Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii. Nawapongeza kwanza Mheshimiwa Waziri, Naibu na Watendaji wote kwenye Wizara hii. Kwa muda huu mchache nitachangia kwenye maeneo matatu kama muda utaniruhusu. Kwanza, ni kuhusu upatikanaji wa madawa kwenye vituo vyetu vya kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninatambua juhudi kubwa zilizofanywa na Serikali kujenga miundombinu kwenye maeneo ya kutolea huduma za afya; hospitali zimejengwa, vituo vya afya na zahanati. Kama miundominu hii itakuwepo katika mazingira yaliyo mazuri, lakini kukawa na shida ya upatikanaji wa madawa, bado haitakuwa na tija sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na shida kubwa sana ya upatikanaji wa madawa bado. Pamoja na kwamba tumeongeza bajeti ya huduma za afya hasa kwenye eneo la madawa, lakini bado kuna shida kubwa sana ya upatikanaji wa madawa kwa watu wetu kwenye vituo vya kutolea huduma za afya. Hili linachangiwa sana na deni lililoko MSD. Nikitolea mfano case study ya Ukerewe; Ukerewe ili tuwe na madawa ya kutosha kwa mwaka mzima, tunahitaji karibu shilingi milioni karibu 80, lakini mpaka mwezi Desemba mwaka 2020 ndiyo wamepata shilingi milioni 20. Kwa hiyo, utakuta kuna shida kubwa sana ya madawa kwenye Hospitali yetu ya Wilaya, kwenye zahanati na vituo vya afya.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Hospitali yetu ya Wilaya inahudumia watu mpaka wanaotoka eneo la Bunda kutoka Kisolya wanakuja kutibiwa pale. Sasa yanahitajika madawa mengi sana. Kwa hiyo, kunapokuwa na tatizo la kibajeti kunakuwa na shida sana kwa wananchi wetu. Kwa mfano, kwenye hospitali yetu ile, wanakwenda kununua madawa, wanakuta MSD kule madawa mengi hawana, wanawaelekeza kwenda kununua kwa Mshitiri. Wanapokwenda kwa mshitiri, anataka pesa cash, hospitali hawana. Matokeo yake sasa kunakuwa na shida kubwa sana ya madawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na jitihada zinazofanyika kudhibiti matumizi matumizi mabaya kwenye mnyororo huu wa madawa, lakini tuhakikishe tunapata solution ya haraka ili madawa yawe available kwenye hospitali zetu ili wananchi wetu wapate huduma hizi kwa kiwango kinachotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukizingatia tuko kwenye jitihada za kushawishi watu wetu wajiunge na Mfuko wa Afya ya Jamii, kama wanakwenda kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na hawapati madawa, inawakatisha tamaa hata kujiunga na Mifuko ya Afya. Hata hili tunaloendelea nalo la kutaka tutengeneze Sera ya Afya ya Jamii kwa watu wote, tunaweza tukapata kikwazo sana kwa sababu wananchi wanakosa imani kwamba hata wakiwa wanachama, basi zile huduma wanazozitarajia watazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, naipongeza Serikali kwa kukubali ombi letu la kupandisha Kituo cha Afya cha Bwisya kuwa Hospitali ya Wilaya na Hospitali yetu ya Wilaya ya Nansio angalau sasa kuwa Referral Hospital, ni jambo jema.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naiomba tu Serikali, zile taratibu ambazo zimebaki, ziweze kukamilishwa ili basi vituo hivi viweze kutoa huduma kwa wananchi wetu, kwa sababu dhamira ni kufanya Visiwa vya Ukerewe hasa kwa changamoto za kijiografia, iwe kama eneo linalotoa huduma kama self-contained. Huduma zote ziweze kupatikana kwa sababu ikitokea changamoto ya kiafya Ukerewe, kumpeleka mgonjwa kwenye Referral Hospital kwa mfano Sekou Toure ni changamto kubwa sana. Kwa hiyo, tukiwa na huduma zote kwenye kisiwa kile, angalau itasalimisha na itaokoa maisha ya wananchi wetu wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu sasa, pamoja na jitihada ambazo zinaendelea, najua kuna timu imepelekwa pale kufanya tathmini kuona upungufu uliopo. Naomba hasa wodi ya uzazi ya akina mama ina matatizo makubwa sana. Katika maboresho yatakayofanyika, liangaliwe kwa kipekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, jengo la mama na mtoto ambalo limejengwa kwenye miaka 1960 huko nyuma lina hali mbaya sana, nalo vile vile liangaliwe liweze kuboreshwa, lakini hata idadi ya watumishi kwenye maeneo yetu yale, bado yaangaliwe sana hasa kwenye Hospitali yetu ya Wilaya ili kuwe na staffing ya kutosha kuweza kuhudumia watu wetu na hasa kama itakuwa Referral Hospital. