Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri, kwa hotuba nzuri ambayo inalenga Tanzania kuwa nchi ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa sekta ya viwanda na biashara kwa maendeleo ya kiuchumi ya nchi na watu wake unahitaji mtazamo tofauti. Nchi za Tiger (Tiger nations) zimeendelea kiuchumi ukilinganisha na Tanzania kwa sababu ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiasi kikubwa sekta hii inaleta ufunguo wa sekta nyingine hasa kilimo. Serikali iweke mkazo kwenye viwanda vidogo vidogo vya kuongeza thamani za mazao ya kilimo. Kutokana na kazi nzuri ya REA, napendekeza kuangalia uwekezaji mdogo mdogo wa viwanda vijijini ili kuongeza thamani ya mazao yetu na pia kuongeza ajira kwa vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa la mitaji linaweza kutatuliwa na benki mpya ya kilimo (TADB). Napendekeza milioni 50 kwa kila kijiji, zipelekwe TADB, kwa kusimamia hizo pesa ambazo ni mfuko wa kuzunguka (Revolving Fund) kwa kila kijiji. Hii itawezesha TADB kutoa huduma moja kwa moja kwa wakulima ikiwa ni pamoja na kuiongezea mtaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufanikisha ufanisi wa viwanda na biashara ndogo ndogo, ni muhimu kutoa elimu za muda mfupi kwa vijana na hasa wa vijijini, ili ujasiriamali uwe na tija na mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na umuhimu wa kufufua viwanda vyetu, zoezi hilo liendeshwe kwa uangalifu mkubwa kutokana na kubadilika kwa teknolojia na ushindani mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Mbeya, imetenga eneo mahsusi katika kijiji cha Mjele kwa ajili ya Kiwanda cha Nyama na bidhaa zingine zitokanazo na mifugo. Hilo eneo ni mbadala wa eneo lililokuwa la Tanganyika Packers ambalo kwa sasa limezungukwa na makazi ya watu (Mji mdogo wa Mbalizi).