Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Nashukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika wizara muhimu ya Viwanda na Biashara na niseme tu wizara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwa kuanza na Ripoti ya Benki ya Dunia iliyotolewa mwaka 2020 ambayo ripoti hiyo imeitaja Tanzania kuwa imeshika nafasi ya 141 kati ya nchi 190 kwa urahisi wa kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka sita mfululizo sasa Tanzania imeweza kushika nafasi mbalimbali kama ifuatavyo ambavyo nitakwenda kuzitaja. Kwa mwaka 2015 Tanzania iliweza kushika nafasi ya 131 kati ya nchi 190; lakini kwa mwaka 2016 Tanzania imeweza kushika nafasi ya 139 kati ya nchi 190; kwa mwaka 2017 Tanzania ilifika nafasi ya 132 kati ya nchi 190; kwa mwaka 2018 Tanzania imeweza kushika nafasi ya 137 kati ya nchi 190; kwa mwaka 2019 imeshika nafasi ya 144 kati ya nchi 190 na kwa mwaka 2020 Tanzania imeweza kushika nafasi ya 141 kati ya nchi 190. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja nafasi hizo ambazo Tanzania imeshika lakini bado hatujafikia lengo la Tanzania kushika nafasi ya tarakimu mbili. maana yake lengo letu tulikuwa tushike walau kutoka 99 kushuka chini mpaka moja, lakini hatujaweza kufikia lengo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini hatujaweza kufikia lengo hili? Hii yote inatokana na mazingira magumu yaliyojitokeza ndani ya miaka mitano ya wafanyabiashara wetu kufanya biashara. Ndani ya miaka mitano wafanyabiashara wamefanyabiashara kabika mazingira magumu sana na mazingira hayo yamepelekea wengi kufunga biashara zao. Lakini hata wengine waliotamani kufungua biashara wameshindwa kufungua bisahara kutokana na masharti magumu yaliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hiyo imeathiri sana, ninaweza kuzungumzia hasa wa mikoa iliyoko mpakani. Mimi ninatokea Mkoa wa Songwe ambao uko mpakani mwa Tanzania na Zambia. Ukifika pale Tunduma ni mpakani, sasa hivi asilimia kubwa wamefunga maduka yao kutokana na changamoto kubwa ya biashara. Na hii yote inatokana na mlundikano mkubwa wa kodi ambao wafanyabiashara wengi wameshindwa kuumudu badala yake wamekimbia na kwenda kuwekeza kwenye nchi jirani ya Zambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ukienda upande wa Zambia, asilimia 60 ya wafanyabiashara wakubwa walioko Zambia ni Watanzania. Ukienda jioni pale Nakonde, Black maduka makubwa yote yanamilikiwa na Watanzania na Watanzania wamekwenda kuwekeza kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna sababu ya kufanya mabadiliko sana na siku zote nimeendelea kusema kinachopelekea yote hayo ni mlundikano mkubwa wa kodi, tuna sababu kubwa sana na siku zote tumeendelea kusema kufanya marekebisho ya kodi, ya Sheria za Kodi. Marekebisho hayo tukiyafanya wafanya biashara wetu wataweza kufanya biashara kwa uhuru. Sasa hivi tunapata faida gani kama Watanzania wanakwenda kuwekeza nchi jirani, lakini huduma zote wanakuja kuzipata Tanzania. Tukizungumzia barabara wanakuja kunufaika Tanzania, tukizungumzia maji, afya wanakuja kunufaika Tanzania, lakini wakati huo wamekwenda kuwekeza katika nchi jirani ambapo Tanzania hatupati faida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Zambia kule mfanyabiashara ataulipia mzigo wake wakati wa kuujumua. Atafanya biashara kwa uhuru hata bughudhiwa na jambo lolote, lakini ukija Tanzania mlundikano wa kodi unawakimbiza wafanyabiashara wetu. Siwezi kutaja