Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Charles John Mwijage

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushuru kwa kunipatia fursa ya kuchangia bajeti hii muhimu, neno muhimu linaweza kuonekana la kawaida, lakini hii ni muhimu kwa maana ni muhimu. Unapoona mtu unalala, unaamka unatembea, una amani na utilivu, una usalama ina maana kuna watu wanaumia kwa niaba yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mukhtadha huo nishukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa niaba ya Serikali ina maana Amiri Jeshi Mkuu, Mkuu wa Majeshi Makamanda na Wapiganaji wote, kazi yenu ni nzuri sana na Mwenyezi Mungu atawalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ulivyohitimisha wakati Mjumbe wa Kamati anamaliza kusoma taarifa, mimi naungana kabisa na mapendekezo yote ya Kamati hiyo ya Ulinzi ingawa mimi sio Mjumbe. Nimeisoma na nimewasikiliza nawaunga mkono. Sasa na mimi nichangie kwenye bajeti hii kwa kusisitiza mambo mahususi yanayohusu Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma yale malengo sita ya Wizara ndio utajua uzuri wa Wizara hii, nimechagua mawili katika sita. Moja ni kujenga uwezo katika tafiti mbalimbali na uhaulishaji wa teknolojia kwa matumizi ya kijeshi na kiraia, nachukua ile ya kiraia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyosema Kamati kitengo chetu cha Nyumbu kilichoasisiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kinafanya mambo makubwa, huyu naye ni ng’ombe wa maziwa sioni kwa nini Serikali tunasita kutoa pesa za kutosha kusudi Nyumbu aweze kufanya maajabu. Nimewahi kukaa nao mara nyingi na mimi nilikwenda Jeshini sio wiki mbili mwaka mzima na kwa wale wanajeshi mimi nilifundishwa na Kanali Mtono alikuwa ni commando failure yaani alikwenda kwenye kozi ya ukomando akashindwa, akaja kunifundisha mimi. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo jeshi nalijua kwa hiyo Nyumbu ukiangalia mfumo wa Nyumbu na vitu wanavyotengeneza katika hizi zama za uchumi wa viwanda kama hawa watu wakiwezeshwa, matatizo mengi yanayotusumbua yasingeweza kuwepo. Kamati imezungumza vizuri siwezi kuzungumza zaidi naiyomba na kuishauri Serikali yetu iweze kutekeleza mapendekezo ya Nyumbu.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwijage, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Mwijage, babu yangu kwamba hata humu ndani kuna wanajeshi wa akiba mmojawapo ni mimi ambaye nilikuwa kikosi cha JKT Ruvu na akina Mheshimiwa Halima Mdee, kina Silinde, kina Lusinde na wengine nilikuwa nakupa hiyo taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwijage unaipokea taarifa hiyo?

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, amesema yeye ni mjukuu sasa babu usipokubali taarifa ya mjukuu usipochemshiwa maji itakuwaje.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni moja ya malengo sita ya Wizara kutengeneza jeshi la akiba ndio hilo jeshi la akiba. Kwa hiyo ninachozungumizia mimi hoja iko kwenye Nyumbu, tuna-under utilize uwezo wa Nyumbu nizungumze mimi Nyumba naiona mbali ya kuwa ile teknolojia waliyonayo nyumbu kinapaswa kiwe chuo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ijipange, Wizara ya Elimu, mjipange na Nyumbu mnaweza kuchukuwa wahandisi wetu kutoka kwenye vyuo baada ya kumaliza, badala ya kukuaa mtaani wanatembea na mabahasha wakaenda kuwa attached Nyumbu, wale watu wamakaniko watu wa IT wakafanya practice, watawapikia, watakula, watashiba, unapotoka pale unakuwa na competence iko Nyumbu yako mambo makubwa. Niwashauri Waheshimiwa Waziri wanaohusika na sekta hizo basi na waende wakajifunze Nyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapoiacha Nyumbu nizungumzie JKT na ninaizungumza kwa upole mkubwa, naishauri Wizara