Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, leo tena naomba kuanza mchango wangu kwenye Wizara hii kwa kuwapongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ya kusimamia Wizara hii nyeti. Hata hivyo naomba kuishauri Serikali katika mambo yafuatayo:-

Kwanza, kwa kuwa tunayo mazao ambayo kitaifa yanaonekana kuwa ni mazao ya kimkakati, ni ushauri wangu kuwa mkakati wa mazao hayo ni lazima uunganishwe na mikakati mingine. Kama vile mikakati ya utafiti ili kuboresha tija ya mazao hayo, uwepo wa miundombinu rafiki ya usafiri ili kuwezesha wakulima wa mazao hayo kuyafikia masoko kwa urahisi.

Mheshimiwa Spika, aidha, kuwepo na mkakati maalum wa kudumu wa kutafuta masoko kwa mazao hayo ya kimkakati utakaowahakikishia wakulima uwepo wa masoko kwa mazao yao. Kwa hali ilivyo sasa masoko ya mazao hayo ya kimkakati sio ya kuridhisha hasa kwa upande wa bei ya mazao hayo.

Pili, kwa zao la korosho ambalo ndio mgongo wa maendeleo kwa Mikoa ya Kusini na Taifa kwa ujumla. Ili kuendeleza zao hilo naiomba sana Serikali kuimarisha kituo chetu cha utafiti pale Naliendele kwa kukipatia chuo hiki fedha za kutosha ili kukiwezesha kuendelea na tafiti mbalimbali.

Jambo la pili naishauri Serikali kuona umuhimu wa kurejesha zile fedha za export levy, fedha ambazo zilikuwa mahususi kwa kuendeleza zao hili la korosho, kwani uzoefu unaonesha kuwa tangu Serikali Kuu kuchukua fedha hizo, uzalishaji wa zao hilo umeshuka sana, hii ni kutokana na wakulima wengi kushindwa kumudu gharama kubwa ya pembejeo.

Nikiendelea kuishauri Serikali katika kuimarisha kilimo chenye tija, liko suala la uhaba wa watumishi wa ugani kwenye Halmashauri zetu, na wale wachache waliopo hawafanyi shughuli za ugani na badala yake wamekuwa wanakaimu kama watendaji wa kata na vijiji na hivyo kusahau kazi zao walioajiriwa nayo. Kutokana na uhaba wa watendaji wa kata na vijiji sehemu nyingi huwatumia wataalamu hawa kama watendaji wa kata na vijiji.

Mwisho niombe Serikali kuifanyia mapitio Sheria ya Ushirika, sheria hii kwa sasa ina mapungufu sana, mfano iko taasisi ya COASCO; taasisi hii badala kuwa mkombozi wa vyama vya ushirika imekuwa adui wa ushirika. Hivyo niombe sana Serikali kuifanyia marekebisho sheria hii ambayo imepitwa na wakati.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa naiomba sana Serikali kuhakikisha bei za mbegu, pembejeo hasa zinazozalishwa nchini zikawa na bei rafiki kwa wakulima. Kwani hadi sasa wakulima wengi bado wanatumia mbegu zao za asili ambazo tija yake kwa mkulima ni ndogo sana na Serikali bado haijawekeza vya kutosha ili kuhakikisha mbegu zinapatikana kwa bei nafuu.