Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, niko hapa mwisho kabisa. Naomba upaone kabisa, nimesimama. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kukushukuru sana kwa kupata hii nafasi na kwa kweli, wavuvi wana matumaini sana na wewe, hasa baada ya kuona jinsi ambavyo umeweka msisitizo katika Wizara ya Kilimo na leo kwenye Wizara hii ambazo ulisema kabisa zote ziangaliwe kiundani kwa sababu, zinawaajiri wananchi wengi sana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwapongeza Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu wake, lakini pia Makatibu Wakuu wote wa Mifugo na Uvuvi wanajitahidi kwa kadiri inavyowezekana pamoja na timu zao zote.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo niseme pia, nawashukuru sana Wizara hii kwa kusikiliza kilio cha wananchi wa Jimbo langu la Nyasa ambao sisi tunatumia takribani ukanda wa kilometa 150 za Ziwa Nyasa. Kwa muda mrefu zaidi ya miaka 20 tumekuwa tukilia, tunalalamika kwa ajili ya kutuzuwia kuvua samaki wanaoitwa vitui, samaki wadogo ambao hawakui, lakini mwaka jana mwezi wa nane tulipata hiyo ruhusa na wananchi sasa hivi wanafurahi na wanasomesha watoto wao. Kwa hiyo, nafurahi kwamba, wamekuwa wasikivu katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe kufanya tafiti kabla ya kutoa makatazo kwa sababu, watu wameteseka zaidi ya miaka 20 kwa sababu tu, kulikuwa hakuna taarifa za kutosha. Hata sasa hivi tulivyoruhusiwa hatujapata majibu kwamba, sasa yule kitui anakua au hakui? Kwa hiyo, tunaomba wakati mwingine tusiwe tunafanya makatazo kabla ya kuwa na taarifa za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kukuunga mkono na kuendelea kusisitiza juu ya umuhimu wa halmashauri ambazo zimeanza hivi karibuni na kipato chake ni cha chini, ziko pembezoni na kipato chake ni cha chini. Sawa na ile Wilaya yangu ya Nyasa, kuweza kuangalia upya namna ya kuziendesha halmashauri hizo. Kwa sababu, bila kufanya hivyo hizo halmashauri badala ya kuwa ni sehemu nzuri ya kuwahudumia wananchi inakuwa ni sehemu ya kuwa na kikwazo, kuwa na manyanyaso, kuwa na mateso kwa wananchi kwa sababu, ya kutafuta fedha za kujiendeshea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halmashauri nyingine zilizopata uwezo mkubwa kimsingi tumezijenga wote kwa sababu, inapotokea tunakubaliana kwamba, safari hii tutajenga barabara ya mahali fulani au tutajenga fly-over mahali fulani au tutajenga miundombinu mahali fulani, ina maana wengine wote tunasubiri ili kuwezesha hizo halmashauri zipate mapato na hatimaye tufaidike wote. Sasa zinapoenda tu kuhudumia hizo halmashauri zenyewe ambazo zimeshapata uwezo na wengine wakaachwa wanateseka si sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hayo? Katika uvuvi, Halmashauri kwa mfano ya Nyasa, inakusanya ada ya leseni 20,000/= eti ili uende ukaingie kuvua mle majini ulipe kwanza 20,000/= kwa maana hiyo, kila mvuvi anayeenda kuvua lazima afanye hivyo. Na vijana wetu wengine ambao wako kule na wengi ambao kwa kweli, hawajasoma sana kwa sababu, hata nikiuliza sasa hivi kwenye Wizara wavuvi wangapi wana cheti angalau cha uvuvi, sidhani kama nitapata jibu. Nikiuliza wavuvi wangapi wana degree hatutapata jibu kwa hiyo, ni wale tu ambao wamekuwa wajanja wa kuzaliwanao ndio wanaenda kuvua kule halafu unamwambia ili uingie majini leta kwanza 20,000/= wewe umemsaidia nini mpaka yeye kujua kwenda kuvua? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna tulichomsaidia, wanahangaika tu wenyewe na vimitumbwi hivyo. Na kimtumbwi hata kikawa kidogo kiasi gani nacho kinachajiwa (Charge) leseni ya 20,000/= wakati ni hatari huko anakoenda, anaenda tu ilimradi ameenda. Ndio maana nasema kwamba, hata suala la elimu kwa wavuvi ni muhimu sana, lakini huko hatujaenda.

