Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nashukuru sana kwa kunipatia nafasi, mimi kwanza niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya yeye na watumishi wote katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji aliyekuwa akichangia/aliyemaliza sasa hivi naye amekumbushia suala la Kiwanda cha Vifaa Tiba katika Mkoa wa Simiyu hasa vifaa vinavyotokana na zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni tatizo ni nini, nani kakwamisha kibali hivi kama sisi tunataka nchi iwe ya viwanda sisi wenyewe tena tunakuwa vikwazo maana yake nini. Naiomba Serikali mjitahidi kuhakikisha kwamba kiwanda hiki cha vifaa tiba kinaanza kufanyakazi kwa sababu ndiyo mkombozi wa Watanzania kwa maana vifaa tiba, lakini bado ni mkombozi kwa wakulima wa pamba katika mikoa inayozalisha pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la pamba linalimwa katika mikoa takribani minne, mitano zaidi na bado kuna mikoa mingine zaidi. Mkoa wetu wa Simiyu, Mkoa wa Mwanza, Mkoa wa Shinyanga, Mkoa wa Mara na Mkoa wa Kagera ni wazalishaji wazuri wa pamba, na sisi katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 tumesema kabisa kwamba tutajikita katika kuhakikisha tunasimamia uzalishaji wa mazao na hasa mazao ya biashara pamba ikiwemo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamba ndiyo mkombozi wa wakulima wa maeneo haya, lakini naomba nikuambie uzalishaji wa pamba huu kila siku umekuwa na maneno, umekuwa na kelele kwa sababu zao la pamba limekosa soko la kudumu. Mkulima wa pamba ananyanyasika miaka yote, sisi kwetu pamba imebadilika imekuwa siyo zao tena la biashara limekuwa zao la kisiasa, is a political crop kwa sababu wewe Mbunge, wewe Diwani unapoomba kura inabidi uongelee maslahi ya zao la pamba ndipo upewe kura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sisi Wabunge tuliomo humu wa mikoa tunayozalisha pamba tukirudi hivi hivi mimi naomba niwaeleze hatutarudi tena humu Bungeni kwa sababu wakulima wengi wa pamba wanaona kama vile hatuwatetei. Zao la pamba linakwenda kuzalisha nguo, market ya nguo iko Tanzania, iko Kenya, iko Uganda nchi zote za Afrika Mashariki wanahitaji nguo na binadamu anapozaliwa leo mpaka kufa kwake anahitaji nguo; ukizaliwa unafunikwa nguo, ukikua unavaa nguo, ukilala unajifunika nguo, ukienda msibani, ukifa tunakuzika umevalishwa nguo. Hakuna product iliyokuwa muhimu kutoka baada ya chakula kinachofata ni nguo na market hii ya East Africa ni kubwa mno. Lakini nguo zinazozalishwa zinaingizwa kutoka nchi za nje na tunalipa kodi kubwa tunatumia fedha za kigeni kupeleka fedha nje na tunalipa kodi hizo na tunaponunua fedha za kigeni tunakwenda kuingiza nguo kwa ajili ya matumizi ambayo ni basic kwa mwanadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamba tunayozalisha asilimia 75 tuna export hebu ona hiyo miujiza yaani raw material inayohitajika kwa bidhaa ambayo ni muhimu raw material yake badala yaku-consume sisi hata Tanzania kuitumia katika viwanda vyetu vya kuzalisha nguo, bidhaa hiyo tuna gin tuna-process kwa asilimia 25; asilimia 75 ya process yaani kwa maana ya mnyororo wa thamani tunaupeleka nje, halafu tukishaupeleka nje tunakwenda kuzalisha ndiyo tuna import tena, haya ni maajabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali msimame na miradi ya kimkakati mlijali suala la zao la pamba kuna mkakati wa CC (Cotton to Cloth) nimeona imekuwa ni maneno tu hatujui mkakati huu ni wa Wizara ya Kilimo, hatujui mkakati huu ni wa Wizara ya Viwanda, hatujui mkakati huu ni wa nani? Tunaomba Serikali