Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, niungane na Wabunge wenzangu wanaotoka mikoa ya kusini. Moja niunge mapendekezo ya Kamati ya Kilimo kuhusu Sheria ile ya Mfuko wa kuendeleza zao la korosho ambao mwaka 2018 Spika ukiwa kwenye Kiti hicho ililetwa sheria ile tukaibadilisha Sheria Na.17A. Kamati imependekeza vizuri kwamba sheria ile irejeshwe ili kumlinda mkulima huyu ambaye asilimia 65 ya fedha ile ilikuwa inakwenda moja kwa moja kwenye pembejeo, Bodi ya Korosho na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, mheshimiwa Nape amezungumza jambo mahususi hapa kwa sababu kwa matamko ya Serikali yenyewe ilisema fedha zile bilioni 200 ilizichukua baada ya kuona Bodi ya Korosho imeshindwa kuzisimamia vizuri. Sasa na Serikali nayo imeshindwa kuzisimamia vizuri mara tatu kuliko yale yaliyokuwa yanafanywa na Bodi kwa sababu kwa miaka minne au mitatu tumeishi hatuna Bodi ya Korosho, fedha zimechukuliwa na Serikali, wakulima hawana pembejeo na uzalishaji umepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe sana kwa sababu fedha zilitunzwa, tunajua zimetumika mahali pengine lakini Serikali igharamie pembejeo hizi ambazo leo Wizara imefikiria jambo jema lakini approach yake inakwenda kumuongezea mzigo mkulima. Unaposema mkulima aendelee kuchangia 110 wakati Serikali imechukua bilioni 200 ya fedha za wakulima, nadhani Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Bashe ulikuwepo na ulikuwa unaunga mkono kwamba wakulima wanadhulumiwa, sasa ukae na Serikali hiyohiyo umepewa dhamana ya unaibu Waziri, Profesa ufanye kazi hii muiombe Serikali itupe bilioni 55/60 iende kulipa pembejeo wakulima wapate pembejeo mtakuwa mmewasaidia sana wakulima wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali inachukua bilioni 200 ilisema ingelipa gharama zote yenyewe, mwaka jana Serikali imechukua tena shilingi 25 kuchangia gunia za fedha ya korosho 2017/2018. Fedha ambayo wameikata kwenye mjengeko wa bei toka mwezi wa kumi lakini mpaka leo hao wenye magunia hawajalipwa hiyo fedha, fedha imechukuliwa wanaodai magunia hawajapewa lakini ni Serikali ilibeba mzigo wote kwamba tungeweza kulipa korosho hizi fedha, tungelipa magunia; wenye magunia wanadai, watu wa pembejeo wanadai na fedha zimechukuliwa.

Mheshimiwa Spika, niombe kwa sababu tuna Serikali Sikivu sana, na Mawaziri mpo makini kwelikweli lakini sijui shida mnaipata wapi, shida mnaipata wapi? Kaeni na Serikali muiambie kwamba tulikopa fedha za wakulima wa korosho maana zile mlisema matumizi sio mazuri, haya matumizi sio mazuri mmeshindwa kuunda Bodi ya Korosho, kwa miaka mitatu hakuna Bodi ya Korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkaja na ngonjera nyingine ambayo siiafiki kabisa eti uunganishe bodi za mazao haya ipatikane bodi moja, tuache bodi za kila zao libaki lenyewe litashughulika vizuri kuliko hayo mambo anayokuja nayo yaani Bodi ya Korosho, Bodi ya Pamba, Bodi ya Nini utengeneze dubwana moja Mheshimiwa Rais ndiyo maana alimuondoa Meya wa Jiji la Dar es Salaam kwa kuona kwamba unatengeneza mtu amekaa tu pale kama picha, acheni tupate Bodi ya Korosho ambayo itasimamia zao na Sekta ya Korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana, Mheshimiwa Nape kawakumbusha hapa miche ya korosho ambayo imekuja mpaka Dodoma watu wake hamjawalipa, fedha zilikuwepo za kutosha, zilikuwa zinaweza kugharamia