Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi. Naamini kabisa tunakubaliana kwamba Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi ni sekta muhimu sana kwa Taifa letu na ndiyo maana tunasema tunachangia asilimia 25 ya fedha za kigeni, lakini zinachangia asilimia 30 ya pato la Taifa, zinachangia asilimia 65 ya ajira na zinachangia asilimia 100 ya chakula.

Mheshimiwa Spika, tunakubaliana pia kwamba kwa mwaka tuna wastani sasa hivi wa kuagiza chakula cha thamani ya trilioni 1.3. Sasa tu niseme nimesikia hapa wadau wazalishaji wa mbogamboga, matunda, maua na viungo wako kwenye Bunge lako hili. Nachukua nafasi hii kuwapongeza sana kwa sababu kati ya sekta ambazo zimefanya vizuri katika miaka mitano iliyopita 2015 - 2020 ni hiyo sekta ya wazalishaji hao ambao nimesikia wapo hapa pamoja na CEO wao Jacqueline Mkindi ambao uzalishaji ulikuwa milioni 400 tuliweza kuuza maouzo yetu ya nje milioni mia nne kumi na mbili mwaka 2015 ilipofika mwaka 2020 tayari wameshafika milioni 779, karibu mara mbili. Kwa hiyo, ni moja ya eneo linaenda vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, tunazungumza hiki kilimo chetu cha wananchi wetu hawa ambacho kimekumbwa na mzigo mkubwa wa matatizo, kimebeba mzigo mkubwa wa matatizo. Hapa wenzangu wamezungumzia suala la watumishi, watumishi wamesema wako 6,000 na kitu hapa, lakini wengine wako wilayani, hawapo kwa wakulima kwa hiyo tuna vijiji karibu 7,000, havina Maafisa Ugani. Sasa kama huna Afisa Ugani, ni nani anawaongoza wananchi wako, nani anakagua magonjwa ya wananchi katika mimea yao, nani anayewaongoza wakulima kupata mbegu bora, nani anayetibu mimea yao na kama hakuna wa kutibu na sisi ndiyo tunasema hili eneo ndiyo uti wa mgongo, ni uti wa mgongo gani ambao hauangaliwi hata ukipata magonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuna suala hili la mbegu bora. Mheshimiwa Waziri amezungumza mambo ya mbegu bora hapa. Kwanza mbegu zinazozalishwa ni chache na hazitoshi, lakini gharama yake ni kubwa sana, tatizo la gharama limetatuliwaje? Mbona hatujaelezwa kwenye hotuba yake kwa sababu wananchi wengi wanashindwa kununua mbegu kwa sababu ya gharama kubwa sana, kilo moja unaambiwa Sh.6,000/=, Sh.7,000/= au Sh.8,000/=, nani atanunua? Kamfuko kamoja ka kilo mbili unauziwa Sh.10,000/ na zaidi nani atanunua?

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ni kubwa sana, Wabunge wenzangu wamezungumza hapa, ni suala la bei na suala la masoko. Wananchi wetu wana tatizo kubwa sana la masoko na tatizo linalotupeleka kwenye masoko hapa ni kwa sababu tunauza malighafi nje ya nchi. Tutaacha lini kuuza malighafi katika masoko ya Ulaya, tutaacha lini kuuza malighafi masoko ya China, India na sehemu zingine za AGOA na kwingine na kwanini tuendelee kuuza malighafi? Ni lini tutajenga viwanda vyetu wenyewe na kwa nini tusiamue leo na kukataa kuuza malighafi nje ya nchi? Tukiuza malighafi nje ya nchi wananchi wetu wananyonywa bei, wananchi wetu hawapati kipato kinachostahili, ajira tunaziuza nje, Watanzania wanageuka kuwa manamba wa kufanyia kazi viwanda vya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kujenga viwanda vya kimkakati shida kubwa ni mitaji kwa baadhi ya watu. Nani atakuja akujengee kiwanda hapa cha pamba wakati pamba anaweza akaichukua kwa bei ya kutupa, akaipeleka China, aka-process, akakuletea nguo, pamba ya s Sh.3,000/= akaja kukuuzia shati la Sh.50,000/= au Sh.100,000/=, nani atakuja kujenga kiwanda hapa? Kwa nini tusifanye maamuzi kama tulivyofanya kwenye umeme au kama tunavyofanya kwenye miundombinu ya barabara? Tukajenga viwanda hapa, tunajenga kiwanda kikubwa cha nyuzi, tukajenga kiwanda cha nguo, tukajenga kikubwa kiwanda kikubwa cha korosho kwa kutenga fedha zetu wenyewe, hata kama sisi Serikali tusipoendesha Watanzania wako wa kuendesha./ Tunajenga kiwanda kama ni cha bilioni 100, tunawakabidhi Watanzania waendeshe.

