Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwanza kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa uchapakazi wake katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu unajikita mwanzo kwa Kitengo cha Upimaji wa Ardhi, naomba kuishauri Serikali kuongeza kasi ya upimaji wa ardhi kwenye Halmashauri zetu. Kitendo cha kuiachia Halmashauri jukumu la kupima ardhi bila msaada wa Serikali Kuu kutaacha Halmashauri nyingi kuwa na makazi holela kwenye Halmashauri zetu nchini, hasa zile Halmashauri zenye mapato kidogo. Hivyo basi niishauri Serikali kuongeza fedha za upimaji wa ardhi ili kupunguza utaratibu wa urasmishaji wa aridhi ambao hauna tofauti sana na makazi holela.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya yangu ya Liwale yuko Afisa Ardhi ambaye ameleta huu utaratibu wa urasmishaji ambao kwa mazingira ya Wilaya yetu haina uhaba wa ardhi, hivyo nikuombe Mheshimiwa Waziri kumsimamisha mara moja mpimaji huyu ambaye anakwenda kuharibu makazi ya mji wetu wa Liwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye Halmashauri yetu inakabiliwa na uhaba mkubwa watumishi wa ardhi kiasi cha kulazimika kuazima wapima toka Wilaya jirani ya Nachingwea ambapo Halmashauri huingia gharama za ziada ya upimaji kwa kuwa mpima toka jirani hulipwa malipo ya ziada nje ya bejeti. Jambo hili huongeza bei za viwanja na kuwafanya wananchi wa kawaida kushindwa kumudu viwanja hivyo na hivyo kuwafanya wandelee kukaa kwenye makazi holela.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Lindi, Liwale ndio Wilaya pekee iliyokubali kupokea wafugaji katika Vijiji vya Kimambi, Ndapata na Lilombe. Lakini hadi leo vijiji hivyo havijafanyiwa matumizi bora ya ardhi, jambo linalosababisha migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo niiombe Serikali kuja kuisaidia Halmashauri kufanya matumizi bora ya ardhi katika vijiji hivi.