Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Afya ambayo ni muhimu sana katika Taifa letu. Mtu yeyote asipokuwa na afya nzuri hawezi kuzalisha au kuwa na amani kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeifanya katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Kwa sababu wameweza kujenga zahanati zaidi ya 423 na vituo vya afya zaidi ya 449 na Serikali imeweza kukarabati Hospitali za Halmashauri zaidi ya 22 na Hospitali za Rufaa zaidi ya 23. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali imetumia zaidi ya shilingi bilioni 102.9 kwa ajili ya kukarabati na kujenga Hospitali za Rufaa katika Mikoa ya Geita, Katavi, Njombe, Simiyu na Mara. Kwa hivyo, ninayo sababu ya kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeifanya katika kipindi hiki cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, ninayo machache ambayo napenda kuishauri au kuisemea Serikali ili iweze kufanya marekebisho. Kwa mfano, katika Jimbo langu la Tarime Mjini tunayo hospitali moja ya Halmashauri, kituo cha afya kimoja na zahanati tatu, ukilinganisha na idadi ya watu iliyopo na jiografia ilivyo bado vituo hivi vya afya havikidhi mahitaji katika kuhakikisha kwamba watu wa Tarime wanakuwa na afya nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika Hospitali ya Bomani mara nyingi kilio kinakuwa hakuna dawa, hakuna siku mgonjwa atakwenda pale aweze kupata dawa na matibabu yaliyostahili lakini sababu kubwa ya ukosefu wa huduma hii nzuri ni kama zifuatazo. Moja, tulihitaji madaktari zaidi ya 16 katika hospitali ile lakini madaktari waliopo ni watano peke yake na unajumlisha pamoja na DMO. Sasa ukiangalia idadi ya watumishi hawa haitoshelezi, mtu anafanya kazi usiku na mchana kiasi kwamba anachoka hata kuhudumia, wagonjwa wanapata wakati mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ipo changamoto, kwa kipindi hiki ambapo barabara imekatika na mawasiliano ya barabara hayapo, unakuta hakuna zahanati za kutosha ambazo zinaweza zikahimili watu kupata huduma kwa karibu. Kutokana na hali hiyo watu wengine hufia njiani na akina mama hujifungulia njia kwa kukosa huduma ya afya kwa karibu. Kwa hivyo, nashauri tupate zahanati katika kila kata kwa mfano Kata za Kebaga, Ketare, Nyandoto, Bomani, Nyamisangura, Kenyamanyori pamoja na Sabasaba. Zahanati hizi zitaweza kutoa huduma karibu badala ya watu wote kusongamana katika Hospitali ile ya Bomani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu nyingine inayopelekea huduma kuwa siyo nzuri katika hospitali ile ni kutokana na hospitali ile kuwa kongwe, toka miaka mingi iliyopita ni hospitali ambayo Halmashauri zaidi ya tatu zimetoka pale: Hamashauri ya Rorya, Halmashauri ya Tarime Vijijini imetoka pale na Tarime Mjini. Watu wana imani sana na hospitali ile na hivyo basi wengi wanakuja kutibiwa pale, kwa hiyo, dawa zinazokuja katika hospitali ile zinachangiwa na Halmashauri zote tatu. Naomba hospitali ile ikiwezekana ipandishwe daraja iweze kuwa Hospitali ya Kanda ili at least iweze kupata dawa na madaktari wa kutosha ili watu wetu waweze kupata huduma inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika hospitali ile unakuta hakuna damu na sababu kubwa si kwamba watu wa kuchangia damu hawapo isipokuwa damu inapopatikana pale lazima ipelekwe Bugando ili iweze kupata vipimo na iweze kurejeshwa. Hata hivyo, ili majibu yaweze kurudi inachukua zaidi ya mwezi mmoja na kusababisha damu kukosekana katika hospitali yetu ya Tarime. Naomba Waziri aweze kutujengea kituo pale Mkoani ili huduma hii ya kupima damu iweze kupatikana kirahisi hatimaye kusiwepo na upungufu wa damu katika hospitali zetu. Hii si kwa Mkoa wa Mara peke yake ninaamini katika nchi nzima damu bado ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu huduma inayotolewa kwa akina mama wajawazito, wazee pamoja na watoto. Hii imekuwa ni kero na kila Mbunge anayesimama hapa anaongelea kuhusu suala hili. Mimi nilikuwa naona kama Mheshimiwa Waziri huduma hii hawezi kuitoa vizuri basi tuangalie namna nyingine ambayo tunaweza kufanya ili wazee, akina mama wajawazito na watoto waweze kupata huduma kama inavyostahilli. Wanakwenda pale wanaandikishwa lakini bado hawapati dawa na hatimaye wanarudi nyumbani bila kupata matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nizungumzie kuhusu huduma inayotolewa na watumishi wetu. Kwa mfano, katika Hospitali yetu ya Tarime hakuna wahudumu wanaotosheleza inafikia hatua mpaka wagonjwa wanafanya usafi. Mimi nikifika jimboni kila mtu ninayekutana naye analalamika kuhusu hospitali, tafadhali sana Mheshimiwa Waziri tunaomba sana uangalie hospitali yetu kwa jicho la pekee at least watu wale wapate huduma inayostahili, watu wengi wanafia pale kwa kukosa huduma inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho naependa kukizungumzia na kuishauri Serikali ni kuhusu kuongeza watumishi. Ukiangalia katika vituo vingine ambavyo vipo pembezoni bado watumishi hawatoshelezi kutoa huduma katika vituo au zahanati zile zilizo pembezoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)