Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze wewe binafsi Mheshimiwa Waziri, Naibu wako pamoja na wasaidizi wenu wote kwa namna mnavyoisimamia vizuri Wizara hii nyeti iliyotoa ajira kwa Watanzania walio wengi (75%) na kuchangia 24% ya pato la Taifa. Kutokana na umuhimu huo, na mimi naomba kuchangia yafuatayo:-

Kwanza, Serikali iingie ubia na wawekezaji wa ndani na nje ili kuweza kujenga viwanda vikubwa vya mbolea hapa nchini ili isaidie kupunguza gharama kwa wakulima wetu. Mfano toka Ludewa DAP inauzwa shilingi 80,000 kwa mfuko 24/05/2021, CAN mfuko mmoja unauzwa shilingi 58,000 na UREA ni shilingi 55,000.

Pili, kodi za matumizi ya maji kwa watumiaji wa maji ziangaliwe vizuri ili kodi hizo zisiwe mzigo kwa wakulima na hivyo kudidimiza sekta ya kilimo. Wizara ya Kilimo ikutane na Wizara ya Maji na Mamlaka za Mabonde ili kujadili hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu upatikanaji wa masoko ya mazao ya kilimo; mazao yote ni mazao ya biashara hivyo mtizamo wa kuwa kuna mazao ya chakula na mazao ya biashara unatuchelewesha kuboresha kilimo cha mahindi, alizeti, karanga na ufuta kufanyika kibiashara na kumnufaisha mkulima. Mazao yote haya ni malighafi kwenye viwanda.

Mheshimiwa Spika, Wizara za Serikali zijenge utamaduni wa kukutana na kujadili masuala mtambuka, mfano barabara za vijijini zikiwa bora na zipitike msimu wote hakika zitachangia sana kuinua sekta ya kilimo na viwanda vya uongezaji thamani ya mazao. Wakulima walioko maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao wanakabiliwa na changamoto kubwa za ubovu wa barabara Ludewa. Mfano barabara ya Lusitu-Madilu-Ilininda-Mundindi kuna viazi, chai, kahawa, mahindi, maharage, njegere, mbao na parachichi. Pia barabara ya Kigasi-Milo-Ludende-Amani au Muhoro-Ludende-Mkongobaki-Lugarawa; barabara ya Ludewa- Ibumi-Masimavalafu au Nkomang’ombe-Iwela-Bandari ya Manda na Luilo-Lifua-Liugai na maeneo mengineo.

Mheshimiwa Spika, vyuo vikuu vya kilimo vishiriki kwa vitendo katika kufanya utafiti, ubunifu na kuelimisha wakulima ili kuongeza tija vyuo viendeshe mashamba ya mfano hasa mazao yatakayouzwa nje na kuingiza mapato ya kigeni.

Mheshimiwa Spika, vijana wanaomaliza mafunzo ya JKT wapewe mikopo chini ya uangalizi na waanzishe mashamba ya miwa, alizeti ili kuzalisha sukari na mafuta ya alizeti na karanga.

Mheshimiwa Spika, wahitimu mbalimbali wa vyuo vikuu nao wawezeshwe mitaji ili kujiajiri kwenye kilimo cha kibiashara na kukuza uchumi wa nchi na kujiongezea kipato chao.

Mheshimiwa Spika, Serikali iajiri wataalam wengi wa kilimo na kuwasambaza kwenye kata na vijiji vyetu nao wapewe malengo, wafuatiliwe ili watende kazi kama sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, nawasilisha.