Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU): Mheshimiwa Naibu Spika, nami naanza kwa kushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nachukua nafasi hii pia kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa kazi ya kumsaidia na hasa kumsadia Waziri Mkuu ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba nimhakikishie nitakuwa mtumishi mwema.
Vilevile nawashukuru pia wapigakura wa Jimbo la Peramiho, nawaambia Hapa ni Kazi Tu, wasibabaishwe na kelele za mpangaji wakati sisi wenye nyumba tupo, tunaendelea kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mheshimiwa Rais wetu ametupa kazi kadhaa za kufanya. Naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu na hasa kwa kuonyesha kwa vitendo anajali makundi maalum na hasa ya walemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu amelidhihirisha hilo kwa matendo. Chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mheshimiwa Rais amemteua Naibu Waziri anayeonyesha kama ni kielelezo cha watu wenye ulemavu katika nchi yetu ya Tanzania wanaweza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kwanza kuwapongeza Wabunge wote kutoka katika kundi hilo na Watanzania wote kutoka katika kundi hilo ambao wameonyesha umahiri mkubwa katika kutoa mchango wao kwenye maendeleo ya Taifa letu bila kusita na kuonyesha kwamba kundi hili ni kundi muhimu katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2010 tumetunga Sheria Na.1 ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kusimama katika maneno ya Mkataba wa Kimataifa ambao unatoa haki za binadamu na hasa kwa kundi la watu wenye ulemavu. Mkataba huo tuliuridhia mwaka 2008, mwaka 2010 tumetunga sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hotuba ya Rais inatukumbusha, watu wenye ulemevu wana haki sawa na Watanzania wote. Kwa niaba ya Serikali na kwa maagizo ya hotuba ya Rais, tutakwenda kusimamia wapate haki sawa kwenye elimu, wapate haki sawa kwenye afya, wapate haki sawa kwenye ajira, wapate haki sawa kwenye masuala yote ya uchumi. Hiyo ni kazi tumepewa katika hotuba hii ya Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka kuondoa kila dhana ya unyanyapaa. Kumekuwa na tabia imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge kwamba wapo watoto wenye ulemavu wanafungiwa na hata jamii zetu zimekuwa zikiwachukulia watoto wenye ulemavu, kwa mfano wenzetu wenye ulemavu wa u-albino wafungiwe mahali fulani kwa ajili ya ulinzi na usalama. Katika mipango tulionayo sasa, tumeanza kuona ni namna gani watu hawa walindwe lakini watolewe nje wakawe na wao ni part ya jamii ya Watanzania katika kuleta maendeleo na kupatiwa maendeleo endelevu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi nyingine kubwa ambayo tumepewa pamoja na kusimamia sera, maafa na mambo mengine yote, matatizo ya dawa za kulevya na UKIMWI, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kazi hiyo tunaifanya sawia. Tutapambana na dawa za kulevya, hakuna kurudi nyuma, tutaendelea kupambana na ugonjwa wa UKIMWI hakuna kurudi nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge lililopita tulishatunga sheria, tutazisimamia na ole wao watakaoendeleza biashara ya dawa za kulevya, sheria ile itafanya kazi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumepewa kazi nyingine kubwa ya kuhakikisha kwamba tunaongeza ajira katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, katika hotuba yake ametuagiza, katika kuhakikisha Watanzania wanaondokana na tatizo la ajira mpango huu wa kuwezesha sekta ya viwanda, ifanye kazi ya kutosha kati ya Wizara yetu lakini na Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakikisha huu mpango wa sekta kubwa ya viwanda vidogo, vya kati na viwanda vikubwa, iweze kuchukua asilimia 40 ya nguvu kazi ya Taifa. Waheshimiwa Wabunge, tutafanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kuimarisha mifuko tuliyonayo sasa. Waheshimiwa Wabunge mmesema vijana wetu wanamaliza vyuo, hawana mikopo, vijana wana uwezo wa kuongeza stadi walizonazo ili kuchangia pato la Taifa na kujiajiri, wanashindwa kupata uwezo wa kufanya hivyo. Tumejipanga kuimarisha mifuko hiyo, iwape vijana wetu mikopo yenye riba nafuu na Waheshimiwa Wabunge tunaendelea kuwasiliana, tutaleta mipango hapa Bungeni muiunge mkono, tunataka kuonyesha mwaka 2020 haya yanawezakana; na tuwawezeshe vijana wetu kuweza kuajiriwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutatekeleza mikakati mingine ambayo tayari iko ndani ya Wizara, kwa mfano kukuza ajira kwa vitendo na tutashirikiana na Halmashauri zetu kuhakikisha tunafanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tutakapopata muda, tutatoa maelezo ya kina. Nachukua nafasi hii kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais na ninampongeza sana. (Makofi)