Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hii hoja ya Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuishukuru Wizara, kwa sababu katika kipindi cha mwaka wa fedha unaoisha, wameweza kutukarabatia bwawa moja kati ya mabwawa 27 ambayo ndiyo tegemo la Wanalongido katika Kata ya Kimokouwa. Ahsanteni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwanza kuwapongeza kwa sababu najua kazi kubwa wanayoifanya na ugumu wa kazi hii, kwa sababu Wizara hii imeunganisha sekta mbili ambazo zote zinahitaji rasilimali kubwa sana katika kusimamia ili kuweza kufikia malengo ya kiuchumi kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kufanya ulinganifu kidogo wa bajeti iliyotengewa Wizara hii kwenye fedha za maendeleo. Nimeangalia bajeti ya mwaka huu unaoisha; mwaka jana wa fedha (2020/2021) ambao ndiyo unaisha mwezi wa Sita, fedha za maendeleo zilikuwa ni shilingi bilioni 23.4 na mgawanyo wake katika sekta zake mbili; Fungu 64 ambalo ni Uvuvi na Fungu 99 ambayo ni Mifugo ni kama ifuatavyo: mifugo walipewa shilingi bilioni 10.3 na uvuvi walipewa shilingi bilioni 13.05; na walijitahidi kufanya kazi walizozifanya na hizi ni fedha za maendeleo. Returns au maduhuli yaliyokusanywa katika hizo fedha walizowekeza mpaka mwezi huu wa Tano, mifugo wanakaribia kufikia shilingi milioni 40, nadhani wameshafika shilingi milioni 40 kufikia sasa, lakini uvuvi wako chini ya shilingi milioni 18. Sasa utaona kwamba ni kwa jinsi gani hizi sekta zinaweza zikazalisha lakini haziwekezewi mtaji wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu wa fedha bajeti ambayo Waziri amewasilisha leo hotuba yake hapa, jamii yote ya wafugaji Tanzania pamoja na mimi tuna masikitiko makubwa. Kwa nini nasema hivyo? Kwa sababu mwaka huu mmeongeza bajeti ya maendeleo kwa asilimia 80 kutoka shilingi bilioni 23 mpaka shilingi bilioni 116.01, lakini katika mgawanyo kwenye mafungu yake yote mawili, mmeipendelea Sekta ya Uvuvi mkawapa shilingi milioni 99 ambayo ni sawa na asilimia 76 ya fedha yote ya maendeleo mkiaibakizia Sekta ya Wafugaji ambayo nayo ndiyo uti wa mgogo wa watu wengi katika nchi hii, asilimia 14 tu ambayo ni shilingi bilioni 16.8. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni masikitiko makubwa sana kwa sababu katika ukusanyaji wa maduhuli, bado mmeiweka sekta hii kwamba mnatarajia iwape shilingi bilioni
50 na uvuvi iwape shilingi bilioni 33 na wakati huo huo mmeshaona kwamba hata katika fedha kidogo za mwaka unaoisha wa fedha sekta hii ya mifugo ndiyo iliyokuwa inaleta returns zaidi kuliko uvuvi. Sasa imenifanya niungane na mwenzangu Mheshimiwa Olelekaita leo asubuhi akisema, kama mnaona kwamba hii Sekta ya Uvuvi ndiyo ina umuhimu mkubwa, basi ni bora Sekta ya Mifugo ipewe Wizara yake ijisimamie yenyewe ili tuweze kutafuta rasilimali za kuiendesha kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeangalia katika ilani ya CCM ya mwaka 2020 mpaka 2025 ambayo ndiyo iliyounda Serikali inayoongoza nchi hii wameshabainisha vipaumbele na kwa masikitiko makubwa sidhani kwa bilioni hizi bilioni 16 tunaweza tukafanikisha masuala ya ugani na utafiti masuala ya uzalishaji wa mifugo na kutafuta masoko ya maziwa na nyama biashara ya nyama biashara ya mifugo na mazao yake soko landani na la nje ukarabati wa miradi mbalimbali ya minada mambo ya kimkakati ya mpakani na mapitio ya ada na tozo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hata wizara yenyewe waliweka malengo ambayo sijui watayatekelezaje na bilioni 16 kwenye hii sekta ya mifugo maana ndio ninayoisemea. Walisema kwamba tutasimamia kuimarisha afya ya mifugo ambayo ni mambo ya chanjo madawa majosho walisema watasimamia mambo ya vyakula vya mifugo na maji na wakati wilaya kame ndizo zenye wafugaji wengi kuliko wote nchi hii unakuta hawana vyanzo vingine wanategemea mabwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Olelekaita yeye anahitaji mabwa 40 mimi nahitaji 27 wametengeneza moja tu na fedha sizioni hapa, lakini basi kwa masikitiko makubwa nipende tu kusema kwamba wizara imetuangusha katika kugawa hizi rasilimali na ninamuomba waziri atueleze ni utaratibu gani au ni kwa sababu gani ameamua kuwapatia uvuvu asilimia 75 ya fedha zote za maendeleo akawapatia wafugaji asilimia 15 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwa sababu ya uhaba wa muda nilimsikia Mheshimiwa Spika, asubuhi hii akiongea kwamba NARCO imeferi kweli imeferi, lakini mimi ninaomba tu nishauri Serikali sisi kama kamati niseme kwamba naunga mkono hoja ya kamati yangu yote na kazi tuliyoifanya. Tulishapendekeza kwamba ifanyiwe review kwa ajili ya kujua ilianzishwa kwa nini, kwani ni imeferi na kama malengo yako bado yanahitajika wakati huu miongozo na kanuni zilizoianzisha zipitiwe kabla ya kufikia hatua ya kusema tuifutilie mbali maana yake nadhani ndio shamba darasa la kuzalishia mbegu bora za kuendeleza wafugaji wa nchi kwa hiyo naomba wapewe nafasi ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la mwisho, napenda kuongelea huu mtafaruku ulioko wa migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na wakulima na watumiaji wengi, katika jimbo langu la Longido sisi hatukuwahi kuwa migogoro na wakulima kwa sababu sisi ni wafugaji kwa asilimia 95 na maeneo ya hifadhi lakini pia hatujawahi kuwa na migogoro na hifadhi. Isipokuwa katika kipindi hiki kililchopo kuna pendekezo nadhani liko mezani halijaingia katika Bunge hili lakini limeshapita kwenye Baraza la Mawaziri la kutaka kumegua eneo la Wilaya ya Longido kuwa pori la akiba na ile ni ardhi prime land ya wafugaji ndio inaenda kuchukuliwa kuwa pori la akiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati marais wote wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Joseph Magufuli na wa Awamu ya Sita mama yetu mpendwa Samia Suluhu Hassan wana tuahidi kwamba ardhi ya ufugaji inakwenda kuongezwa ifikie hekta milioni sita sasa inakuwaje leo kuna wizara inanyemelea tena nyanda zetu za malisho na kuzipunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Waziri wa Mifugo ebu angalia kutana na mwezako wa maliasili kwamba utaratibu huo wa kwenda kutwaa ardhi ya wafugaji ,ardhi ambayo imepimwa ni ya vijiji, na maeneo ambayo yametenga ili kuyafanya hifadhi iangaliwe upya kwa sababu inaenda kinyume na matarajio katika maeneo ya wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)