kodi moja moja, lakini nitasema tu kwa ufupi. Ukija Tanzania mfanyabiashara ili afanye biashara yake kwanza jambo la kwanza atatakiwa kuisajili biashara yake, na kwenye suala zima la kuisajili biashara sio bure, kunatakiwa fedha. Akishaisajili anatakiwa kulipia kodi TRA, huyo huyo mfanyabiashara mmoja. Lakini baada ya hapo kuna kodi ya zuio anatakiwa kuilipia huyu huyu mfanyabiashara. Baada ya hapo ya kodi ya zuio, kuna kodi nyingine nyingi ambazo zingine ni kodi yaani anatoa kodi kadri anavyopata wateja anatakiwa kulipia kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna gharama za OSHA huyu huyu mfanyabiashara anatakiwa kulipia; kuna leseni za biashara kwenye Manispaa na Halmashauri zetu huyu mfanyabisahara anatakiwa kulipia; kuna Zimamoto kuna mambo mengi ya kodi mlundikano umekuwa ni mkubwa wa kodi na mlundikano huu unasababisha wafanyabiashara wetu wanashindwa kuwekeza kwenye Taifa letu na badala yake wanakwenda kuwekeza kwenye mataifa jirani. Ni dhahiri kwamba hata mataifa yetu jirani na yenyewe kwenye ushindani wa kibiashara. Kwa hiyo, yanatafuta kila njia kuhakikisha kwamba yanawashawishi Watanzania kwenda kuwekeza huko kwao, tuna sababu ya kufanya marekebisho ya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda kununua tv ya shilingi 500,000 ukimuomba mwenye duka akupunguzie anakuambia wazi kabisa bei yangu halisi ni shilingi 425,000, ukitaka nikuuzie 425,000 sitakupa receipt. Maana yake hapo kodi katika hiyo tv moja ya shilingi 500,000 ni shilingi 75,000.

Sasa Mtanzania yupi ambaye atakubali kutoa shilingi 500,000 asikubali kutoa shilingi 425,000 kwa hiyo watu wanakubali kununua vitu bila receipt ili kukwepa hiyo shilingi 75,000 kwasababu anajua itamsaidia katika masuala mengine. Na badala yake tumeendelea kuzikosa hizo kodi. Ni lazima tukubali kufanya marekebisho ya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie wawekezaji, wawekezaji wanapokuja kuwekeza kwenye Taifa letu kumekuwa na mzunguko mkubwa sana na usumbufu mkubwa wao kupatiwa vibali vya uwekezaji na nafasi hiyo imepelekea wengine kukata tamaa, mwekezaji anafuatilia kibali mpaka miaka miwili, mitatu anaendelea kufuatilia kibali cha uwekezaji, mwisho wa siku anaamua kukata tamaa anakwenda kuwekeza kwenye mataifa mengine ambapo anaona kuna uwalau hakuna usumbufu. Lakini usumbufu huu umesababisha mianya ya rushwa, badala yake kumekuwa na mianya mikubwa ya rushwa mtu anajikuta mpaka anapatia hicho kibali lazima atoe rushwa. Sasa tunajitengenezea sisi wenyewe mianya ya rushwa kwa wawekezaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la viwanda. Katika suala zima la viwanda NSSSF waliamua sijui nizungumzieje hapa, yaani Mifuko ya Hifadhi ya Jamii waliamua kujiwekeza katika suala zima la ufufuaji wa viwanda. Na waliweza kutoa takribani shilingi bilioni 339 kwa ajili ya kufufua viwanda 12. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua, Serikali ina mkakati gani ama imeweka malengo gani kuhakikisha fedha hizi zinarudi ili kutokuwatesa wastaafu wetu. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja atuambie jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo mwisho ni suala la teknolojia. Ninaamini kabisa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia maana yake kengele imeshapiga malizia sentensi yako.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, aaah, ni refu sana. Nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante. (Makofi)