Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Kassim Majaliwa Majaliwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote namimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumshukuru Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa wakati wa akizindua Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 20 Novemba, 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, sina shaka kuwa majadiliano ya hotuba hiyo hapa Bungeni yamedhihirisha umakini wa namna Waheshimiwa Wabunge walivyoielewa hotuba ile na umakini uliotumika katika kutayarisha na uwasilishaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Spika na wewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa jinsi ambavyo mmesimamia mjadala huu. Aidha, kwa pekee kabisa, nampongeza Mheshimiwa Mtemi Andrew Chenge ambaye alipata fursa ya kusimamia mjadala wa hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nachukua nafasi hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia mjadala huu wa hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. Aidha, nawashukuru kwa kuunga mkono maeneo mbalimbali yaliyobainishwa katika hotuba hiyo. Kitendo cha kuunga mkono kimeipa Serikali nguvu ya kutekeleza ushauri wa michango mizuri iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuwadhihirishia kwamba michango ya Waheshimiwa Wabunge yote kwa ujumla itasaidia sana Serikali kutekeleza ufanisi zaidi, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 mwaka 2020. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, itasaidia kutekeleza pia Mpango wa Miaka Mitano, kutoka mwaka 2016/2017 kwenda mwaka wa fedha 2020/2021 na Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025. Jumla ya Waheshimiwa Wabunge 171 wamechangia mjadala huu, nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhitimisha hoja hii, siyo nia yangu kujadili tena hoja moja baada ya nyingine kama ilivyotolewa wakati wa Waheshimiwa Wabunge wakichangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, bali nitajielekeza katika ujumla wake. Aidha, Waheshimiwa Mawaziri tayari wameshatoa maelezo ya maeneo muhimu na ambayo yanayotakiwa kuzingatiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya awamu ya tano imeweka msisitizo katika kuhakikisha inarejesha nidhamu katika Utumishi wa Umma kwa kuweka mkazo katika misingi ya uadilifu, uwajibikaji, kutoa huduma kwa wakati na kuchukua hatua za haraka dhidi ya watumishi wote wanaokwenda kinyume na misingi ya utendaji kazi Serikalini.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kuwa Serikali ya awamu ya tano kwa kuzingatia falsafa ya Hapa Kazi Tu, ambayo ilitolewa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, itaendelea kuhakikisha kwamba inawakumbusha kuwa kila Mtanzania anatumia muda wake katika kufanya kazi zaidi na kila Mtendaji Serikalini anatimiza wajibu wake na pia Serikali itahakikisha inachukua hatua dhidi ya wote watakaokiuka maadili ya kazi na sheria zilizowekwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusisitiza kuwa kila mtumishi mahali popote alipo ni lazima atimize wajibu wake ipasavyo. Tunataka kujenga utumishi wa umma wenye kuzingatia uadilifu unaowajibika na watumishi wanaofanya kazi kwa bidii na maalifa na kamwe hatutavumilia mtumishi mzembe na anayefanya kazi kwa mazoea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mjadala wa hotuba ya Mheshimiwa Rais, zipo hoja zilitolewa na Waheshimiwa Wabunge ambazo utekelezaji wake utahitaji kufanya maandilizi ya kutenga Bajeti ya Serikali. Baadhi ya maeneo hayo ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya barabara, mawasiliano, uchukuzi, ikiwemo bandari pamoja na miundombinu ya usambazaji wa maji na nishati.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ipo miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa nchini katika sekta za uzalishaji mali ikiwemo kilimo, mifugo, maliasili, madini na kadhalika na sekta za huduma ya jamii, kama vile elimu na afya ambayo inahitaji pia kukamilishwa wakati huu sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kuwa Serikali itajitahidi kupanga vipaumbele vyake vya Mpango na Bajeti kwa kuzingatia ahadi za Mheshimiwa Rais kuanzia mwaka huu wa fedha na kuendelea. Maoni na hoja za Wabunge zitazingatiwa wakati wowote wa utekelezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa zaidi ni kuomba ushirikiano wa wananchi wote ili utekelezaji uwe wa ufanisi na tija. Ili kutimiza azma ya kutekeleza miradi yote hiyo, Serikali itahakikisha inasimamia ukusanyaji wa mapato yake ipasavyo ili kuwahudumia Watanzania wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika sekta ya kilimo, Waheshimiwa Wabunge wameeleza changamoto nyingi zinazowakabili wakulima ikiwemo kupatikana kwa pembejeo, uchelewaji wake wa kuwafikia pia wakulima wetu. Tatizo la ununuzi wa mazao hasa tumbaku, pamba, kahawa na korosho na huduma chini ya Stakabadhi Ghalani, Serikali imepokea ushauri wa Wabunge na utazingatiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutumia fursa hii kueleza kuwa kutokana na baadhi ya maeneo katika nchi yetu kukumbwa na uhaba wa chakula, uliotokana na aidha uzalishaji hafifu katika msimu uliopita ama kutokana na mazao ya vyakula kusombwa na mafuriko, Serikali inaendelea kutumia akiba yake ya chakula kuhakikisha kwamba waathirika wote wanapata chakula.
