Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa nafasi hii, pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa mema yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwa Amiri Jeshi Mkuu wa kwanza Mwanamke Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, michango mingi iliyochangiwa na mimi nimeipenda sana naiunga mkono, mchango wangu ambao nataka niunge mkono kwa jitihada zote ni suala la kuhakikisha kuwa Wizara hii inapewa fedha za kutosha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba jeshi linaweza kufanya tafiti muhimu za kisayansi ambazo zinawezesha kulifanya Taifa hili liwe na nguvu zaidi.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba ulinzi uliokuwepo katika siku za nyuma ni ule ambao hasa tulikuwa tunaenda, tunajipanga zaidi kwenye mipaka yetu kuona kwamba labda adui atakuja kwa njia ya silaha ya moja kwa moja. Atakuja na SMG, atakuja labda pengine na silaha ya aina fulani, lakini vita vya sasa hivi ni vya tofauti, ni vita ambavyo hata adui yako humuoni, lakini upo naye jirani, ni vita ambayo inaweza ikapitia teknolojia au hizi tafiti za kisayansi zikaangamiza Taifa wakati nyinyi wenyewe hamjawa na taarifa za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi letu limeonesha nguvu kubwa sana katika mambo mbalimbali, mimi ningetamani kuona kwamba hata katika Hospitali hii inayotarajiwa kujengwa katika eneo la Msalato basi Jeshi liweze kupewa na sehemu ambayo itaweza kufanya tafiti kubwa za kibailojia ambazo zitaweza kushirikiana na taasisi nyingine za kimataifa na ndani ya Taifa kuweza kuleta matokeo chanya zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba pamoja na hayo kwa sababu Jeshi letu halijaanza leo, yawezekana katika baadhi ya sheria tulizonazo na sera zilizopo haziwezeshi kufanya hayo, kufanya hizi kazi za mashirikiano na taasisi nyingine ndani ya nchi na nje ya nchi. Kwa hiyo, ni vyema tuziangalie pia sheria zetu ili ziwezeshe kufanya Wizara hii kupitia taasisi zake au majeshi yake kuweza kufanya kazi hizi za kitafiti, kazi hizi za kiuwekezaji na kuwezesha tuweze kupata mafanikio makubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwanza pamoja na kwamba umetolewa ufafanuzi mkubwa, lakini niseme kwamba hawa ndugu zetu wanajeshi wanatakiwa pia kufahamu namna ambavyo sekta mbalimbali zinafanya kazi ikiwemo masuala ya kisiasa, kwa sababu wakati mwingine unakuta kinachosababisha mpaka vita ikatokea mahali ni masuala ya kiuchokozi tu, au masuala ambayo mengine yangeweza kudhibitiwa mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hawa wanapokuwa wanapata nafasi ya kushiriki katika maeneo mbalimbali ya kiuongozi inasaidia pia kurudisha mrejesho kwenye taasisi zinazohusiana na masuala ya kiulinzi ili ziweze kujipanga vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika suala la ulinzi mipakani; kwanza nianzie kuzungumzia hili suala la mpaka wa Ziwa Nyasa kwa upande wa Tanzania na ndugu zetu kule Malawi. Hili suala ni la muda mrefu, watu tunakaa tunahofu, hatujui kinachoendelea, uwekezaji unakuwa wa shida basi niombe pengine jitihada zifanyike zaidi ili suala hili la mpaka liweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati huo huo mimi nafahamu mlinzi wa kwanza katika nchi ni raia mwenyewe ni mwananchi mwenyewe, lakini sasa utakuta katika maeneo ya baadhi ya mipaka ikiwemo mpaka katika eneo la Ziwa Nyasa hali ya barabara siyo nzuri, ukitoka kule Chiwindi ukifika mpaka Lituhi uende mpaka Lipingu, Manda, Lipingu ufike mpaka Matema hali siyo nzuri, afadhali hata sisi tuna barabara ya vivumbi kidogo, lakini wenzetu unakuta wanategemea maji. Kwa hiyo ni vema ile barabara ikapewa kipaumbele na sema hayo pamoja na Wizara ya Ujenzi lakini hao Wizara hii ndiyo wadau wakuu wa kufaidika barabara itakapokuwa imeimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile eneo la Mpepo mpaka Dapori nalisemea kila siku, jamani kuna changamoto kule kubwa, hivi ninyi ndugu zetu ninyi hamshauri ninyi si mnashirikiana na hawa wenzetu wa barabara! Kwa nini hali imekuwa mbaya vile? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba katika masuala ya kuimairisha ulinzi eneo lile ni vyema lifanyiwe kazi ikiwemo daraja la Mto Ruvuma pale Mitomoni ili kuhakikishwa kwamba usalama wa maeneo yale unaimarika na unakuwa ni mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende katika suala la haki za binadamu lakini pia kutoa fursa sawa kwa wote. Kwa siku za nyuma uwe mwanajeshi au uwe polisi ukishakuwa mfupi kama mimi Engineer Manyanya hawakuchukui, lakini siku hizi hatuangalii urefu tu, hatuangalii maumbile tu, hawa ndugu zetu wenye ulemavu mbona hawapati fursa za kuingia Jeshini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatusemi waende wakapigane mstari wa mbele, lakini kichwa chake na mikono yake yawezekana kina uwezo mzuri katika masuala ya ICT, katika masuala ya kimkakati na wakafanya vizuri tu. Kwa nini sasa Serikali isiangalie kuona namna bora ya kuweza kusaidia hata kundi hilo hata kama hawatawekwa katika nafasi hiyo ya kwenda kwenye mstari wa mbele, lakini waweze kufanya kazi ambazo pia zinaweza kusaidia katika kutoa maarifa na mambo mbalimbali yanayohusiana na kuimarisha Jeshi letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naamini inawezekana, hatuwezi kusimamia tu sheria zile za zamani zinasema kwamba wewe tumekuona mkono wako umekaa hivi basi wewe huwezi kwenda. Hapana, kuna watu tena watu wenye ulemavu Mungu amewapa vipawa vikubwa sana, unaweza kukuta kwamba huyo ndio akawa master mind mzuri sana. Kwa hiyo, mimi nasema hili suala tuliangalie ili hilo kundi na lenyewe liweze kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, katika haya masuala ya JKT hawa vijana ambao wako barabarani wanaomba na wenyewe waweze kuwekewa utaratibu wa kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si jambo la heshima kuiona Tanzania bado inakuwa na watu wengi barabarani wanaombaomba. Hapana hawa vijana wanaweza wakasaidiwa, huyo anayesemekana labda hana mzazi yawezekana kweli wazazi wake wote wawili hawapo, lakini pengine kuna wale wazazi ambao hawajali hao ni Taifa.

Kwa hiyo, mimi niombe kupitia Jeshi letu tuone pia uwezekano wa kunusuru eneo kama hilo, lakini kwa Serikali kutenga fungu maalum la kusaidia Wizara hiyo kuweza kusaidia masuala kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa kweli pamoja na yote niliyozungumza mimi nalipongeza sana Jeshi letu, napongeza sana sana Wizara hii inavyojitahidi katika kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Nampongeza sana Mheshimiwa wetu Waziri Ndugu Elias kwa kazi kubwa ambayo anaifanya, kijana mpole, lakini mambo yako makubwa. Mimi nakupongeza kwa kweli, naona kwamba ndio maana hata Jeshi letu linaendelea kutulia, lakini nizidi kusisitiza kuomba kwamba hao ndugu wawezeshwe na kwa sababu wakiwezeshwa watafanya kazi kubwa zaidi ikiwemo kuwasaidia vijana waliopo vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na sio wabakie tu kufundisha migambo kule vijijini, mbali ya mgambo wafundishwe hata hizi shughuli za kujiajiri kule vijijini, isiwe tu kutembea, kukimbia, root matching, hapana; lakini pamoja na masuala ya kiuchumi wakati wanapofundishwa masuala ya mgambo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo niliyozungumza naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)