Mheshimiwa Spika, unakuta kwamba, kimazoea karibu wataalam wengi tunaokuwa tunawaandaa, vyeo vyetu vingi, ni kwa ajili ya kwenda kufanya udhibiti sio wao wenyewe kwenda kufanya ile kazi ambayo inaendelea kama kazi ya uvuvi. Ndio maana mwanafunzi akimaliza anasema sasa kazi iko wapi? Kwa sababu umemfundisha kazi za kudhibiti hukumfundisha kazi za yeye kwenda kufanya shughuli ile kwa mfano ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hilo linaumiza sana na ndio maana hata mara ya mwisho niliulizia kuhusiana na engine za maboti, kwa nini watu wakopeshwe kwenye vikundi? Lazima walazimishwe kuwa kwenye vikundi? Kwa sababu, mtu akiwa peke yake anajisikia acha nifanye hii kazi kufa na kupona niweze kupata faida, lakini unamwambia kwamba, lazima uende kwenye kikundi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika tumeona hapa kwa upande wa kilimo, angalao tunasema kwamba, tani moja mtu apite bila kulipa ushuru, lakini mvuvi akishakuwa hapo na vidagaa vyake vichache, visamaki vichache, basi utakuta kila kona inamdai alipe, kila kona alipe. Huyo mvuvi lini atabadilika akawa ni mvuvi mwenye uwezo? Ndio maana mara nyingi katika maeneo ya fukwe wavuvi wengi bado ni masikini, hawajawa na kipato cha kutosha kwa sababu wanabanwa kiasi kwamba, hawawezeshwi vizuri, lakini nina imani kubwa sana na Wizara hii, nina imani kwa sababu, nyie ni wasikivu. Hata siku ile nimeuliza tu swali naona Naibu mara kwa mara unakuja tuna-share, tunashauriana, basi naamini kwamba, tutaweza kwenda vizuri kwa hiyo, niwaombe sana Wizara.

Mheshimiwa Spika, sitachangia katika mambo ambayo ambayo ni ya macro, macro level hayo ya kisera, sheria, nini, hayo nendeninayo ninyi. Wananchi wangu wamenituma nije nilalamikie hayo madogomadogo wanayoishinayo kila siku. Nachangia kwenye micro level ili ukitatua hilo tatizo lao dogo wao wanaendelea kuishi wakati mikakati mikubwa ya kitaifa inaendelea. Kwa hiyo, sitachangia kuhusu meli ya uvuvi kwa sababu meli ya uvuvi tutapata nne zitakuwa Bahari ya Hindi, hilo ni jambo jema sana kwa sababu, tumelalamika kwa muda mrefu kwa nini watu tunafikia mpaka tunakamata watu kutoka nje wanakuja kutuvulia kwenye maji yetu, lakini sisi wenyewe tunashindwa kuvua, hapo mmepiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hilo kwa sababu, najua kwamba, tukipata mapato hayo mapato tena yataondoka asilimia chache kwenda kusaidia kule kwa wavuvi wangu wa Wilaya ya Nyasa. Kwa hiyo, niwaombe sana tufanye hivyo, lakini na hizo ranch ambazo tumeambiwa hapa, ndugu zangu hata nilikuwa kule Rukwa, ranch ilikuwepo pale eneo la Namanyere, Nkasi, ng’ombe wachache tu na hata yule mwekezaji tuliyemuweka pale eneo la Sumbawanga mjini bado na yeye ng’ombe 150 kwenye eneo la zaidi ya hekta elfu kumi kwa hiyo, lazima tuangalie vizuri namna gani tunawekeza, namna gani tunasaidia kuona kwamba, yale tunayowekeza yanakuwa yenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni pamoja na kuwasaidia hao wananchi tunaosema kwamba, wao sasa sekta binafsi ndio iwe engine katika kuwezesha masuala ya kilimo, masuala ya mifugo, masuala ya uvuvi. Nimegundua kitu kimoja, private sector huwa sisi ni rahisi kumhamasisha aingie katika kutenda, katika kuwa kwenye mfumo tunaouhitaji, lakini akishaingia humo akapata kikwazo sisi Serikali, sisi watunga sera, sio rahisi sana kumsaidia, yaani tunataka aanze aingie likishampata huko atajijua mwenyewe na saa nyingine tunamlaumu kwa nini anafanya hivyo? Ameshindwa yule bwana.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu kuna mfano Hai. Hivi kile kiwanda cha pale Sumbawanga cha Mzee Mzindakaya kwa nini kimeshindwa kufanya kazi mpaka leo? Tatizo ni nini? Kama alichukua mkopo na mkopo ulikuwa ni wa Serikali kwa nini sisi Serikali tusichukulie ule mkopo ni sawa na asset yetu tuliyoiwekeza pale tukazungumza na mzee yule ili kukiona kile kiwanda kirudi katika hali yake ya uzalishaji?