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hili litafanikiwa kufanya Hospitali ya Nansio ambayo ni Hospitali yetu ya Wilaya kuwa Referral Hospital, itahitaji vituo vingine vya afya kwa ajili ya ku-support eneo hili. Ndiyo maana nimekuwa ninaomba Mheshimiwa Waziri mtusaidie Kituo cha chetu cha Afya cha Nakatunguru ambacho kimejengwa mwaka 2012 chenye upungufu kidogo wa majengo na vifaa tiba, kiweze kukamilika ili kiweze ku-support hospitali yetu hii ya Wilaya. Kama itakamilika, mzigo mkubwa uwe unaelemea huku ili Hospitali yetu ya Wilaya iwe kweli ni referral hospital. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, kitakwimu ukienda hospitali ya Ocean Road kuna wagonjwa wa cancer wengi, lakini asilimia kubwa ya wagonjwa waliopo pale wanatoka Kanda ya Ziwa. Ndiyo maana mwaka 2009 Hospitali ya Bugando ikaanza kuhudumia wagonjwa wa cancer. Wakati ule ilianza na wagonjwa takribani 300, lakini hivi leo ina hudumia wagonjwa karibu 14,000 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2017 imeanza kutoa huduma ya mionzi, lakini bado ina upungufu wa miundombinu. Ina vitanda 20 pekee na kwa siku wanapokea wagonjwa karibu 200; ni wagonjwa wengi sana. Bado kuna upungufu mkubwa sana. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mkundi, kuna taarifa kutoka Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nampa taarifa mchangiaji na mchango wake mzuri, naamini mkakati wa Serikali ilikuwa ni kuhakikisha hizi mashine za mionzi zinakwenda katika hospitali zote za Kanda, kwa sababu tatizo la cancer ya shingo ya uzazi limekuwa ni kubwa sana hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi, wewe unajua Mbeya pale, kwenye Hospitali ya Mbeya, kuna tatizo na mashine haipo na iliahidiwa kupelekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nampa taarifa mchangiaji.

NAIBU SPIKA: Sasa hiyo taarifa sijaelewa kama niipokee mimi au mchangiaji. Mheshimiwa Mkundi unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, maadam ina dhamira njema, haina shida. Ninachotaka kusema, Serikali ione namna ya kuisaidia Hospitali ya Bugando. Sasa hivi wana ujenzi wa wodi ambapo itasaidia kupokea wagonjwa wengi zaidi, basi Serikali ifikirie maombi yao katika bajeti waliyonayo ya karibu shilingi bilioni tano, wodi ile iweze kukamilika. Iwasiaidie mashine za ku-backup za mionzi ili zile zilizopo zikiharibika, kuwe na mashine nyingine kwa ajili ya ku-support. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo vituo vimekamilika na hospitali zimekamilika, Serikali ipeleke vifaa tiba na wataalam viweze kufanya kazi. Kama nilivyosema, Kituo chetu cha Nakatunguru kinahitaji kuwezeshwa, majengo yaliyobaki yakamilike, vifaa viwekwe ili kiweze kutoa huduma kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo kwa mfano Ilemela, hospitali yao ya Wilaya imekamilika muda mrefu, kimebaki kuwekwa tu vifaa na watumishi kiweze kufanya kazi, iweze kuwasaidia wananchi. Naomba Serikali vilevile kama ilivyo Hospitali ya Wilaya ya Ilemela, kama ilivyo Vituo vya Afya cha Nakatunguru Ukerewe na vingine vyote nchi nzima, basi vipelekewe vifaa na wataalam viweze kuanza kutoa huduma kwa wananchi wetu ili wananchi wapate kile ambacho tunakitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa nafasi, Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)