Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru wewe mwenyewe binafsi, kwa kadri jinsi unavyoiendesha taasisi yako hii ya Bunge. Lakini nimshukuru pia Naibu Spika kwa kazi hiyo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze katika sekta hii ya kilimo, Sekta ya kilimo imekuwa ni sekta nzuri ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa sana uchumi wa nchi hii. Kwa muda wote sekta ya kilimo imekuwa namba moja katika uchangiaji katika uchumi wa nchi hii. Kwa mfano, mwaka 2018 sekta hii ilichangia kwa takribani asilimia 27.9 ya bajeti nzima. Lakini pia mwaka 2019 ilichangia kwa takribani asilimia 26.6 kwenye bajeti ya nchi nzima. Lakini imeendelea pia kuchangia sekta hii katika ajira, asilimia 58 ya ajira zinazopatikana katika nchi hii zinachangiwa na sekta ya kilimo. (Makofi)

Halikadhalika asilimia 65 ya malighafi (raw materials) inachangiwa na sekta ya kilimo. Baada ya kuona umuhimu wote huu bado Serikali imeendelea kuwa na kigugumizi kikubwa katika kuhakikisha kwamba sekta ya kilimo inapata haki inayostahili. Serikali imekuwa haioneshi weledi wake katika kuchangia sekta hii kikamilifu. Naomba kwa namna moja au nyingine, Serikali ioneshe nguvu zake zote kwenye sekta ya kilimo kusudi tuweze kufanya mapinduzi ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi tunatumia jembe la mkono, maeneo mengi sana jembe la mkono limekuwa siyo Rafiki. Hali hii imesababisha mpaka vijana ambao ndiyo wengi katika nchi hii kushindwa kujiingiza katika sekta ya kilimo kwa sababu ya ugumu wa matumizi ya hili jembe la mkono. Kwa hiyo, naiomba Serikali itilie mkazo kwa kiasi kikubwa kuiinua sekta hii ambayo inabeba ajira za wananchi walio wengi hasa wananchi walioko pembezoni vijijini huko.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali pia inaona shida gani kutumia sekta zake tofauti, kwa mfano sekta ya fedha kama benki, kuyaamrisha au kuyapa taarifa kwamba wawakopeshe wananchi. Kuna ugumu gani kwa sababu hii ni sekta muhimu na kilimo kinakopesheka. Wananchi wote ambao wanashughulika na kilimo wanakopesheka.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia mfano mdogo tu wa zao la korosho limetoa dola takriban bilioni 589. Hizi ni fedha nyingi sana, ni trilioni 1.3. Nashangaa kwa nini Serikali imekuwa na kigugumizi kuwekeza katika kilimo kwa sababu hii trilioni 1.3 ni takriban asilimia 4 ya bajeti nzima. Ukiangalia ni mchango mkubwa sana, sioni sababu kwa nini Serikali haijajielekeza kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, sisi pia tumejitambulisha kuwa tunataka kuendesha uchumi wa viwanda. Uchumi wa viwanda hauwezi kufanikiwa pasipokuwa na sekta ya kilimo. Kama tulivyoona pale kwamba asilimia 65 ndiyo inapeleka pale kama malighafi, sasa ugumu uko wapi?

SPIKA: Unajua Mheshimiwa Mchungahela, Waheshimiwa tuwe tunawasikiliza Wabunge wanaochangia. Huyu ni Mheshimiwa Issa Mchungahela wa Lulindi, unajua kule Kusini zamani neno mhasibu halikuwepo walikuwa wanaitwa wachungahela. (Kicheko)

Mpaka sasa hivi Mheshimiwa hueleweki kwa kweli, yaani hujajikita moja kwa moja kujaribu kueleza kitu chako, unapiga theory. Hebu endelea kidogo lakini shuka kwenye kitu ambacho unataka kifike.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, nilitaka kujikita kwenye korosho. Korosho kwa namna moja au nyingine iko wazi kabisa kwamba inachangia kiasi kikubwa kwenye uchumi lakini pia kwenye ajira ya wananchi wa Kusini kwa sababu ni pesa nyingi sana ambazo Serikali inapata kupitia kwenye korosho.

SPIKA: Yaani mtu anaweza akakuuliza swali, haijajikita vizuri kivipi, unataka kusema nini? (Kicheko)

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Ahaa.

T A A R I F A

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Ndiyo, taarifa, nimekusikia.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Mchungahela, anaposema Serikali haijajikita ipasavyo kwenye kulisaidia zao la korosho, hivi tunavyozungumza hata Bodi ya Korosho yenyewe haijaundwa. Bodi ile ya Korosho kwa sasa inakaimu Mkurugenzi hamna analolifanya. Kwa hiyo, napenda kumpa taarifa msemaji anaposema Serikali haijajikita alijumuishe na jambo hilo la Bodi ya Korosho. (Makofi)

SPIKA: Yaani anasema lilelile nililokuwa nakushauri mwanzoni, unaposema kitu hebu fika mwisho.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Yes! Napokea taarifa Mheshimiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nataka kusisitiza kwamba hata jitihada zinazofanyika sasa hivi za kupeleka pembejeo, hizo pembejeo mpaka sasa kuna maeneo ya Jimbo langu ambapo ndipo panapozalishwa korosho mapema sana, sasa ni kipindi cha maandalizi ambapo pembejeo zinahitajika lakini hazijafika. Kwa hiyo, nilikuwa najaribu kuonesha pia katika mazingira hayo kwamba kwa namna moja au nyingine umakini sana unatakiwa katika utekelezaji wa yale tunayoyazungumza.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Issa Mchungahela, bahati mbaya dakika zimeisha. Nakushukuru sana sana kwa mchango wako.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)