Nachukua fursa hii kuwataka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kusimamia kikamilifu ugawaji wa chakula hicho ili kuwafikia walengwa bila ya upendeleo na bila ya kuchepusha na kukipeleka mahali pengine. Aidha, chakula hicho kigawanywe hadharani ili kuondoa malalamiko ya wananchi ili kuhakikisha walengwa wa chakula cha msaada wanafikiwa na kuhudumiwa pia.
Mheshimiwa Naibu Spika, viongozi wakuu na watendaji wa Serikali katika ngazi zote, watoke maofisini kwenda vijijini ili kuhakikisha kwamba kila mwananchi anajishughulisha na shughuli za kilimo kwa lengo la kuzalisha chakula zaidi kwa ajili ya matumizi ya msimu ujao. Wakulima katika maeneo yaliyopata mafuriko wapatiwe mbegu za mazao yanayokomaa haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu usambazaji wa pembejeo, Halmashauri zote zihakikishe kuwa pembejeo zinafika mapema katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za masika na zipelekwe kwa walengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili limesisitizwa vizuri na Waziri wa Kilimo lakini pia Serikali itaendelea kuangalia mfumo bora wa kusambaza pembejeo hizo za ruzuku ili kuondoa malalamiko ya wakulima. Halmashauri na Wizara ya Kilimo wakae kuondoa tozo za ushuru zenye kero kwa mazao yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la maji ni changamoto ya nchi nzima. Ili kuboresha huduma ya maji Serikali itajitahidi sana kutumia mbinu zake zikiwemo kuvuna na kuhifadhi maji ya mvua ili yatumike wakati wa kiangazi. Aidha, Serikali imepanga kuhakikisha kwamba fedha kwa ajili ya miradi ya maji ambayo haijakamilika, zinapatikana na kutumwa kwa wakati katika maeneo husika. (Makofi)
Vilevile Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa wakandarasi wanaopewa kazi za kujenga miradi ya maji, wana uwezo wa kutosha ili miradi hiyo iwe na ubora unaotakiwa na itaendelea kulipa madeni ya wakandarasi na wataalam washauri kama ambavyo imeelekezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo yanayoikabili sekta ya maliasili na utalii yakiwepo ya ujangili wa wanyamapori na nyara, migogoro ya mipaka kati ya vijiji na hifadhi na upotevu wa mapato yanayoshughulikiwa kwa wakati ili kuifanya Serikali hii muhimu kuchangia katika uchumi wa Taifa na kuhifadhi rasilimali hii kwa ajili ya kizazi kijacho. Ushauri uliotolewa na Waheshimiwa Wabunge wote utazingatiwa na wadau wote pia ili kuhakikisha wanyamapori hususan tembo na faru hawaendelei kuuawa na majangili.