Mheshimiwa Spika, kiwanda ni kizuri sana na yule mzee aliwekeza, mimi ninavyoamini aliwekeza kwa hamu kwamba, ngoja nikawekeze Sumbawanga angalao nako na sisi tuwe na kiwanda. Yaani alikuwa na ile kiu ya mafanikio, alikuwa na ile sifa kwamba, Sumbawanga kuwe na kiwanda. Matokeo yake wakati ule anawekeza barabara kutoka Sumbawanga mpaka Tunduma ilikuwa ni ya vumbi, mashimo matupu. Alikuwa anasafirisha hizo nyama mpaka Dar-es-Salaam, hakukuwa na Kiwanja cha Songwe kinachofanya kazi, kiwanda cha ndege.

Mheshimiwa Spika, matokeo yake magari yale na mkopo wake ameutumia wakati akiwa na mazingira magumu ya uwekezaji, ame-fail. Kwa nini sasa hatumnyanyui? Tunaona kwamba, kama lile ni suala la Mzindakaya na sio suala la nchi, hela aliyotumia ilikuwa ni zile ambazo zilikuwa zinasaidia wajasiriamali wadogo wavuke kwenda kwenda kwenye ujasiriamali wa kati. Kwa hiyo, nasema kwamba, pale tutakapomuona huyu private sector ni ndugu, huyu private sector anawekeza kwa manufaa ya nchi, anawekeza kama kichochezi cha uchumi wa nchi, hapo ndipo tutakapoenda vizuri, lakini tukimchukulia yeye ni mtu binafsi, amekwama kodi, huyu ana miaka mingapi sasa halipi, mwizi, matokeo yake inakuwa kwamba, wengi wanakimbia kwenda kwenye private sector.

Mheshimiwa Spika, sisi wenyewe sasa kama Serikali tunarudi, acha tuwekeze na sisi kuwekeza kwetu ni ngumu kwa sababu, kwanza ili tukubaliane kuwekeza au kufanya jambo fulani lazima tukae vikao. Na tukitoka kwenye vikao pengine iundwe kamati na kamati na yenyewe kutoa majibu saa nyingine inaogopa inasema nitaambiwa nimekula fedha. Matokeo yake yote tunatoa majibu ambayo yanakuwa yako kati kwa kati. Haya ikitoka hapo sasa fedha zinapatikana vipi, miaka mitatu hatujafanya. Niwaombe sana Ndugu zangu tuiunge mkono sekta binafsi ili tuweze kuendeleza eneo letu la mifugo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)