naishauri Serikali tuwe na mtazamo wa JKT, mtazamo ulio mpya. Tuwapeleke vijana wetu JKT awali na mwanzo, tuwaambie wanakwenda kufanya nini. Tanzania inahitaji bidhaa nyingi mojawapo ya bidhaa iliyoko JKT unayoweza kuiendesha JKT ni wana michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kijana anaweza kukimbia, anaweza kupiga ngumi, anaweza kucheza mpira, mpeleke JKT kama nilivyoshauri mwanzoni akafundishwa hesabu na jiogorafia na Kiingereza acheze mpira asubuhi na jioni basi akisha fika kule siku za mwendo asiende JKT asiende JKT timu ya JKT ajiunge na kablu kubwa kama Simba aende Barcelona na Manchester. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo twende specifically tukiwatumia hawa watu tatizo wasiende JKT wakidhani wanataka kwenda Jeshi la Wananchi, hapana, aende kwa mfano mtu anakwenda kujifunza kilimo na nichukuwe fursa hii kuwapongeza Jeshi la Kujenga Taifa, nimeona mashamba yao ya irrigation kule Morogoro, ni mashamba yanaonesha yana tija kubwa. Basi hata tunapohangaikia kutafuta pesa JKT sehemu zake ziwe sehemu za vitengo vya biashara, sio kama hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna rafiki mmoja yuko JKT sitamtaja nilimwambia unapojenga kiwanda JKT usijenge kiwanda cha maji, ningependa kuona majeshi yetu yanawekeza kwenye viwanda vikubwa kama wangekwenda Mchuchuma na Liganga kama wanaweza waende, lakini Jeshi letu nisingependa kuona Jeshi la Wananchi eti wana kiwanda cha maji; kiwanda cha maji mtu yeyote anaweza kutengeneza. Basi vijana wako watakaokwenda jeshini watengeneza viwanda vya maji kusudi uwape jeshi libaki kwenye co-activities ambazo ni very sensitive.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini TAMISEMI niwaeleze tunazo pesa tunazowapa vijana kila mwezi kutokana na Halmashauri, unaweza kupeleke vijana kutoka kwenye Halmashauri wakaenda JKT, wakajifunza kazi mahususi, siku ya kuhitimu, siku ya graduation basi ile Halmashauri ilete vifaa ambavyo mfanyakazi huyo vijana atakwenda kutumia na impe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yaani mtu anapata mafunzo mahususi anapotoka anakwenda moja kwa moja kazini kwa mfano, sifa ziwaendee tumewaona vijana wanafanya kazi nzuri ya ujenzi, sasa siku ya kumaliza miaka mitatu au sita huyo kijana apewe vifaa na si vifaa tu, apewe na hati kwamba yeye ni mkandarasi daraja la saba au daraja la kumi aende moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwa sababu ndio wenye miradi kupitia Wizara mbalimbali Ujenzi, Afya tunaweza kuwapa makandarasi vijana ikiwepo sifa ya kwamba ulipitia JKT. Ndio maana ya lengo lenu moja kuwajengea uzalendo unatangaza tender unasema tutakupa wewe mkandarasi sifa mojawapo uwe wewe mwenye kampuni ulikwenda JKT, hapo uje uone vijana watakavyokwenda JKT wao kwa upenzi wao wakitegemewa kuandaliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuzungumzia suala moja muhimu; Mheshimiwa Waziri katika kambi ya Kaboya walikolala mashujaa waliopigana vita ya Uganda, kando yao kuna wananchi waliopisha eneo kwa ajili ya jeshi lile wanalalamika na kwa mila za kikwetu ukiwa una marehemu wanalalamika na majirani wanalalamika mambo hayawezi kutuendea vizuri. Nikuombe kabla hatujaenda kufagia makaburi Kaboya, wale wananchi ambao tulichukua ardhi yao kwa sababu nzuri za kiusalama tutafute pesa mimi na wewe tusaidiwe twende tukawafidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wale waliolala kwenye makaburi wanalalamika acha wananchi wenyewe, waliolala kwenye makaburi wanalalamika kwa sababu wenye ardhi zile wanalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, Mheshimiwa Kwandikwa, usinitupe twende tukafagie makaburi, lakini huwezi kufagia makaburi kama hujalipa fidia ya wale uliowahamisha. (Makofi)