Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Kwanza kabisa, naomba nimpongeze Waziri wa Wizara ya Kilimo, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa jinsi walivyoanza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili naomba niwapongeze kwa sababu wameleta mikakati mizuri ambayo itatusaidia kutukwamua kwenye suala hili la kilimo. Pamoja na mikakati mizuri ambayo imetolewa na Wizara, lakini bado kuna changamoto ambazo zinatakiwa zitatuliwe ili tuweze kufikia malengo na kilimo chetu kiweze kuchangia kwenye Pato la Taifa kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitajielekeza sana kwenye upande wa utafiti. Changamoto kubwa ambayo nimeiona upande wa kilimo ni suala la utafiti. Changamoto nyingi ambazo zimetokana na suala la kilimo zinatokana na kukosa utafiti.

Mheshimiwa Spika, suala la kwanza, mimi natoka Mbinga kule Milimani ni wakulima wa kahawa na takriban sasa miaka 80 kilimo cha kahawa kinaendeshwa katika milima ile ya Umatengo. Changamoto iliyopo ni kwamba udongo ule umechoka. Kwa hiyo, tunaomba tafiti ya kupima udongo ili wakulima wale sasa waweze kupata ushauri mzuri utakaowasaidia kuongeza uzalishaji katika mashamba yale yale ambayo wanatakiwa waendelee kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utafiti unahitajika pia kwenye suala la pembejeo. Kama nilivyoeleza hapo mwanzo kwamba udongo ule umechoka na uzalishaji katika udongo ule bado ni tatizo na wakulima wale hawawezi kuhama katika maeneo yao ya asili. Kwa hiyo, leo usipopima udongo na ukajua wakulima wale wanatakiwa watumie pembejeo za aina gani ina maana wakulima watanunua pembejeo kwa kubahatisha, kitu ambacho hakitaleta tija kwenye uzalishaji wa kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la miche na mbegu upande wa mahindi. Unakuta kwamba kuna vituo vya utafiti havipewi nguvu za kuzalisha miche ya kutosha lakini kwenye suala la mbegu kuna kampuni nyingi sana zinazalisha mbegu lakini mkulima huyu hapewi maelekezo kwamba ni mbegu zipi sasa anatakiwa atumie ili aweze kupata mavuno mengi katika mazao yake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Serikali iongeze nguvu kwenye utafiti na kama utafiti huo unafanyika, unafanyika kwa manufaa ya nani? Kama huyu mkulima hajapata matokeo na ushauri kutoka kwenye utafiti huo, huo utafiti ambao unaendelea unafanyika kwa manufaa ya nani? Kwa hiyo, niiombe Serikali ihakikishe kwamba matokeo ya utafiti na ushauri yawafikie wakulima ili waweze kuzalisha kwa tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaongelea suala la wakulima ambao wako kule vijijini lakini wanahitaji msaada wa wataalam. Kama nilivyosema mwanzo kwamba utafiti kama umekamilika wale wataalam wanatakiwa wapeleke matokeo ya utafiti kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa waziri ametuambia kwamba wataalam waliopo ni takriban 7,000 lakini ukiangalia upande wa pili unakuta wataalam wale hawana vitendea kazi, sasa watafikaje kwa wakulima na kuwapa maelekezo kwenye masuala yanayohusu kilimo? Utakuta wataalam hawa hawana pikipiki, magari na hawawezeshwi mafuta ya kufika vijijini. Ni namna gani sasa hawa wakulima wetu ambao wako vijijini watapata utaalam ili waweze kuzalisha na waweze kuleta tija katika uzalishaji wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo nilitaka nilielekeze kwenye suala la kilimo kama walivyosema wenzangu ni miundombinu. Miundombinu yetu ni shida kwenye suala la barabara, hata kama utafiti na mambo mengine yatafanyika, lakini bado tutapata kikwazo kwenye suala la namna gani wataalam wanafika kule vijijini kwa wakulima na ni namna gani wakulima wanatoa mazao kutoka vijijini kwenye zile feeder roads ambazo ziko katika hali mbaya kupeleka sokoni. Kwa hiyo, hilo bado ni tatizo kwenye upande wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine naomba niishauri Wizara iache utaratibu wa kubadilisha sera mara kwa mara. Sera zinavyobadilika Bodi za Mazao pamoja na vyama vya ushirika vinashindwa kusimamia mazao kwa sababu hakuna sera endelevu. Kunakuwa na tatizo kwamba sera imetolewa leo baada ya miezi sita maelekezo mengine yanatolewa. Kwa hiyo, kwenye mpango mkakati wa muda mrefu ni vigumu kuutekeleza kwa sababu kunakuwa na mabadiliko ya maelekezo ya kiutendaji mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni masoko. Suala la soko ni tatizo kwenye mazao, kwetu ni zao la kahawa na mahindi. Kwenye zao la kahawa niipongeze Serikali imeanzisha ile minada ya kanda, lakini mpaka mkulima anapeleka mazao yake sokoni hajui gharama za uzalishaji wala hajui atauza kwa bei gani na hajui kama akiuza kwa bei ile italipa gharama zile za uendeshaji. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba zile tafiti kama zingekuwa zinafanyika zingekuwa zina uwezo wa kumuelekeza mkulima ili ajue zile gharama anazotumia baada ya kuuza mazao yake fedha zake zilizotumika zinarudi na mkulima huyu anakuwa amezalisha mazao haya kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa mahindi kuna tatizo kubwa sana nalo linalotokana na soko kwamba wakulima wale wanalima kwa gharama kubwa na ni wakulima wadogo wadogo wanalima kwa jembe la mkono, lakini bado wanapata tatizo la soko kwenye upande wa mahindi.

Mheshimiwa Spika, kama mwaka 2020 wakulima wetu wa Mkoa wa Ruvuma, Wilaya ya Mbinga na Songea Vijijini, kwa dada yangu Mheshimiwa Jenista wametapeliwa mahindi yao ambayo ni ya thamani kubwa na mpaka sasa hivi hawajui hizo fedha zitalipwa kwa namna gani? Hawajalipwa, Serikali ipo, inaona, lakini mpaka leo wakulima wamekopa kwenye benki na…

SPIKA: Wametapeliwa na nani?

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, wametapeliwa na mfanyabiashara mmoja anaitwa Njau na mpaka leo hawajui ni namna gani hela zao zitapatikana. Kwa hiyo, naomba wakati Mheshimiwa Waziri anahitimisha hapa atamke Kauli ya Serikali kwamba inasema nini kuhusiana na hawa wakulima ambao wamepoteza mazao yao.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)