Mheshimiwa Spika, pia tunaweza kuwapa mikopo ya masharti nafuu, hata ya miaka 30, tatizo liko wapi? Leo hii tungekuwa na viwanda vyetu tusingekuwa tunapata matatizo haya, wananchi wetu wangenufaika kwa bei nzuri, lakini Taifa lingepata kodi nzuri katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tu ya muda, niseme pia kwamba, viwanda hivi tunaweza kuvijenga, lakini tatizo tulilonalo lingine ni ulinzi wa viwanda vyenyewe, viwanda vingi vilikuwepo, vingine vimekufa, vingine vimefungwa na wawekezaji wengine hawatakuja. Moja linalofanya viwanda vyetu viwe na changamoto kubwa ni mfumo wa kodi mbaya, unsupportive taxation regime yetu haifanyiwi tathmini mara kwa mara. Unaweza kukuta wakati mwingine hata mazao ya kutoka nje ya nchi yanakuwa exempted, wazalishaji wa ndani wanapigwa kodi, wale wanaoingiza mazao hayo ndani ya nchi na bidhaa hizo ndani ya nchi wamesamehewa. Sasa atashindanaje mwenye kiwanda hapa ndani? Hawezi kushindana.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa huu mfumo nilitegemea Wizara ya Kilimo wangeleta tathmini hapa ya kodi ambazo zina changamoto kubwa, tuna changamoto kubwa sana kwa mfano kwenye maziwa, ngano na kadhalika. Wazalishaji wa ndani ya nchi wanapigwa kodi lakini wanaoingiza wanasamehewa kodi, sasa nani atawekeza viwanda ndani ya nchi yako. Matokeo yake tuna mfumo wa ku-favour watu wanaoingiza bidhaa ndani kuliko wale wanaozalisha wakauze ndani. Huwezi kupiga hatua kwa namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, lingine ni ulinzi wa viwanda vyenyewe, viwanda hivi vinalindwaje wakati bado kuna importation kubwa ya mazao mengine kutoka nje ambayo sambamba na haya yanayozalishwa hapa nchini, mengine yanaingia holela bila kufuata utaratibu, hawalipi kodi wala hawafanyi chochote, wanaingiza na kuuza mazao hapa. Ulinzi unafanywaje na Wizara ya Viwanda na Biashara, ulinzi unafanywaje na Wizara ya Kilimo, ulinzi unafanywaje na vyombo vyetu vya dola, hapa kuna viwanda vinakufa kwa sababu ya kukosekana kwa ulinzi wa kulindwa viwanda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hata mipango yetu mingine tunaanza tena, wananchi wanahangaika kuuza hiyo malighafi, tunaleta ushirika wa kuua wanunuzi wengine, unatengeneza ushirika wa kwenda kuua wanunuzi wengine, matokeo yake wananchi wanakopwa mazao yao hawalipwi, wengine wanapoteza kabisa fedha zao na wengine wanacheleweshwa fedha zao halafu kwenye Kijiji kimoja wanakuwepo wanunuzi wapo kumi unaenda kuamua awe mnunuzi mmoja; unaua ajira zote, Na Waziri hapa kwenye hotuba yake anazungumza ana… (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: …anazungumza mambo ya ajira ya vijana wakati umeenda kuua ajira za vijana kwa kuthamini ushirika peke yake na kuwaondoa vijana waliokuwa wamejiajiri; kwa nini usiweke ushirika wenye pesa na vijana wanaonunua kivyao wakanunua halafu wakashindwana kwenye bei, wananchi wakaenda kuuza kwenye bei nzuri iliyokubwa aidha ya ushirika au ya mtu wa kujitegemea, tatizo liko wapi? Sera zetu zinakinzana na tunachotaka kufanya. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)