Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi, awali ya yote niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo kwa uwasilishaji pamoja na timu yake yote. Lakini pia Kamati; lakini kipekee kabisa niipongeze Serikali kwa mwaka huu wa 2021 kwa kupeleka michezo ya UMITASHUTA pamoja na UMISETA katika Mkoa wa Mtwara kwa sababu kwa kufanya hivyo inafungua milango ya fursa kwa Wana Mtwara, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende sasa kwenye mchango, Tanzania wote tunatambua kwamba imekuwa ikishiriki mara nyingi kwenye michezo mbalimbali ya kitaifa pamoja na kimataifa. Kuna wakati huwa tunafanya vizuri, lakini kuna wakati hatufanyi vizuri sana. Lakini ukiangalia ni kwa nini hatufanyi vizuri sana kuna sehemu kuna gap.

Mheshimiwa Spika, Tanzania pamoja na Serikali yake kwa ujumla imekuwa ikiwekeza fedha nyingi katika maandalizi ya michezo ya UMISETA, pamoja na UMITASHUTA jambo ambalo ni jema kwa sababu tunataraji wanamichezo hawa ambao wanaenda kucheza michezo ya kimataifa watokane na maandalizi ambayo yanafanyika katika michezo ya UMISETA pamoja na UMITASHUTA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukianglaia Serikali inatenga shilingi 600 kwa wanafunzi wa shule za msingi kila mwanafunzi mmoja kwa ajili ya maandalizi ya UMITASHUTA na shilingi 1,500 kwa ajili ya wanafunzi wa shule za sekondari, ni jambo jema tunawashukuru na kwa kweli wanafunzi wanahamasika na wanafanya vizuri. Niwapongeze TFF kwa sababu wakati wa michezo hiyo wamekuwa wakiwabaini wanafunzi wanaofanya vizuri wanawaweka kwenye database yao pamoja na CHANETA na watu wa basketball.

Mheshimiwa Spika, lakini pale michezo ambayo inashindanishwa ni mingi ipo pia michezo ya ndani wale wa michezo ya ndani sijaona mkakati madhubuti wa Serikali kuwashirikisha au kuwachukua katika database yao ili waweze kuwatumia baadaye. Nishauri sana Serikali kwamba michezo ya ndani ni sehemu ya michezo na yenyewe ichukuliwe kwa uzito wake Watoto wale nao wapate kushiriki katika michezo mingine hapo baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wale wanafunzi wanaomaliza wanaoshiriki michezo ya UMISETA pamoja na UMITASHUTA wakishamaliza shule hakuna wanakoelekea, wamejitahidi wamefanya vizuri, wamemaliza masomo yao wanarudi wanakaa nyumbani hakuna muendelezo wa michezo kwa wanafunzi wale. (Makofi)

Sasa swali la kujiuliza ni kwamba Serikali iliwekeza kwa kiasi kikubwa, wanafunzi wakajitoa, maandalizi yakafanyika, lakini mwisho wa siku fedha za Serikali ambazo zimeenda kuwekeza katika michezo hiyo hazileti tija kwa sababu wanafunzi wanapomaliza hakuna wanakoelekea tena ukiondoa wale wachache wa football, netball pamoja na basketball.

Kwa hiyo, niombe Serikali sasa iwe na mkakati madhubuti wa kuhakikisha wale wanafunzi wanaomaliza shule wanachukuliwa au wanaendeleza michezo yetu mbalimbali ili baadaye iweze kutuletea tija katika Taifa katika fani hiyo ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niongelee pia suala la utamaduni; hii ndiyo Wizara ambayo inasimamia kwa ujumla masuala yote ya utamaduni, utamaduni kwa maana ya vyakula, maadili na mambo yote yale ambayo yanakusanyika huko, lakini tumeona mmomonyoko mkubwa sana wa kimaadili sasa hivi katika nchi yetu. Niiombe Wizara kwa sababu ni Wizara ambayo ina vyombo vya habari; ina television pamoja na magazeti na redio kwa kupitia vyombo vyake vya habari waanze kurejesha au watoe elimu kuhusiana na suala la maadili katika nchi hii, hali iliyoko ni mbaya hata Mheshimiwa Rais alisema wakati anaongea na wazee wa Dar es Salaam, mwanafunzi au kijana amekaa kwenye kiti, lakini hampishi mama mjamzito wala wazee na hiyo inatokana na mmomonyoko wa maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutumie vyombo vyetu tulivyo navyo kutoa elimu ili suala la maadili liweze kuendelezwa katika nchi hii. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Maimuna Mtanda.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)