Sekta ya Korosho, lakini hatuna cha kujifunza. Msumbiji ambao wamekuja Tanzania kujifunza mfumo wa stakabadhi ghalani wanatoa pembejeo kwa wakulima bure kwa miaka 13 sasa, wamekuja kujifunza Taifa hili nyinyi waliokuja kujifunza ndiyo kwanza mnawaza tupate 110 tumkate mkulima, tufanye hivi, tunajifunza kutoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbona Ethiopia tulikojifunza sisi wanampa mkulima pembejeo bure, magunia bure, mabomba ya kupuliza korosho bure kila kitu wanafanya bure Serikali, mnapokusanya asilimia 15 ya export levy kwenye tani zile ulizokusanya 2016/2017/2018 laki tatu mnakusanya zaidi ya bilioni 144 ambazo mkichukua bilioni 55 mnaweza kugawa mapembejeo hayo na bado Serikali mkabakiwa na bakaa, mkawa mnamnyonya ng’ombe maziwa huku unamlisha.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali hii unamnyonya mkulima humlishi, mkulima huyu ataendeleaje? Mnasema asilimia 65 ya watanzania ni wakulima, wakulima ambao hawapewi pembejeo, wakulima ambao hawapewi magunia, wakulima ambao wakati wa kilimo hakuna mafunzo mnawapa, wakulima ambao kila jambo wanafanya wenyewe (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana, Mheshimiwa Waziri translate sasa u-professor wako kwenda kwenye vitendo vya kumsaidia mkulima, tusiwe tunajisifia ma- professor mpo tunakata ma-professor mtafsiri elimu yenu ije kwenye manufaa add value addition kwa wakulima wa korosho tutakaa tutapongeza tunama-professor chungu nzima, tuna madaktari chungu nzima, tafsiri elimu yenu kwenda kwenye value addition ya wakulima wa korosho, kwenye value addition ya wakulima wa mahindi, wakulima wamekuwa wakilalamika kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Taifa hili linautajiri wa kutosha kutoka kwenye kilimo, korosho tunayoisema hata Marehemu Mheshimiwa Rais, Mungu amrehemu alishasema kwenye korosho kama leo mtaamua kuwekeza vizuri kwenye korosho mkaleta viwanda, maganda ya korosho yanatengeneza brake pad ya kwenye magari tena Mercedes – Benz, maganda. Mafuta yanayotokana na korosho unaenda kutibu mbao zile za Mufindi haingii na mchwa hata mmoja hawezi kuharibu mbao, mabibo ya kwenye korosho leo mkiamua kufanya yawe na thamani tunaweza kutengeneza juisi, tunaweza kutengeneza pombe, Ulaya mkauza mapombe, mkulima wa Tanzania asingekuwa maskini hata dakika moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waziri kaeni mtafakari jambo hili, Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake amesema vizuri sana anataka kuona wakulima wakinufaika, Waziri onyesha mfano huo, tuanze na kwenye korosho huku, ombeni fedha, pembejeo hizi mtoe bure, lakini mkiangalia tathimini mliyoifanya natoa tani 8730 za Sulphur. Lakini nenda kwenye jedwali zenu 2017/2018 ambapo tumezalisha tani 313 Sulphur iliagizwa tani 18,000, nyinyi mmeagiza tani 8730 maana yake hatuendi kuongeza uzalishaji mnaoukusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye dawa za maji tuliagiza lita laki tatu na, leo mmeagiza lita 82,438 hamuendi kutoa majibu ya wakulima, hamuendi kutoa majibu na hiyo ipo kwenye hotuba zenu, mkae mfanye tafakari ya kina, tunahitaji mkusaidia mkulima huyu, mkulima ambaye anapata shida watu wamezungumza hapa adha ambazo mkulima anapata. (Makofi)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Katani.

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, shukurani sana. (Makofi)