mkae muamue leo kwamba tunakwenda kulipa soko zao letu la pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusitegemee wafanyabiashara watutengenezee kiwanda cha nguo, ni lazima Serikali i-invest kwa sababu gani, mnyororo wa thamani wa kutoka pamba kwenda nguo hapa katikati kuna viwanda vingi sana kuna uzalishaji wa pamba, kuna kufanya mambo ya ku-gin, kuna kutengeneza majora na kutengeneza majora kuna kuhitaji hapo katikati kuna process nyingi, hapo kuna utengenezaji wa rangi za nguo, kuna utengenezaji wa label za nguo, pakken material kwa maana ya plastic kuna vitu vingi hapa katikati mjasiriamali mmoja hawezi kutengeneza value chain ya pamba mpaka kwenye nguo ni lazima Serikali intervene, ni lazima Serikali itengeneze miundombinu wa wajasiriamali kila mmoja katika value chain hii ya pamba alenge sehemu moja afanye biashara. Kama ni mtengeneza rangi atengeneze rangi, kama ni mtengeneza vifungo atengeneze vifungo, kama ni mtengeneza uzi atengeneze uzi, kama mtengeneza label atengeneze label, the end of the day hii value chain ikikamilika ndipo unaweza ukatengenezewa shati ukavaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo nguo uliyovaa hapo Mheshimiwa Waziri nguo uliyovaa hapo kifungo ni kiwanda kingine, label ni kiwanda kingine hiyo rangi ni kiwanda kingine viatu ni kiwanda kingine. Kila kitu ni kiwanda kingine bila Serikali ku-intervene ikatengeneza value chain nzima hatuwezi kuwa na cotton to cloth, hiyo strategy yenu haitafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu havihitaji elimu sijui ya namna gani, kwani hamuoni kuna kiwanda kinachotengeneza baiskeli? Baiskeli inatengenezwa na fundi chini ya mti tu, lakini anayetengeneza tairi mwingine, anayetengeneza rim mwingine, anayetengeneza wire, ni mwingine ni Serikali ndiyo inayotengeneza utaratibu huu kama mnasema sijui mnaanzisha sijui industrial park tengenezeni industrial park ya tairi, tengeneza ya spoke, tengeneza ya kengele, tengeneza ya mpira, tengeneza ya wire; the end of the day mtu anakwenda ku-assemble baiskeli chini ya mti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wewe leo mnasema leo mfanyabiashara atengeneze kiwanda cha nguo! Mimi nawaeleza haitawezekana mtu akatengeneza eti nguo kamili ukienda hata pale EPZ Dar es Salaam kuna watu wanatengeneza nguo wana-export wanapeleka Marekani, lakini leo unakuta kifungo kimetoka Malaysia, unakuta sijui majora yametoka India, sijui zipu imetoka sijui wapi, rangi imetoka sijui wapi, ndiyo wanakwenda ku-assemble pale wakisha-assemble ndiyo wanapeleka wanakwenda kuuza sehemu zingine. Serikali na kama mimi leo ningeongea na Mama Samia Suluhu Hassan - Rais wetu ningemwambia aanzishe Wizara inaitwa Textile Ministry, iangalie kutoka pamba mpaka nguo kwa sababu Wizara ya Viwanda na Biashara hamtaweza peke yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hili mlizingatie bila hivyo sisi wakulima wa pamba tutaendelea kulia na wakati tunazalisha pamba nzuri yenye thamani nzuri ambayo sisi kama Serikali tunaomba muiongezee thamani pamba yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani leo pamba tunauza shilingi 1000 tu na bado tukiuza shilingi 1000 mkulima bado analaliwa, mkulima anacheleweshewa fedha, mara tunaanzisha Ushirika, mara sijui tunafanya nini tuna chemka. Tengeneza demand ya pamba katika nchi yetu sisi tuweze kuuza pamba yetu na tuongeze thamani ya pamba yetu, tukauze Kenya, tukauze Uganda, tukauze sehemu zingine. Market ipo binadamu wote wanahitaji nguo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)