Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuzungumza. Kwanza, napenda kuishukuru na kuipongeza Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya kwa wakulima wetu na kuongeza kasi ya maendeleo katika sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kujikita katika zao la ufuta. Wilaya ya Kilwa ninayotoka ni wilaya ambayo inaongoza kwa kilimo cha zao la ufuta katika Mkoa wa Lindi. Katika zao hili kumekuwa na changamoto kubwa hasa wakati wa minada. Katika mwaka uliopita Wilaya nzima ya Kilwa yenye vijiji 90, kata 23, tulishuhudia tukiwa na kituo kimoja tu cha mnada wa zao hili la ufuta hali ambayo ilipelekea kuwepo kwa biashara ya holela ya zao hili la ufuta almaarufu kule tunaita chomachoma, wenzetu wale wa Kagera nilisikia pale asubuhi kuna kitu wanaita butura. Kule kwetu tunaita chomachoma yaani biashara ya magendo ambayo ina dhulumati nyingi kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, vilevile wapo wakulima walikata tamaa kuuza zao hili wakabaki na ufuta wao mpaka mwaka huu. Hivi napozungumza sasa hivi hawajauza ufuta wa mwaka jana kutokana na hii hali ya kuwa mnada ni mmoja tu na uko eneo la mbali, ambalo ni zaidi ya kilometa 200 toka kule ambako mashamba yaliko. Pia mzunguko wa fedha ukawa umepungua lakini hata bei kwa wale ambao walimudu kupeleka sokoni au mnadani mazao yao walijikuta wanauza kwa bei ya chini sana. Hii ni kutokana na kwamba wale wanunuzi walikuwa wanafidia gharama zao za usafirishaji wa yale mazao toka kwenye vyama vya msingi. Kwa hiyo, kwa ujumla kumekuwa na shida katika huu mfumo wa minada.

Mheshimiwa Spika, jana kulikuwa na taharuki kubwa katika Wilaya ya Kilwa kwa sababu ratiba ambayo ilitumika mwaka jana ndio ambayo jana imetangazwa tena, tuna kituo kimoja tu cha mnada kupitia Chama cha Ushirika cha Msingi cha Muungano kule Kilanjelanje. Naomba Wizara itusaidie kuhakikisha kwamba inaongeza vituo vya minada ili wakulima wetu waweze kuuza mazao yao maeneo ya karibu.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuwa na vituo vingi itasaidia wakulima kushiriki kikamilifu na kuwa na ownership wakati mnada unafanyika tofauti na hali ilivyo sasa. Mnada ukiwa mbali wakulima wanashindwa kuhudhuria mnada badala yake wanakuwa na wawakilishi tu ambao pengine ni viongozi wa vyama vya msingi na hatimaye unakuta hata bei wanayoipata inakuwa ni shida. Kwa hiyo, naomba Wizara ilisimamie suala hili, ile ratiba iliyotolewa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Mwambao iweze kurekebishwa tupate hata maeneo matatu au manne katika Wilaya ya Kilwa ya kufanya minada na kuuza mazao yetu bila shida ili wakulima wetu waweze kunufaika na bei ambazo zinaridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo napenda kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Kilimo ni suala la Kampuni ya Mbolea Tanzania. Katika taarifa ya CAG kampuni hii imekuwa ni miongoni mwa taasisi za umma 11 ambazo zilishindwa kuwasilisha hesabu zake za mwaka kwa CAG katika mwaka wa fedha uliopita. Siyo mwaka huo tu, hata miaka mitano, sita iliyopita kulikuwa na hali kama hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Ndulane Francis, dakika zako zimekwisha.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)