Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ISSAAY Z. PAULO: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuungana na viongozi wa Taifa letu kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote kama Taifa kupitia majanga mbalimbali hususan janga la corona, kimbunga cha jobo kule Mtwara na mengi kadha wa kadha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupokea uongozi wa Taifa letu. Hivyo tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu amjalie ulinzi na baraka katika kuongoza Taifa letu tuwe kielelezo mbele ya mataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge letu navipongeza sana vyombo vyetu vyote vya ulinzi na usalama, kama nchi siyo rahisi kutambua haraka kujua kazi kubwa ya vyombo vyetu vya ulinzi ndani ya nchi na nje ya nchini. Nayasema haya kwa sababu majeshi yetu ni nguzo ya tunu ya amani na utulivu ulioko nchini kwetu. Hivyo basi sisi kama Bunge tuwe mstari wa mbele tuwatetea kupata stahiki zao mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini nachukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015 na 2020 kwa jimbo langu la Mbulu, hongereni sana wadau mbalimbali walioshiriki kwa kwa hali na mali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee naungana na Watanzania wote kumwombea sana Mheshimiwa Hayati John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano kwa kweli kama Taifa mchango wake tutaukumbuka daima. Ee Mwenyezi Mungu umpokee mtumishi wako mwaminifu, mzalendo, mtiifu mwana mapinduzi wa Afrika katika ufalme wako wa milele mbinguni, Amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha naungana na waheshimiwa viongozi wa Taifa letu, Bunge zima, Watanzania wote kwa ujumla kutoa pole nyingi kwa msiba wa kifo cha mpendwa wetu Mheshimiwa Hayati Khatib Said Haji, Mbunge wa Jimbo la Konde, Mwenyezi Mungu ampokee katika ufalme wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa ushauri wangu kupitia bajeti hii ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa nikianza na kutokana na changamoto kubwa sana ya makazi ya askari, upungufu wa magari na vitendea kazi hivyo Serikali ijitahidi kupeleke fedha zote zinazopangwa kwenye bajeti zetu kwani hali ni mbaya sana ili majeshi yetu yatekeleze majukumu yao kwa weledi mkubwa kuendana na utandawazi mkubwa duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema hayo kwa sababu nimehudumu kwenye Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Serikali yetu haijafanikiwa kupeleka fedha za maendeleo kwa zaidi ya 50% zinazopangwa.

Pili, kutokana na vijana wengi kujiunga na JKT na baada ya kuhitimu wanarudi uraiani. Ni wakati sasa wa kuona kuwa na matawi ya SUMA JKT kwa ngazi ya mikoa ili kuchochea fursa za ajira kupitia matawi hayo. Kuna umuhimu wa kutoa maelekezo ya Serikali kuajiri vijana wote kwenye ulinzi katika taasisi za umma kama vile halmashauri, elimu, afya na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie umuhimu wa dhana ya uraia na uzalendo ambao ndiyo nguzo muhimu sana kwa kila Mtanzania ili kuwajengea vizazi vyetu na Watanzania kwa ujumla kwani ni dhahiri kuwa vijana wote wanaohitimu JKT hawataweza kupata nafasi za ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa vijana wengi wanaojiunga na JKT toka awali hawajiandai kisaikolojia kuwa lengo lake ni kujiari hivyo ni muhimu toka mwanzo wa kujiunga vijana wetu waulizwe hulka yake ni nini katika kujiajiri kama sekta za kilimo, ufundi, ufugaji ili kubaini anapaswa kwenda kambi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naunga hoja mkono asilimia 100 na naomba kuwasilisha.