Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri na Naibu Waziri pamoja na wataalamu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi ni hitaji muhimu la binadamu wote. Kumnyima binadamu haki ya kumiliki, kutunza na kutumia ardhi ni kuvunja haki za binaadamu. Katika jimbo langu la Moshi Vijijini, kuna migogoro mikubwa baina ya wakulima na wafugaji katika Kata za Mabogini (Kijiji cha Mserekie) na Arusha Chini (Mikocheni na Chemchem) zilizoko maeneo ya tambarare. Migogoro hii inahusiana na matumizi ya ardhi. Migogoro hii imeshasababisha madhara makubwa ikiwemo vifo na uharibifu mkubwa wa mali. Mpaka sasa Serikali ya Wilaya na Mkoa haijaweza kupambana na changamoto hii, kwani tatizo hili linajirudia mara kwa mara. Kwa mfano, katika Kata ya Arusha Chini, Kijiji cha Mikocheni migogoro hii imesababisha shule ya sekondari isijengwe, kwani mmiliki halali wa haya maeneo hajaainishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro ya wakulima na wafugaji jimboni kwangu inasababishwa na uhaba unaoendelea kukua wa rasilimali ardhi. Vilevile, migogoro hii inakuwa kwa sababu pande hizi mbili zina maadili ya kimila yanayotofautiana sana yanayohusisha makabila ya Wamasai (wafugaji) na Wachaga na Wapare (wakulima).

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro hii kwa kiasi kikubwa inasababishwa na haya yafuatayo; kupanuka kwa shughuli za kilimo na makazi ya watu; kubadilika kwa tabia nchi kunakopelekea malisho kukauka na kusababisha uhaba wa chakula cha mifugo na pia Serikali haijayapima haya maeneo na kuyamilikisha kwa wahusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali; kwanza kutokana na migogoro inayoendelea, kuna umuhimu wa Serikali kuingilia jambo hili na kuhakikisha kuwa maeneo husika yamepimwa na kumilikishwa rasmi kwa wahusika, ili utatuzi wa migogoro hii kupitia mifumo ya kimila na ile ya kitaifa iweze kutumika kwa usahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kutokana na mazingira ya Kitanzania, ninaishauri Serikali ipitie sera za umiliki wa ardhi zenye utata zinazoweza kuchochea migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji. Sera nzuri na rafiki itasaidia kutoa haki bila malalamiko.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.