Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa maoni yangu kwa maandishi kama ifuatavyo; kwanza naipongeza sana Serikali hasa Wizara ya Kilimo kwa ushirikiano mkubwa ambao Wilaya ya Kilolo tulipata wakati wa kukarabati scheme ya Ruaha Mbuyuni baada ya mkondo wa maji kuhama kutoka katika scheme hiyo. Kwa namna ya pekee napongeza moyo wa kujituma wa watumishii wa Wizara waliotumwa kufanya kazi ile kwa umahiri na weledi wao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi, napenda kutoa maoni yafuatayo kwa Wizara; nakupongeza wewe Waziri na Naibu Waziri kwa ushirikiano pamoja na Katibu Mkuu na Mkurugenzi wa Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mpango wa Serikali kugawa miche bure kwa mazao ya kimkakati kama ilivyo kwa kahawa na michikichi nashauri Wizara ianze mara moja kuotesha na kugawa miche ya parachichi bure katika Wilaya ya Kilolo ambayo kilimo hicho kinakuwa kwa kasi kubwa na ni mkombozi katika mazao ya biashara. Tayari nimefanya maongezi na Naibu Waziri wa Kilimo na Mkurugenzi wa TARI kuhusu suala hili, hivyo naomba msukumo wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, nafahamu Wizara inazo taarifa kuhusu shamba la chai la Kidabaga ambalo lilikuwa linamilikiwa na TTB na ambalo ni miaka 30 sasa tangu limetelekezwa. Lakini pia katika eneo la Kidabaga na kata za jirani wapo wakulima waliolima chai yao na wanaendelea kusubiri kiwanda cha chai kwa miaka hiyo yote. Hivi sasa kuna tishio la wananchi kung’oa chai hiyo na kupanda mazao mengine baada ya uvumilivu wa miaka mingi bila mafanikio.

Naiomba Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Uwekezaji na Wizara ya Viwanda na Biashara mlete majibu ya ufumbuzi wa kiwanda cha chai cha Kidabaga. Nitashukuru kama kwenye hitimisho lako utakuja na majibu ya suala hili.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Tume ya Umwagiliaji wapo wafanyakazi wa tume wamewekwa kwenye ngazi ya mkoa. Kwa bahati mbaya watumishi wale hawana bajeti na sina uhakika kama wana maelekezo ya kutosha kuhusu kazi zao na uhusiano na Halmashauri zetu. Naomba jambo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, zao la pareto ni kati ya mazao ambayo sasa yanapanda katika soko la dunia, wapo wakulima katika Wilaya ya Kilolo naomba kusiwe na urasimu katika upatikanaji wa vibali vya wanunuzi kwenye zao hili.

Mheshimiwa Spika, kuna magonjwa ya mazao hasa nyanya yamejitokeza ambayo hayakubali dawa zilizopo, naomba timu ya wataalamu itumwe kwa ajili ya uchunguzi.