Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, naungana na waliotangulia kukushukuru sio tu kwa kunipa nafasi lakini kwa kuendesha Bunge lako vizuri kama walivyopongeza wengine katika siku hizi za karibuni tunajifunza kitu kipya kutoka kwa Ndugai tuliyemzoea, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi na wananchi wangu wa Kigoma Mjini unapozungumza habari ya uvuvi, unazungumza kiwanda kinachoajiri watu wengi na ambacho ni tegemezi kubwa la wananchi wa Kigoma Mjini. Hii inatokana na kwamba tunazo malighafi nyingi ambazo tungeweza tukaweka viwanda lakini kwa sababu hatujapata umeme wa grid ya Taifa bado malighafi hizo zinachukuliwa kwenda sehemu nyingine na nyingine hazijatumika kabisa na kwa maana hiyo uvuvi ndiyo eneo pekee ambalo tunalitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitamshukuru Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya uvuvi na Wizara yake kwa ujumla. Hivi karibuni mimi na yeye tulifanya ziara Kigoma, ilikuwa mwezi jana Aprili na tukaongea na wavuvi. Napenda kutumia nafasi ya Bunge hili kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Uvuvi, kwa namna ambavyo ametatua matatizo ya wavuvi baada ya kupata ukweli na hali halisi ya manyanyaso wanayoyapata ambayo yana maeneo mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ni eneo la Kanuni zilizotungwa zinazoongoza shughuli za uvuvi. Pili, ni utendaji wa ofisi yake kwa baadhi ya watu ambao wamekuwa hawana huruma kwa wavuvi. Siwezi kurudia mambo ambayo naona Mheshimiwa mwenzangu Aida ameyasema na wengine, lakini niseme, uzalishaji wa uvuvi uko chini karibu maeneo yote ya nchi yetu. Ukitafuta sababu kubwa ni mbili, sababu ya kwanza ni zana duni, lakini sababu ya pili, ni kanuni ambazo si rafiki kwa wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hili la Kanuni Waziri ametusaidia na namuomba aendelee kutusaidia. Kaja Kigoma pale katoa tamko la Serikali la kutaka wavuvi wa samaki wa migebuka watumie wavu wa inchi mbili, ply mbili badala ya maelekezo yaliyokuwa kwenye Kanuni ya wavu wa inchi tatu ply nne mpaka sita, ambao kwa kweli muda mrefu umewasumbua wavuvi kutokuvua. Kwa hiyo, nashukuru sana hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nimwombe Mheshimiwa Waziri asiishie hapo, kuna jambo pale tulisahau kuliweka sawa la tundu au macho ya wavu. Kanuni ya zamani ilikuwa inasema macho 144 kwa sababu wavu ulikuwa wa inchi tatu ulikuwa upana wa wavu sasa unakuwa mita 12.5. Sasa ukishapunguza upana wa macho yale kuwa ni ya inchi mbili ukiacha macho 144 ina maana kwamba wavu ule unakuwa sasa kina chake kwenda chini ni mita saba tu hauwezi kuvua. Kwa hiyo, wavuvi wanasema wanataka waende kwenye ile ile mita 12 kwa hiyo, lazima uongeze macho kwa sababu umepunguza ukubwa. Hili tulikwishalizungumza na Waziri akalielewa vizuri kwa hiyo, wameomba macho angalau
yafike 300 yawawezeshe kuvua vizuri na hasa katika ziwa hili lenye kina kirefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la zana duni za uvuvi, mimi nashangaa sana kwenye nchi yetu, tunapiga kelele ya mambo mengi lakini tunajizuia sisi wenyewe, tunasukuma gari halafu tunaweka gingi sasa itakwendaje? Ipo kampuni ya uvuvi ya wazawa wa Kigoma tangu mwaka 2015 maombi yao yako Wizarani, wametimiza vigezo vyote hamuwaruhusu kuingiza boti za kisasa za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, baba yangu alikuwa mvuvi, kulikuwa na vyombo pale vya Wagiriki vinaitwa Angella wengine Yorobwe na kulikuwa hata na chombo cha Kibwedeko. Tulikuwa tunavua samaki mmoja wa nonzi na sangara anabebwa na watu nane leo hii hatuvui kwa sababu ya zana duni za uvuvi. Hata hivyo, urasimu uliopo wa kupata vibali vya zana za uvuvi, bora uombe kibali cha kwenda peponi utaingia haraka kuliko kupata zana za uvuvi. Haiwezekani lazima tubadilike Mheshimiwa Waziri tutoe hapo, hatuwezi kupata tija kwa zile zana zilizopo sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni ushuru katika mazao ya uvuvi. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri umelizungumza kidogo. Ushuru huu umekuwa tofauti sana katika mazao ya uvuvi ya Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika. Kwa mfano, kilo moja ya dagaa inayotaka kusafirishwa kwenda nje inadaiwa Dola 0.5 ambapo ikifika mahali unasafirisha kilo 100 ni zaidi ya Dola
50. Sasa hii kwa kweli unafika mahali unawakatisha tamaa hao wanaotaka kufanya biashara hii. Lazima tuangalie, ushuru uwe kidogo unaovutia biashara kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda mfupi hapa ulipokuwa unatambulisha wageni, umetambulisha wageni wangu na wako mpaka sasa kwenye gallery pale. Hawa walikuwa wananisubiri, tunakwenda nao Kigoma, wamewekeza kwenye kuchakata samaki Mwanza na tunataka kwenda nao Kigoma. Ila katika mazingira haya ya urasimu wa miaka mitano watu hawajapata vibali, haitawezekana.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kitu kimoja, uwekezaji huu lazima tuujue uko wa aina mbili. Wapo wawekezaji ambao wanakuja kuwekeza katika nchi yetu, lakini soko lao wanategemea ndani ya nchi yetu. Wapo wawekezaji wanakuja kuwekeza katika nchi yetu, soko lao wanategemea nje. Hawa ndiyo wawekezaji bora zaidi. Kwa mfano, hawa nilionao mimi, Wachina wamefika mahali wamewekeza kule Mwanza. Wenyewe wanachukua yale matumbo ya samaki ambayo zamani yalikuwa yanatupwa. Wanachukua minofu, mapanki wanachukua Waswahili wenzetu wanakula, matumbo yalikuwa yanatupwa. Wenyewe wamechukua yale matumbo (fishmonger), wanafika mahali wanasafirisha huko nje na tunapata pesa nyingi. Huu ndiyo uwekezaji mzuri zaidi maana wanatoa hela nje kuingiza ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikoni mtu ambaye ameleta material zake hapa anafika mahali anawekeza marumaru ambazo zinanunuliwa na Watanzania wenyewe humu humu wanachukua hela zetu. Kwa hiyo, nataka nisisitize lazima tutengeneze mazingira mazuri. Leo hao wawekezaji wa Mwanza…

