Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sikupata nafasi ya kuchangia hoja hii ndani ya Bunge naomba niwasilishe mchango wangu kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitangulie kwanza kumpongeza Waziri Mheshimiwa Lukuvi, Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Angelina Mabula, Katibu Mkuu na watendaji wote Wizarani pamoja na taasisi zilizoko chini Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya. Nadiriki kusema bila kumumunya maneno kwamba Waziri Lukuvi ni mmoja wa Mawaziri wenye uwezo mkubwa ndani ya Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze Waziri kwa kufuta hati ya shamba la Valeska kule Arumeru Mashariki na kwamba sasa yuko tayari kwenda Meru na kukabidhi shamba hilo Halmashauri na wananchi wa Meru.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo sasa nachangia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, upimaji na umilikishaji na kupanga matumizi bora ya ardhi; nilipokuwa nahudumu kwenye Kamati ya Ardhi Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Waziri aliwahi kutuahidi kwamba kila inchi ya nchi yetu itapimwa na kuwekewa mpango bora wa matumizi. Mpaka sasa zoezi la upimaji wa ardhi linafanyika kwa kususua sana. Nashauri Wizara ije na mpango kabambe wa kuharakisha upimaji na umilikishaji wa ardhi nchini kote ili tuondokane na janga la ujenzi holela ambao unapelekea miji yetu kuwa squatters. Lakini si hivyo, ardhi iliyopimwa na kumilikishwa ni chanzo cha kuaminika cha mapato. Serikali iangalie eneo hili kwa jicho tofauti na kulifanyia kazi kwani zoezi hili linaweza kuwa mwarobaini wa tatizo sugu la ufinyu wa bajeti ya ujenzi wa barabara na sekta zingine ambazo ni muhimu na zinahitaji fedha nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro ya ardhi; Serikali ibadilike sasa na kuacha kunyang’anya wananchi ardhi bila ustaarabu kwa kisingizio cha kupisha miradi ya kitaifa/ uwekezaji. Nikisema hivyo siyo kwamba napingana na Serkali katika utekelezaji wa miradi muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Tatizo liko kwenye namna ya utekelezaji wa zoezi zima la kuwaondoa wananchi kwenye mashamba ambayo yamekuwa earmarked kubadilisha matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba wananchi washirikishwe kikamilifu kabla ya kuwaondoa kwenye mashamba husika. Mfano mzuri ni mashamba ya Malula upande wa Meru na Hai jirani na KIA. Wananchi walioko kwenye mashamba hayo waliambiwa siku nyingi wangeondolewa na kulipwa fidia kwa lengo la kuwawezesha wakapate mashamba sehemu nyingine ukizingatia kwamba wamekua pale kihalaii kwa miaka zaidi ya 40. Baada ya miaka takribani kumi tangu watangaziwe kwa mara ya kwanza kwamba wangeondolewa kupisha mradi wa industrial park na bandari kavu hivi karibuni Serikali ilikuja kwa ukali kwamba ardhi hiyo ni mali ya Serikali. Matisho hayo si sawa kwa sababu ardhi yote nchini ni mali ya Serikali na hata pale penye nyumba yangu ya kuishi ni mali ya Serikali, lakini ninaamini Serikali ikipahitaji itaniondoa kwa utaratibu fulani. Iko mifano mingi nchi nzima lakini itoshe kusema kwamba tuondokane na migogoro ya ardhi kwa kuwatendea wananchi haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu migogoro ya mipaka; nashauri Wizara ije na mkakati wa kumaliza migogoro yote ya mipaka kati ya wananchi na hifadhi ikiwa ni pamoja na mpaka wa kitongoji cha Momella na ANAPA (Hifadhi ya Arusha). Pia kuna migogoro kila leo kwenye mpaka wa Arumeru na Hai na Siha. Naomba Waziri atenge muda kidogo aje Arumeru na Siha aone ni jinsi gani matatizo yaliyoko kule yataondolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya haya machache, nakushuru na naunga mkono hoja.