Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Waziri Mheshimiwa Lukuvi kwa kazi kubwa anayoifanya pamoja na timu yake kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze kwa hotuba yake iliyojaa matumaini makubwa ya kupelekea kwenda kumaliza upimaji pamoja na kupunguza kama sio kumaliza kabisa migogoro hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto imekuwa ni Wilaya ambayo ipo chini sana hasa katika suala la upimaji ardhi na sijajua hili suala la kutopima ardhi Lushoto inasababishwa na Maafsa Ardhi ambao sio waaminifu, kazi yao maafisa hawa ni kula pesa za wananchi na kuwadanganya kuwa mtapata hati. Mpaka sasa hivi ninavyoandika ujumbe huu kuna wananchi ambao wameshalipia gharama zote za kupimia viwanja vyao, lakini mpaka sasa ni miaka saba sasa hawajapata hati zao wala kupimiwa viwanja vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya Ardhi iende Lushoto kwenda kuwanasua wananchi wale waliodhulumiwa na Maafsa Ardhi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na migogoro ya ardhi kwa wananchi na Serikali pamoja na mipaka ya vijiji na vijiji, kata kwa kata na hata wilaya kwa wilaya. Hivyo basi ili migogoro hii imalizike Wizara iendelee kukopesha Halmashauri ili ziweze kupima maeneo haya hasa ya wakulima na wafugaji. Jambo hili linachelewesha sana maendeleo kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali ianzishe sera ya nyumba kwani sera hii itakapoanzishwa itakuwa ni sheria yenye manufaa hasa katika ukusanyaji wa kodi za nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo niendelee kuishauri Serikali yangu tukufu hasa Wizara ya Ardhi itenge bajeti kubwa zaidi ili imalize kupima ardhi yote hapa nchini, kwani ardhi itakapopimwa kwanza kabisa migogoro ya ardhi itaisha, pili, Serikali itapata pesa za kutosha ambazo pesa hizo hazipatikani kwa kutokupimwa kwa viwanja vingi hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa asilimia mia kwa mia.