Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na namshukuru Mungu kwa mara ya kwanza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitumie nafasi ya pekee kwanza kuwashukuru wananchi wapiga kura wote walionipigia kura nyingi kule kwenye Jimbo la Buhigwe. Ninawashukuru sana na ninawaahidi sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi ya pekee kutoka kwenye moyo wangu wa shukrani kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliotoka humu wakaja kunipambania. Ushindi wangu nilioupata ni wa sisi sote, ni wa Chama Cha Mapinduzi. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru Chama changu Cha Mapinduzi, Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi iliyoniteua na hatimaye nikapeperusha bendera ya Chama Cha Mapinduzi na leo niko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, ninaomba sasa niende kwenye hoja mama. Kwenye wilaya yangu naenda kujikita kwenye suala la minada ya mifugo. Wizara ya Mifugo tunashukuru sana imetengeneza, imekarabati, imejenga mnada ambao unasimamiwa na wizara. Lakini huo mnada mpaka sasa hivi una zaidi ya miezi saba ulikwishakamilika, mkandarasi amekwishawaomba ili awakabidhi Wizara nao hawajafika. Ninaomba Wizara ije ifungue ili huo mnada ufanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wilaya ninayotoka iko mpakani, tunayo changamoto inayotokana na tozo ambalo inaonekana ni kubwa kwa wafanyabiashara wa mifugo. Ng’ombe mmoja anayesafirishwa nje na ni wafanyabiashara wadogo wadogo tu, tozo yake, ada yake ni 25,000. Hiyo imesababisha wafanyabiashara wa nchi jirani ambayo ni Burundi pale, hawaji kwenye minada yetu. Naomba Wizara ipunguze tozo hiyo ili waweze kuvuka na wanunue mifugo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mnada wa halmashauri ambao uko mbali kwenye Tarafa ya Myama. Kwenye Tarafa ya Manyovu tuna ng’ombe wengi sana. Mifugo hio wanaenda kiholela, wanatoroshwa, hatuna mnada. Ninaomba tufungue mnada mwingine wa Halmashauri katika Kata ya Kibande ambayo ni karibu kabisa na iko mpakani mwa Burundi, ili Warundi waweze kuvuka wenyewe na wakishavuka wanunue wale ng’ombe na biashara nyingine zitaamka pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi hapo hapo kwenye Idara ya Mifugo ninayo Tarafa ya Myama, ina kata saba. Kuna kata moja inaitwa Kata ya Kajana, ina mifugo wengi; hatuna josho. Naomba josho lijengwe pale. Nikirudi kwenye minada, tulikuwa na Afisa Minada mmoja lakini mpaka ninaposimama na kuzungumza hapa mbele ya Bunge lako Tukufu amekwishahamishiwa Pugu. Naomba mtuletee Afisa Minada ili aendeshe huo mnada ambao mmetujengea ulete tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea kuchangia hapo kwenye mifugo, tuna matatizo na tuna upungufu wa Maafisa Ugani. Hata wale waliopo hawana vitendea kazi. Tunaomba Wizara yako iwaone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara ya kwanza, naamini Wabunge wenzangu mtaendelea kunilea. Naunga mkono hoja. (Makofi)