Mheshimiwa Naibu Spika, masuala haya ya uvuvi yataimarishwa kwa kuwatafutia wananchi na wadau wa sekta ya uvuvi nchini na kuhakikisha kwamba wanapatiwa vifaa vya kisasa vya uvuvi; kuwatafutia masoko na kuongeza kasi ya uwekezaji katika viwanda vya mazao ya samaki hususan katika ukanda wa bahari kuu na maziwa makuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanya uvuvi katika maeneo ya bahari, maziwa na mito unakua endelevu, usimamizi na doria utafanyika kwa nguvu zote ili kukabiliana na uvuvi haramu. Serikali pia itaendelea kuhimiza wananchi kuanzisha ufugaji wa nyuki kwa kutumia mizinga ya kisasa, lakini pia Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Halmashauri zote nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata mizinga ya kisasa kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima tuzingatie sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kwa mtazamo wa kibiashara zaidi na viwanda kwa lengo la kuwa na viwanda vya kisasa vya kuongeza thamani ya mazao yake. Mkazo utakuwa katika kuanzisha viwanda ambavyo sehemu kubwa ya malighafi itatoka ndani hususan kwenye sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, madini na maliasili nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na migogoro ya ardhi nchini; na malalamiko katika maeneo mengi nchini yanahusu matumizi ya ardhi. Maeneo ambayo yamekuwa yakilalamikiwa ni kati ya wakulima na wafugaji, wananchi kuhodhi maeneo makubwa bila ya kuyaendeleza, mipango miji na ujenzi katika maeneo ya wazi. Serikali imepokea michango mbalimbali ya Wabunge na namna bora ya kumaliza migogoro hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwahakikishia kwamba Serikali kupitia michango yenu itasimamia utekelezaji wa ushauri wenu ili tupate kupunguza migogoro iliyopo. Wizara zinazohusika zitashirikiana na wadau wa sekta ya ardhi nchini ili kubaini vyanzo vya migogoro hiyo na kuipatia ufumbuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali inayo dhamira ya dhati kuona migogoro hii inakwesha. Wito wangu ni kuwa watumiaji wote nchini lazima waheshimu sheria, kanuni na taratibu zilizopo kwenye matumizi ya ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nimeona nielezee haya kwa kifupi kama njia ya kuwaomba sana Waheshimiwa Wabunge wote na wale wenzangu wa upinzani ambao kwa hulka yao waliamua kufanya waliyofanya, lengo letu sote ni kujenga nchi yetu na kuleta maendeleo ya nchi yetu. Tunalo jukumu la kufanya kama wadau ikiwemo Serikali. Sisi kama Wabunge na wananchi wote, tuna wajibu wa kuishauri Serikali jukumu letu ni kuwaongoza wananchi na kutekeleza yaliyomo katika hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nawaomba sana Wabunge wenzangu wa vyama vyote vya siasa na wananchi wote nchini, kutambua wajibu wetu na kwa umoja wetu, kujenga nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sababu na wala siyo busara kubeza juhudi za kila mmoja wetu ambazo zinasaidia sana kujenga nchi yetu. Nawaomba tuunge mkono na tuungane pamoja katika juhudi za kuwaendeleza wananchi na maendeleo yao. Michango yetu na mawazo yenu ndani na nje ya Bunge ndiyo kielelezo chetu kama Wabunge wenye mtazamo wa mbele kwa Watanzania waliotupatia dhamana ya kuwaongoza na kwamba tutatekeleza wajibu wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunayoyafanya hapa Bungeni yawe yanalenga maslahi ya Taifa. Hivyo basi, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge hasa wenzangu wa Kambi ya Upinzani kwamba tunalo jukumu la kufanya jambo ambalo tumepewa deni na wapigakura wetu waliotuchagua, tujitahidi sana kuondoa tofauti zetu kwa maslahi ya Watanzania.
Aidha, sisi wote ni Watanzania, hivyo hatuna budi kufanya juhudi za dhati kudumisha upendo, amani, mshikamano na kusaidiana kwa masilahi ya Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge wote, baada ya kusema hayo, namshukuru tena Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa kunipa nafasi hii ili kusema hayo ambayo nimeyasema kufuatia michango iliyotokana na hotuba ya Mheshimiwa Rais. Kupitia hotuba hii, nimeridhishwa na michango yenu na sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)