mbichi; vipaji vinaandaliwa watoto wakiwa bado wadogo na watoto wetu hawa kwa muda mwingi huwa tunawakabidhi shuleni, tunawakabidhi kwenye Wizara ya Elimu. Mpaka mtoto yule anaporudi kwako, kama mara nyingi anavyosema Mheshimiwa Jumanne Kishimba ambaye leo nafikiri hayuko hapa anasema tunakukabidhi mtoto yule akiwa mdogo unakuja kunirudishia mtoto akiwa mkubwa na hajui chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sasa huku shuleni kuna michezo na kwenye shule zote za Serikali huwa kuna pesa zile za capitation. Pesa zile zinaingizwa kila mwezi na ni pesa nyingi sana ambazo kama tungezisimamia vizuri, Wizara ya Michezo nayo ingekuwa inafuatilia, wakashirikiana na Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI, nafikiri tungeibua vipaji vingi vya watoto wakiwa kuanzia wadogo mpaka tukawaendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mdogo tu, tuchukulie tuna shule za msingi na za sekondari 20,000 zote jumla, na ziko zaidi ya hizo, na kila shule kwa mfano mimi nilikuwa mwalimu, kwa mwezi shule yangu ilikuwa inapokea shilingi 243,000 pesa za michezo kila mwezi kwenye kila shule ya Serikali ni asilimia kumi, unatenga pembeni, pesa ile ya capitation ambayo ilikuwa ni kama elfu ishirini na kitu hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukichukua tu ile 20,000 mara shule 20,000 ni pesa nyingi sana, ni millions of money na huo ni mwezi mmoja, sikwambii mwaka mzima, sikwambii miaka mitano. Ni billions of money tunapeleka pesa za michezo kwenye kifungu kile cha capitation lakini hakuna vipaji vinavyozalishwa huko kwa sababu kwanza hakuna vifaa, hakuna viwanja na wale wanafunzi hawana lishe, hawawezi wakashiriki michezo wakiwa na njaa, tutakuwa tunajidanganya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapohapo kila mwaka tuna mashindano ya UMISETA na UMITASHUMTA. Yale mashindano yapo toka enzi kwa hiyo sasa hivi yamekuwa tu ni kama mazoea. Tulitarajia pia kupitia mashindano yale ya michezo shuleni kila mwaka, pale ndiyo tungekuwa tunaibua wanafunzi ambao wanapenda michezo, ni rahisi sana kuwasoma pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mashindano yale huwa yanaanza ngazi za shule Tanzania nzima, yanakwenda ngazi ya Wilaya Tanzania nzima, ngazi za Kata, ngazi ya Kkoa na baadaye wanafunzi wanapelekwa Taifani. Na maeneo yote humo inakopita kwenye hiyo michakato wanafunzi huwa wanalala kambini na wanachangiwa chakula na baadaye wanafunzi wanafika mpaka mwisho Taifani tunapata washindi wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya kupata wale washindi wa Kitaifa kila mwaka, hawaendelezwi na wala Serikali haitambui chochote. Na ukimuona kama kuna mchezaji ambaye ameibuka yaani ni yeye mwenyewe juhudi zake mwenyewe, usifikiri kwamba kuna jitihada za Wizara pale, hapana. Kwa asilimia kubwa wanaoibuka; si wasanii, si wachezaji, si kwenye vikundi vya ngoma, ni jitihada zake mwenyewe. Ni mwanafunzi tu alikuwa na interest ya michezo, akitoka shule anakwenda kwenye viwanja vya vumbi, anacheza na baadaye anakuwa mchezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni wakati sasa wa Wizara hizi tatu kushirikiana, hizo pesa zisipotee. Tunaweza kuibua wachezaji wengi sana kupitia pesa zile na Wizara yenyewe ikifanya jitihada. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Wizara, tunaweza tukajenga shule za kanda; ni ngumu sana kujenga shule za michezo katika kila mkoa, lakini tunaweza angalau tukaanza na kanda. Kwa hiyo, wale wanafunzi tukishakuwa tumewachagua kwenye zile UMITASHUMTA na UMISETA, ni vizuri sasa wale wakawa historia yao vizuri, ndiyo mana nasema hizi Wizara zishirikiane.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Wizara ya Elimu ndiyo yenye watoto, Wizara ya TAMISEMI ndiyo yenye miundombinu ambayo ndiyo tunaweza tukawaomba baadaye wakatusaidia kujenga shule hizo. Kwa hiyo, naomba niishauri Serikali tunaweza tukafikiria kujenga shule hizo za kikanda lakini pia tunaweza tukaboresha viwanja vyetu shuleni pamoja na kuboresha lishe ku-promote michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nashukuru sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)