Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara nyeti ambayo inawagusa wananchi moja kwa moja. Nianze kwa kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa William Lukuvi, kimsingi huyu ni mlezi wangu, kwa sababu miaka 10 ambayo nimefanya kazi kwenye sekta hii, amenitumia vizuri sana na nimejifunza mambo mengi sana. Kwa hiyo, namshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile namshukuru Mheshimiwa Angeline Mabula, naye amekuwa kama mzazi na mlezi wa karibu, kwa kweli niwapongeze, mnafanya kazi nzuri sana. Nampongeza Katibu Mkuu, Mary Gasper Makondo, bosi wangu wa zamani, naye anafanya kazi nzuri sana. Naweza kusema ni Katibu Mkuu wa kwanza ambaye ame-practice kwenye sekta hii kwa muda mrefu. Kwa hiyo, anaisimamia vizuri na anaifahamu sana. Kamishna Mathew na Makamishna wenzangu wote, maana mimi niliachia hicho cheo cha Ukamishna Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo, nawashukuru sana, tupo pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi, naomba Serikali iangalie Wizara hii kwa jicho la karibu sana, kwa sababu ardhi ni rasilimali namba moja. Mheshimiwa Waziri wa Fedha anajua, ni mchumi mzuri kwamba number one resource ni ardhi. Migogoro mingi siyo wakati wote inatokana labda na matatizo yaliyomo kwa wataalam, wakati mwingine ni kutokana na ardhi yenyewe kuwa ni kitu cha thamani. Kitu cha thamani lazima kigombaniwe. Changamoto za wataalam zipo, lakini na ardhi yenyewe nayo ni tatizo kwa sababu ni kitu cha thamani, kwa hiyo, inahitaji umakini zaidi na bajeti ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukiangalia wakati huu; nampongeza Mheshimiwa Waziri na Serikali wameanzisha Ofisi za Mikoa, maana yake huduma zimesogea jirani na wananchi. Kwa hiyo, wananchi wanapata hati kwa gharama nafuu zaidi na gharama ya muda, gharama ya fedha tumeweza kumwondolea mwananchi wa hali ya chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali, lakini niombe sasa Serikali iweze kuongeza fedha kwenye hii Wizara kwasababu nayo itakuwa na fursa yakukusanya zaidi iwapo itapewa vitendea kazi. Nitatoa mfano mmoja, pale Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa, nina maana ya Ofisi ya Ardhi Mkoa, ina vitengo vinne ambavyo vinafanya kazi tofauti kabisa. Kuna watu wa Mipango Miji, kuna Kamishna wa Ardhi, kuna Wathamini na kuna wale Wapima. Sasa kila mmoja unakuta anahitaji aweze kusafiri kwenda kusimamia kazi, kuna miji mipya huko inakua, inatakiwa itangazwe kwenye magazeti ya Serikali ili ipangwe, lakini wanashindwa kutokana na vitendea kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Wizara hii iweze kuongezewa fedha ili ofisi zile za mikoa ziweze kuboreshwa na kuwa na vitendea kazi vya kutosha; kama vyombo vya usafiri na vifaa vya kupimia ardhi, maana sasa hivi teknolojia imekuwa kubwa. Vile vile wakiongezewa fedha za kutosha wataweza kuboresha hii mifumo ya ardhi; Kuna mfumo unaitwa ILMIS, kuna mfumo unaitwa Land Rent Management System na mifumo mingine ambayo inahitaji uwekezaji mkubwa wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo hii itawezesha Wizara kupunguza muda ambao mwananchi anapata huduma, kwa sababu kila kitu kikiwa kwenye computer ni mouse click mwananchi anahudumiwa. Kwa sababu kitu ambacho kinawakwaza sana wananchi kwenye hii sekta ni upotevu wa muda, kwa sababu sekta hii ina mambo mengi. Kuna mtu anaandaa michoro ya mipangomiji, kuna mtu mwingine anaenda kupima na kuweka beacon, kuna mtu anafanya uthamini kwa ajili ya fidia na mtu mwingine anamilikisha. Kwa hiyo, kuna milolongo mingi ambapo hakuna mlolongo ambao unaweza ukauacha kisheria na kila kitu kipo kwa nia njema. Kwa hiyo, wakiongezewa fedha, waweze kuboresha mifumo hii ya umilikishaji ardhi na utunzaji wa kumbukumbu tutaongeza sana tija kwenye sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Wizara hii ina upungufu sana wa watumishi, kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuangalia namna ya kutoa kibali ili watumishi waweze kuajiriwa. Kwa mfano, mahitaji ya watumishi kwenye sekta hii; nilikuwa nasoma hotuba ya bajeti, inaonekana ni 4,847 