Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu. Kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na team yake nzima ya wataalam inayoongozwa na Katibu Mkuu mzoefu Dkt. Meru. Nawapongeza kwa kutuletea Mpango mzima na mzuri wa mwaka huu 2016/2017. Hotuba yako imefafanua vizuri kwa muhtasari kabisa mwelekeo wenu kwa bajeti hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipongeze Serikali yetu kwa kuona umuhimu wa kuwa na uchumi wa viwanda. Mimi binafsi naona ni hatua kubwa sana na mwelekeo ni mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri masuala machache ili yafanyiwe kazi katika kuboresha dhana nzima ya uchumi wa viwanda. Tanzania suala la viwanda linawezekana sana. Tuna rasilimali nyingi na fursa ya malighafi za aina mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni muhimu, Wizara ya Viwanda, Biashara iwe ndiyo Wizara inayoratibu masuala yote ya biashara na uwezeshaji. Iwe ndiyo kiunganishi (coordinator) baina ya Wizara zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kodi na tozo zinazotozwa na Serikali na taasisi za udhibiti (Regulatory Bodies) pamoja na Serikali za Mtaa. Nyingi hujirudia na shughuli za taasisi za udhibiti hujirudia. Tunashauri nyingi ziondolewe au kupunguzwa na pawe na One Stop Center wakati wa malipo na wakati wa ukaguzi wote kama team moja ya Serikali na siyo kila taasisi kwa wakati wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Regulatory Bodies zisitoze na badala yake Serikali itoe bajeti za kuziendesha na itoze kwa wafanyabiashara sehemu moja na kugawa kwa taasisi hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nashauri pia tuwe na mfuko maalum wa kupata fedha za utafiti. Fedha za utafiti kila mwaka ni ndogo sana. Bila utafiti katika sekta zote hatutasonga mbele. Nashauri kwa kuanzia tutoze shilingi 50 kwa kila lita ya mafuta kwenda kwenye mfuko huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji wa ndani wapo na wanahitaji msaada wa utafiti ili waweze kuwekeza katika viwanda vidogo na kati. Mitaji kwao siyo shida bali ushauri wa kitaalam na msaada wa kufuata sheria na kanuni ili waweze kuwekeza. Wizara ya Viwanda na Biashara inaweza kusaidia kufanya kazi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni katika eneo la uwekezaji wa kimkakati (strategic flagship investments) ya 2015 - 2020. Nashauri suala la Kiwanda cha Mbolea inayoendana na gesi asilia (Urea plant) ili tuweze kuzalisha aina zote za mbolea hapa nchini badala ya kuagiza urea ambayo ni moja kati ya msingi (foundation compound) ya mbolea zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali iangalie namna ya kukuza Sekta ya Biashara ya Mbegu ndani ya nchi. Tulikuwa tumefikia katika hatua nzuri sana kabla ya miaka ya 2004. Baada ya sera kubadilika na kutotoa fedha za kutosha katika taasisi zetu za utafiti na kuondoa kodi na tozo zote katika uagizaji wa mbegu za nje na kuendelea na kutoza uzalishaji wa ndani kwa aina zaidi ya kodi na tozo 26, sekta hii ilidorola na wazalishaji wengi wa nje walihamia nchi zinazopakana na sisi kuzalisha mbegu huko na kuleta nchini bila kodi na tozo yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii pia ni kwa Sekta ya Madawa ya mimea na mifugo ambapo uzalishaji wa ndani hutozwa kodi na tozo nyingi lakini bidhaa hiyo hiyo kutoka nje haina kodi wala tozo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Wizara iangalie namna ya kuwa na Ofisi za BRELA kimkoa, tuanze na ofisi katika Kanda. Leo hii ingawa ipo online lakini bado ni lazima ufike ofisi za Dar es Salaam kupata huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishauri Serikali iangalie namna ya kuboresha huduma katika viwanja vya Kilimanjaro, Dar es Salaam na Songwe. Leo hii mazao ya Sekta ya Mboga Mboga (horticulture) ya Kanda ya Kaskazini yote hupitia Kenya (Nairobi) badala ya KIA. Je, utafiti umefanywa kuwa tatizo ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninashauri kama sababu ni biashara, tuangalie namna ya kuunganisha bodi zote za mazao kuwa moja na kila zao liwe na idara katika bodi hiyo. Hii itasaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa bodi hizo na pia wataalam waliobobea katika biashara ndio waongoze bodi na siyo uwakilishi wa kisiasa na uwakilishi sababu tu ya uwakilishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba bodi hiyo moja iangalie namna ya kusaidia sekta husika bila kuwatoza. Gharama za kuendesha itokane na uwekezaji na faida itakayotokana na biashara ya kuhudumia sekta hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Serikali iangalie namna ya kuondoa kodi kwenye vifaa na mitambo ya ujenzi na kuchimba maji zinapoagizwa (import duty and VAT on earth moving equipment and drilling equipment) na itoze kwenye shughui za kazi na siyo kwenye uagizaji. Hii itafanya ziwe nyingi nchini na zikiwa nyingi ushindani utakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashauri ili kulinda viwanda vya ndani, tutoe kodi ya VAT kwenye mafuta yanayozalishwa ndani ya nchi na tutoze mafuta ya kupikia yanayoagizwa kutoka nje. Pia tutoze tozo maalum kwenye concentrates za juice zinazotoka nje na tozo hiyo itumike kuboresha kwa kuagiza miche ya matunda tuzalishe ndani ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutoze dumping charge kwenye chuma. Leo hii viwanda vyetu vitafungwa kutokana na mzalishaji mkubwa duniani kuleta chuma kwa bei nafuu. Wanafanya dumping kumwaga kwa bei ya chini ya gharama za uzalishaji wa viwanda vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iangalie upya sera ya kulinda viwanda vya ndani badala ya kuangalia upatikanaji wa kodi inayotokana na uagizaji wa bidhaa kutoka nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu Wizara ya Viwanda na Biashara ibadilike na wataalam wake badala ya kuwa wakusanyaji wa kodi na tozo tu, wawe washauri wa wafanyabiashara na wanaotarajia kuwekeza; wawe washauri katika kila sekta kwa kufanya utafiti na kushauri jinsi ya kuboresha sekta hiyo; jinsi ya kupunguza gharama, kupata mitaji, kupata teknolojia mpya na masoko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, coordination and advice hii iwe katika kila ngazi kuanzia Wilaya, Mkoa na Taifa. Wafanye utafiti katika gharama mbalimbali na tozo na kuishauri Serikali namna ya kuboresha biashara ya ndani na nje ya nchi.
na elimu ya kodi. Wizara pia inaweza kusaidia kutoa elimu hiyo. Muhimu hapa ni mindset change kuwa na mabadiliko katika fikra.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara itumie Sheria ya PPP (Public Private Partnership) kufanikisha maendeleo ya biashara nchini na kuboresha mfumo ili uwekezaji ufanyike kwa tija. Naamini Waziri na team yake nzuri ya wataalam wanaweza na wataongoza mabadiliko ya kuelekea katika uchumi wa viwanda. Naunga mkono hoja.