Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Eng. Ezra John Chiwelesa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi pia nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Ulinzi na nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Ulinzi kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo machache ya kuchangia kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Biharamulo nadhani taarifa zangu nilishakaa na Waziri pia lakini ningeomba jambo hili niliweke sawa kwa ajili ya records na kwa ajli ya wale ambao wamenituma, maana nilikuwa Jimboni juzi na jana kelele kubwa ni kwa ajili ya mgogoro wa muda mrefu kati ya Kikosi cha 23KJ na wananchi wa Kata ya Nyarubungo katika Vijiji vya Rusabya na Kata ya Ruziba vilevile katika vijiji vya Ruziba lakini na kata ya Biharamulo mjini sehemu ya ng’ambo Lukoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo mwaka 1984 wakati kambi ya jeshi inaletwa pale Biharamulo tayari wananchi walikuwa wanaishi katika vijiji hivi na ikafanyika tathmini, ilipofanyika tathmini wananchi wakaamuliwa wasifanye maendelezo yoyote yale kwa sababu tayari ilikuwa ni sehemu ambayo imetengwa kwa ajili ya kufanya mazoezi ya kikosi cha 23KJ na hivyo wananchi wakabaki stranded kwa sababu hawakutakiwa kuendeleza nyumba wala kulima au kufanya chochote kile. Lakini tangu mwaka 1984 wananchi wale hawakulipwa wala hawakufikiwa chochote kile. Kwa hiyo ninavyosimama kuongea ni miaka 37 tangu wakati ule, wanachi wamekuwa katika sintofahamu ya muda mrefu na zaidi wakiendelea kuilaumu Serikali kwa kitu hiki ambacho kilifanyika, lakini pia mwaka 1998 iliundwa kamati nyingine ndogo iliyohusika viongozi wa kijiji, ilihusisha viongozi wa Wilaya pale, Afisa Ardhi na watu wengine wakapitia tena upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninasema sio mgogoro ila ni changamoto ambayo imekuwepo kwasababu hata jeshi lenyewe ambalo llimechukua eneo lile ni eneo ambalo lipo ndani perimeter ya kilometa tano kutoka katikati ya mji wa Biharamulo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hata jeshi lenyewe ni kwamba haliwezi kutumia eneo lile ambalo limetengwa kwa sababu ni eneo ambalo lilitengwa kwa ajili ya kufanyia mazoezi, lakini kwa sababu wananchi wale hawakulipwa inaonekana sio mali halali ya jeshi kwa sababu jeshi haliwezi kusema kwamba ni male yake kwa sababu bado halijawalipa wananchi, lakini wananchi waliamuliwa wasiendelee kufanya kazi yoyote. Kwa hiyo kumekuwa na mvutano mdogo mdogo ambao unaendelea. Wananchi wale wanachoka kwasababu sasa ni eneo la mjini unapomtoa pale na ukampeleka sehemu nyingine ni kwamba wamekosa sehemu za kufanyika kazi, maana hata maeneo yale ambayo ilibidi wakimbilie wamekimbilia kwenye kata moja ya Nyamahanga eneo moja linaitwa Kibale lakini hata kule walipo bado ni maeneo ambayo wameenda na kuwakuta watu wengine kwa hiyo wameenda kuanzisha mgogoro na watu wengine tena pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilichokuwa naomba kipindi Waziri ana-wind up tuje na majibu sasa tujue wananchi hawa ambao wamekaa kwa miaka 37 wakisubiria kujua hatima yao ni nini kinaendelea, maana kabla ya mimi kuingia Bungeni niliambiwa kwamba mwaka jana kuna Tume ziliundwa na Mawaziri nadhani wakazunguka kupitia maeneo ambayo yalikuwa na migogoro, lakini kwa Biharamulo hawakufika na maswali ambayo nimekumbana nayo sana na wananchi wale bado wanalalamika kwasababu wanasikia watu walienda sehemu nyingine Biharamulo hawakufika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa ninaomba Serikali itupe majibu ya kina na ya ufasaha ili wakazi hao ambao wameachia maeneo yao, maeneo ya Rubasya, maeneo ya Ruziba, maeneo ya Ng’ambo ili wajue hatma yao ni nini (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hata jeshi nalo pia haliwezi kuyatumia maeneo yale kwasababu kuna kipindi katika kufanya range walipiga risasi wakati wanajeshi wanafanya majaribio pale wananchi wakaja kuokota maganda wakaleta complain nyingi sana kwamba ni kama vile wameshambuliwa na nini. Kwa hiyo, nilikuwa ninaomba hili jambo liangaliwe kwa sababu ninachoelewa kazi kubwa ambalo jeshi linayo pale ni kazi ya kuhamasisha, kuelimisha wananchi juu ya masuala ya ulinzi wa nchi yetu ili waweze kushiriki katika kulinda mipaka ile na mkizingatia sisi tupo mipakani kule. Sasa wananchi wale ambao inabidi muwaelimishe na watusaidie kulinda mipaka ile, wanapokuwa wana-feel kwamba kama wameonewa au wamedhulumiwa eneo lao sidhani kama watakuwa walinzi wazuri wa mipaka kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyote ni mashahidi kwamba sisi ambao tupo maeneo yale wenzetu wa nchi jirani wakati mwingine wanaingia na ndio hao wanatumika, lakini mlinzi wa kwanza ambae anawatambua wale kabla ya Serikali au vyombo vya ulinzi na usalama mlinzi wa kwanza lazima awe mwananchi. Kwa hiyo kama mwananchi ameshirikishwa vizuri ataweza kutusaidia kulinda maeneo yetu ya mpakani kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilichokuwa ninaomba mimi sina maneno mengi sana kwa ajili ya ku-save muda lillilonisimamisha hapa kwenye Wizara hii ni hilo moja ya kwamba sasa tupate majibu ya uhakika ya Serikali mkwamo huu wa tangu mwaka 1984 ambao ume-consume miaka 37 leo tunaumalizaje ndani ya Bunge hili iliwananchi hawa wa Biharamulo waweze kupata haki yao na hatimaye jeshi pia liweze kuwa free kuyatumia maeneo yale kwa ajili ya kufanyia mazoezi wanajeshi. (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Ameshamalizia kuchangia.

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba niunge mkono hoja. (Makofi)