lakini watumishi waliopo ni 2,378. Upufungu ni watumishi 3,114, lakini wenzetu wa Utumishi wa Umma wametoa kibali cha kuajiri watumishi 36 tu. Kwa kweli hapa tutaendelea kulaumu Wizara hii kwa sababu hatuwawezeshi kuajiri watumishi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri tuna vyuo vikuu; tuna chuo kinafundisha pale Morogoro, ni chuo kizuri, kinatoa wataalam wa ngazi ya Cheti na Diploma ya Upimaji, kuna chuo Tabora nacho kinatoa mpaka ngazi ya Diploma, kuna Chuo Kikuu cha Ardhi, kuna Chuo Kikuu cha Dodoma, kuna Chuo cha Mipango na vyuo vingine, vinatoa wahitimu hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakumbuka pale Jiji la Dodoma tulikuwa na watoto wanakuja ku-volunteer wakati mwingine wanafika mpaka 50, 60 na wengine tumewafundisha kazi, ni wazuri. Kwa hiyo, kuendelea kuwatumia wakiwa wanajitolea ni risk sana kwa Serikali. Kwa hiyo, napenda kutoa ushauri kwa Serikali, iweze kuwaajiri hawa na wengine ambao wapo mtaani ili waweze kusaidia kuongeza kasi ya upangaji ardhi, upimaji na utoaji hati za umiliki wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda kuzungumzia kipengele cha upimaji, upimaji shirikishi na urasimishaji. Wabunge wengi wameonekana hawajaridhika sana na kipengele cha urasimishaji. Hii kurasimisha maana yake ni kufanya makazi ambayo hayakuwa rasmi yawe rasmi. Sasa mazoezi haya huwa yanakuwa na migogoro na malalamiko mengi sana kwa sababu wananchi tayari wameshaendeleza maeneo yao, namna ya kuwapanga kwa kweli ni lazima itokee migogoro mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ile ya upimaji shirikishi ni njia ambayo inasaidia sana kuepusha matatizo ambayo yanatokana na uhitaji mkubwa wa fedha kwa ajili ya fidia. Kwa hiyo, kama fedha hamna, maana yake wataalam watakubaliana na wananchi, wanawapimia viwanja, halafu wanagawana viwanja. Viwanja vingine vinakuwa vya wenye ardhi na vingine vinakuwa vya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kinachotakiwa tu, wale wananchi kwa sababu tunawapa viwanja vingi, tuweke tu utaratibu wa kuwasaidia kuuza ili wapate kipato ambacho kinaendana na bei ya soko. Vinginevyo wananchi hawa watakuwa na viwanja vingi na hawana cha kufanyia. Kwa hiyo, tungeweka utaratibu mzuri wa kuwasaidia kuuza ili wapate fedha halali ya haki ambayo inaendana na bei ya soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naipongeza Wizara kwa kuanzisha huu mfuko wa kukopesha fedha kwenye Halmashauri. Sasa Wizara iende mbali zaidi, iangalie pia na haya makampuni binafsi ambayo yanatambulika na Bodi za Mipango Miji na Upimaji. Kama nao wanaweza kuwakopesha hata kwa interest kidogo ili wabadilishe mfumo wa utendaji wao wa kazi, kwa sababu inaonekana hawana mitaji na ni Watanzania, wamesajiliwa na vyombo vinavyokubalika, kwa hiyo, wakipewa mikopo hii hata kwa riba kidogo, tutakuwa tunatengeneza ajira ndani ya nchi yetu na vile vile tunaongeza kasi ya upimaji na sasa hivi upimaji wao kwa kiasi kikubwa unategemea fedha za wananchi. Ndiyo maana utakuta takwimu zinaonesha makampuni binafsi yanawadai wananchi zaidi ya shilingi bilioni 70. Sasa kwenda kupima kutegemea hela ya wananchi ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naomba kule kwangu Ludewa, nami nina miji midogo mitano ambayo imetangazwa tokea mwaka 2001 ila bado haijapimwa; na wananchi wa Ludewa wanaamini kwamba Mbunge wao ni mtaalam mbobevu kwenye Sekta ya Ardhi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri na wataalam wako mniondoe aibu hapa ili tuweze kuwapimia wananchi. Kuna Kijiji cha Lugarawa, Mawengi, kuna Manda pale, kuna Beach Plots, kuna Kijiji cha Amani ambako miradi ya Mchuchuma na Liganga inakwenda, kuna Kijiji cha Mavanga na Mawengi. Kwa hiyo, maeneo haya bila kusahau Kata ya Mlangali pale, ni maeneo ambayo yameshaiva kimji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Nashukuru sana Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu aliwapokea Madiwani wangu, walikwenda pale Wizarani wakapata mafunzo. Kwa hiyo, wana ari ya kupokea hii huduma ya mipango miji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)