Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba hii ya Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, lakini Mheshimiwa Spika nakubaliana na wewe kwamba NARCO imeshindwa moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeambiwa hapa na Mheshimiwa Mwijage kwamba Uganda maziwa peke yake yanachangia shilingi dola milioni mia moja, mapato ya mauzo ya maziwa nje ya nchi, sisi Tanzania maziwa kwanza hatuuzi, lakini Wanyama wote livestock nzima siyo maziwa item moja inazalisha mapato ya ndani asilimia kumi, siyo ile national product, gross GBP mapato ya ndani asilimia kumi peke yake, ng’ombe ambao ni maziwa ndani yake, nyama, ngozi, mbuzi, kondoo, nguruwe, kuku yaani kwa ujumla wote, livestock yote, asilimia kumi kwenye mapato ya ndani gross domestic product. Kwa hiyo kwa kweli hii ni kielelezo kwamba NARCO imeshindwa kabisa kazi, imekuwepo muda mrefu inafanya kazi ya kuendeleza mifugo ambayo haiiendelezi, nimesema, wabunge wamesema na wewe umesema ranch zote zimekuwa machaka, mapori imejaa miti hakuna Wanyama. Tunapoomba sisi kupewa hizo block tuanze kufuga hatupewi ili tuziendeleze ndiyo ile private sector kuingia kule kwenye ile sector wanabaki wana mapori ambayo hawayatumii.

Mheshimiwa Spika, hicho ni kielelezo kimoja cha kwamba wameshindwa, kingine kipo jimboni kwangu Bukoba nina kata mbili ambazo nashindwa kuelewa kwa nini NARCO inashindwa kuweka mipaka kati ya wananchi na hizo ranch au block hizo, wananchi wanapata shida kubwa sana. Kuna Kata ya Luhunga na Kata ya Kibirizi yaani watu wanaishi kwenye ranch humo, wanavurugana, juzi, juzi hapa katika Kata ya Luhunga NARCO ilitenga kipande hivi block hivi ikampa mtu mmoja, mfanyabiashara mmoja tena kiongozi mkubwa, akawaambia hiyo ni block yako, hiyo sehemu inawatu ndani yake, ina makazi ya watu, ina shule, ina makanisa, ina misikiti, ina maeneo wanaishi humo ndani, wakampa mtu aweke pale ng’ombe wake, akaweka ng’ombe wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi kwa hasira wakawaua hawa ng’ombe wote wale wakawaua zaidi ya mia, kwasababu wameingia kwenye makazi yao, wamekula mazao yao, mihogo, ndizi n.k. Sasa unashindwa kufahamu NARCO inafanya kazi gani inayofanya hii. Hii inaitwa ranch ya Mabale ipo pale karibu na Kata ya Luhunga vitongoji na vijiji vya Kayojwe, Tainoni, Kabanga, Milembe vipo mle ndani kwenye ranch, NARCO haiwezi kuweka mipaka ya wazi kwamba hili ni eneo la watu, hili ni eneo la mifugo hiyo ya ranch ambayo wameitenganisha. Hakuna mipaka inayoonekana wazi kwamba hapa ni watu hapa ni mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Kata ya Kibirizi mwaka jana Disemba, mwezi wa kumi na mbili akaenda Meneja wa ranch pale, ranch ya Kagoma akaweka mpaka mpya kwenye maeneo ya watu, akateka kaya 170 ndani ya ranch, akaingiza kwenye ranch, akaziingiza, ambazo zilikuwa nje ya ranch akaziingiza katika mpaka mpya kwa kufanya hivyo akawa amechukua maeneo ya wakazi 1,138 hawana pakukaa, wamekumbwa na ranch ambayo haikuwepo leo wanasemekana kwamba wapo ndani ya ranch.

Mheshimiwa Spika, uamuzi ambao ameuchukua mwenyewe hakushirikisha viongozi, hakuhusisha wananchi amekwenda kuweka mipaka mipya na akachukua maeneo ya wakazi ambayo yalikuwa tayari yana makazi ya watu. Sasa hiyo ni matatizo ambayo yanaonyesha kwamba NARCO kwa kweli kazi haiiwezi imekuwa ngumu kwao tuangalie njia nyingine ya kufanya NARCO waachie hii kazi kama inawashinda. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa, niko hapa Sanga.

