Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara imeleta bajeti ambayo ina mambo mengi mazuri, lakini mimi niseme kama hatuna soko la uhakika, tunapoteza muda na hapa tunafanya ngonjera tu. Huu umekuwa ni wimbo wa kila siku na wewe Spika ni shahidi tumekuwa tukiambiwa tunaleta mbolea, mbegu bora, miche, lakini soko la haya mazao liko wapi? Kwa hiyo, hii ni changamoto kubwa na Wizara lazima ijipange kuhakikisha tunapata masoko. Mkulima amekuwa analima kilimo cha kubahatisha tu, anasema mwaka huu nimelima, lakini sina uhakika wapi nitauza mazao yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni muumini wa ushirika na hii iko kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini niseme kama ushirika hawatakuja na mbinu ambayo itaweza kumnufaisha mkulima, mimi sitaiunga mkono. Tunataka ushirika ambapo mkulima anapopeleka mazao yake aweze kupata pesa yake. Tunataka ushirika ambapo mkulima aweze kutatuliwa matatizo yake sio mkulima anaenda kukopwa. Kwa hiyo, lazima Wizara muwe wabunifu, ukitaka kuleta jambo jema na zuri, lazima uweke vitu ambavyo vitawavutia wale unaowaletea.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi ni kipindi cha msimu wa kahawa. Asubuhi nimepiga simu kuuliza bei ya Uganda kahawa ni shilingi ngapi? Kahawa Uganda sasa hivi ni shilingi 3,500 ya Uganda ambayo kwa kwetu ni shilingi 2,300, lakini kwetu kahawa hiyohiyo ya arabika wanakwambia ni shilingi 1,500. Ukija kwenye kahawa ya robusta ambayo Uganda ni shilingi 2,500 kwetu ukipiga hesabu hela ya Tanzania ni shilingi 1,500 kwetu ni shilingi 1,100.

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho mimi ninakishangaa huyu mkulima wakati anaanza kulima, anaanza kuandaa hii kahawa Serikali huioni popote, lakini kipindi cha msimu unapoanza utashangaa askari wanapelekwa mpakani. Sasa ninataka nikuulize Mheshimiwa Waziri, wewe unasema Uganda hawana bei nzuri, askari wale mnapeleka wa nini mpakani kahawa isiende Uganda? Wewe unasema majirani zetu hawana bei nzuri, sawa ninakubaliana na wewe; kwa nini msimu unapofika ndio mnapeleka maaskari, maana yake kule kuna bei nzuri ndio maana mkulima anakimbilia kule. Kipindi cha msimu kikifika ni kama vita, hili jambo halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana haya mambo ya kuanza kukamata wananchi wanapoanza kuvuna kahawa, ooh, kahawa sijui haijaiva, sisi kule kwetu mtu ana mashamba zaidi ya matatu, analima kwenye kata hii na kwenye kata nyingine, sasa wakikuta unahamisha kahawa yako kuitoa kwenye kata nyingine ambako una shamba unaipeleka kuianika kwako wanasema kahawa unaipeleka Uganda, hili jambo halikubaliki. Kwa hiyo, niombe sana Serikali ijipange kuleta bei nzuri ya kahawa. Tuwe na masoko ya uhakika vinginevyo tunapoteza muda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kiwanda cha TANICA, hiki kiwanda kiboresheni. Mtakapoboresha hiki kiwanda nina uhakika kitaweza kuongeza bei ya kahawa. Kiwanda kinaendelea kubaki vilevile, lakini ninyi kazi yenu ni kutegeshea msimu umefika mnatafuta pesa yenu ya Serikali, hili jambo sio sawa. Kwa hiyo, niombe sana Serikali iboreshe kwanda cha TANICA ili hiki kiwanda kiweze kuongeza bei nzuri kwa mkulima, vinginevyo niombe sana Serikali kama hamjajipanga waacheni wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kitu ambacho siungi mkono ni suala la butura. Hilo mnapambana nalo kwa nguvu zote kwa sababu linamnyonya mkulima, lakini wapeni uhuru wananchi kuuza kahawa wanavyotaka…

T A A R I F A

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa.

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, nalazimika kumpa Taarifa mzungumzaji, mtumishi wa bwana, butura inaingia kwa sababu ya ku-fail kwa mfumo wa ushirika. Butura kwa kwetu ni continuous cash flow, mkulima anahitaji continuous cash flow, anahitaji chenji. Kwa hiyo, akikosa chenji atachukua alichonacho kusudi apate pesa ya kutimiza majukumu yake, anaweza kuuza hata kitanda. Sasa yeye hauzi kitanda anauza kahawa aliyonayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali ilete cash flow, ilete chenji, Wahaya walikuwa wanaita nyantakorakorwa, BCU ilikuwa ina kitu kinaitwa chenji, nyantakorakorwa ndio iliondoa butura. Bila nyantakorakorwa butura itaendelea kuwepo. (Makofi)

SPIKA: Taarifa hiyo inayohusu nyantakorakorwa? (Kicheko)

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, mimi ninachosema napokea hii Taarifa, lakini naishauri Serikali lazima ije na mpango wa kumsaidia huyu mkulima kabla hajauza kahawa yake aweze kupata pesa ya kumsaidia kuendeleza zao hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi nasita kusema naunga mkono hoja kwa sababu bado wakulima wangu wanateseka. Ahsante sana. (Makofi)