SPIKA: Mheshimiwa Kilumbe, kumbe matumbo ya samaki nayo ni chakula!

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Ohooo! Tena kina soko kubwa kuliko hata minofu ya samaki. Wapo hapa (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kushangaza hao hao wawekezaji ambao wapo hapa, wameomba vibali vya wafanyakazi wao wawili, leo miezi sita hawajapata na wameshalipa. Kila mmoja wamemlipia kama Dola 1,000 na risiti wamenipa wanazo hapa, lakini mpaka leo vibali vya wafanyakazi hao ambao wanakuja kuwekeza kwa ajili ya kuchukua matumbo ya samaki ambayo sisi hatuyatumii, wanayapeleka nje, sisi tunapata fedha. Mambo ya ajabu kabisa! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niseme kwenye Sekta hii ya Uvuvi sisi tunategemea Mheshimiwa Waziri na ndugu yetu Mheshimiwa Ulega, Naibu Waziri, mlete mapinduzi makubwa yaongeze pato la Taifa. Katika mapinduzi haya makubwa tunayotaka myatazame, kwanza ni hizi kanuni ambazo namshukuru Mheshimiwa Waziri ameanza kushughulika nazo. Pili, ni kuruhusu uwekezaji mkubwa kwa sababu mnaona leo tunalaumu hapa NARCO.

Mheshimiwa Spika, nami naungana nawe, jamani mwelekeo wa Sera za CCM katika miaka ya 1990 ni kutuondoa katika Sekta ya Umma kutupeleka kwenye Sekta Binafsi. Sekta Binafsi iweze kuchangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa. Sijui kwa nini hatuelewi hili? Kwa hiyo, leo Sekta Binafsi, tuisukume, tuitengenezee mazingira, sisi tukusanye kodi ili kodi zile zisaidie wananchi wetu. Mnakazana na Sekta ya Umma ambayo inafika mahali kila wakati inawekewa ruzuku na ruzuku zile zinayeyuka, kinachoendelea hakuna, mapori yamekaa. Hatuwezi kuendelea hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunataka kwenye uvuvi Sekta Binafsi imeonesha, hivyo viwanda vyote unasikia viko Mwanza, ingawa Mwanza kuna viwanda leo vya minofu mpaka hivi vya matumbo ya samaki, viko kama vinane tu, lakini nenda Uganda, viko 30 kwa sababu, Uganda wametengeneza mazuri ya uwekezaji.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kilumbe, subiri. Mheshimiwa Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nimpe taarifa mchangiaji. Siyo matumbo ya samaki. Yanaitwa mabondo kwa lugha nzuri.

SPIKA: Mheshimiwa Ng’enda unapokea Kiswahili hicho?

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, yaani hiyo taarifa ni sahihi na kama unavyojua Kiswahili kimepanuka sana katika hivi vitu vya kisasa, maana hicho nilichotumia mimi ni cha Kigoma zaidi. Lugha sahihi ni mabondo na kwa kizungu wanaita fish maws. Kwa hiyo, nakubali taarifa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie suala zima la ushuru, kutazama ushuru. Nimeshalizungumza na ushuru usiwe na tofauti kubwa. Leo Ziwa Victoria, dagaa wa kilo
100 ushuru wake ni shilingi 38,000/=, lakini Ziwa Tanganyika 116,000/= kwa kilo 100. Tusiweke hii tofauti kubwa kiasi hicho.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo limelalamikiwa na wavuvi na wafanyabiashara wa mazao ya uvuvi, Mheshimiwa Waziri tukiwa pale Kigoma unakumbuka, dagaa zina grade kama ilivyo tumbaku. Sasa sijui hakuna classifiers wa ku-classify hii ni class gani na hii ni class gani? Haiwezekani classes zote ziwe bei moja tu ya ushuru. Kuna dagaa wanaitwa nyamnunga, walipigwa na mvua, hao ni kwa ajili ya chakula cha kuku…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.