SPIKA: Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa pia mzungumzaji kwamba NARCO kwamba imeshindwa kuna mambo mawili ambayo pia yamejitokeza, kwenye hotuba ya Waziri ya mwaka 2016 na hata zilizofuata wanakiri wazi kwamba Serikali imeshindwa kuzalisha Mitamba kwa maana kwa mwaka 2015/2016 ilizalisha Mitamba 634, lakini Private Sector ilizalisha Mitamba 10,820 na kusambaza kwa wananchi kwa hiyo hicho ni kigezo mojawapo cha kwamba NARCO imeshindwa.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine cha pili Ranch ya Ruvu ambayo inasimamiwa na NARCO kuna mradi wa 5.7 billion ambayo hadi sasa umekwama, lakini mashine zimenunuliwa zipo pale zinaoza kwenye makontena kwa hiyo ni kweli NARCO imeshindwa.

SPIKA: Nakuunga mkono katika taarifa hiyo, wakati Olelekaita anasema katika Wilaya ya Kiteto wana ng’ombe laki kadhaa, umesema laki ngapi, laki tano, NARCO nchi nzima ina ng’ombe haizidi 16,000 can you compare the two, ni wastage, yaani NARCO mmeshindwa endelea. (Makofi)

Mheshimiwa Rweikiza.

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo naikubali na naiunga mkono ni taarifa nzuri.

Mheshimiwa Spika, nashindwa kufahamu kwa nini Wizara inavumilia uozo huu wa NARCO kushindwa hasa kuchukua maeneo ya watu na kuwahamisha isivyo halali, watu wanauliwa, wanaua wanyama hawa, wanyama hawana hatia, hatia ni ya NARCO. Kwa nini Wizara inanyamaza na inafumbia macho jambo hili? Hatuwezi kuthamini wanyama kuliko watu, haiwezekani. Hili ni kosa kubwa linafanyika ni lazima litafutiwe ufumbuzi na tuweze kupata maelezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo navyozungumza hapa, hawa NARCO wako Karagwe katika Jimbo la Mheshimiwa Bashungwa wanapima kule, wanachukua maeneo ya watu wanawaingiza kwenye ranchi. Wako kwenye Kata inaitwa Lugela, wamechukua maeneo ya watu wameingiza kwenye ranchi, watu wako kule ndani, kuna shule na kadhalika. Sasa hawa watu wana nia gani? Wanaingiza watu kwenye ranchi maeneo ambayo hayakuwa ranchi hapo awali.

Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba miaka miwili iliyopita au mitatu Mheshimiwa Rais aliunda Tume au Kamati ya Mawaziri nane kwenda ku-monitor jambo hili nchi nzima. Wakazunguka maeneo ya ranchi na maeneo ya watu, wakaainisha kwamba watu wabaki huku na ranchi zibaki huku na nafikiri walitoa taarifa yao nzuri lakini NARCO au tuseme Wizara haitekelezi jambo hili ili shida hii iishe. Kwa hiyo, kwa kweli hili ni jambo kubwa linaathiri sana watu.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana kwenye kampeni pale kwangu ilikuwa patashika, wananchi wanasema hatukupi kura kwa sababu tunatishiwa na ranchi hizi, tutakupaje kura wewe na CCM kama hamuwezi kumaliza jambo hili? Kwa hiyo, jambo hili ni kubwa sana na ni la kisiasa, kisera, kiuchumi ni vizuri wananchi wakapata mipaka yao inayoeleweka. Kwa hiyo, niombe Wizara inapokuja kumalizia jambo hili itupe maelezo wanafikiria nini kulimaliza.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, wamesema Waheshimiwa Wabunge hapa ni la uvuvi, hata mimi linanihusu nina maeneo mengi ya uvuvi. Watu wanavua samaki wa ukubwa mbalimbali na wanatumia nyavu ambazo wanazinunua kihalali madukani. Nyavu zinalipiwa kodi na zinauzwa kihalalali, lakini wanakwenda kuchoma nyavu hizi kwenye mitumbwi kule ziwani, wanazikamata na kuzichoma moto. Samaki wanakamatwa, akina mama na wavuvi wengine wananyang’anywa, wamenunua kwa wavuvi ambao wamenunua nyavu zile kihalali.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa nini mnaruhusu nyavu hizi zitoke madukani au viwandani, watu wauziwe, halafu unasema hii sio halali. Mnakuwa wapi zinapotengenezwa, zinapoagizwa, zinapouzwa, usubiri mpaka zifike ziwani ndio uwazuie watu kutumia. Huu ni uonevu mkubwa ambao hauwezi kuvumiliwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naunga mkono hoja lakini nataka majibu, ahsante sana. (Makofi)