Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. ALLY M. KISSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza rafiki yangu Dkt. Faustine Ndungulile kwa kuwa Mtanzania muasisi wa Wizara hii mpya ambapo Mheshimiwa Rais amemdhamini, amemuamini na kwa changamoto ambazo Wabunge tunazielezea katika Bunge lako Tukufu, naamini kabisa rafiki yangu Mheshimiwa Ndugulile ataweza kuitendea haki Wizara hii. Atasaidiana na timu yake Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote katika Wizara hii, tuna imani nanyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo langu la kwanza la mchango, ni kuishauri Serikali Wizara hii ya Mawasiliano Teknolojia na Habari kupitia taasisi yake ya TCRA. Kimsingi TCRA ni regulator, lakini Watanzania tunahitaji kufahamu ina regulate nini, masuala yote ambayo TCRA inadhibiti yafahamike. Kama ingelikuwa ni mpira tasnia ya kabumbu au kandanda maana yake ni kwamba TCRA ni referee na makampuni ya simu ndiyo timu wachezaji, sisi watumiaji ndiyo washangiliaji na washabiki. Tunataka tujue sisi washabiki nini TCRA ina regulate. Twende mbali zaidi ipendeze zaidi tufikie wakati kwamba sisi washangiliaji, watumiaji, tupate muda wa kupata forum ya kutoa maoni yetu kwa huyu regulator anayeitwa TCRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili gharama za simu. Huko nyuma tulikuwa tunatumia gharama za simu kwa utaratibu wa ukinunua Sh.1000 au Sh.2000 maana yake ndivyo utakavyotumia, lakini kumekuwa na utaratibu sasa wa kununua bando au vifurushi, imekuwa kana kwamba ni lazima ununue vifurushi, hivi utaratibu huu TCRA na Mheshimiwa Waziri wanasemaje, kwamba ni lazima Watanzania tulazimishwe kutumia simu kwa utaratibu wa vifurushi, usipohitaji vifurushi unataka utumie moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, bado kuna matatizo na tunahisi kwamba sisi wadau wa tasnia hii ya mawasiliano kuna kuibiwa kupitia utaratibu wa vifurushi. Kwa mfano, unakuta unajiunga kifurushi cha wiki au kifurushi cha siku cha saa 24, badala ya kutumia akiba yako kadiri ulivyoweka, muda ukifika wa saa 24 imekata, sasa hii iliyokatwa inakwenda wapi, hapa ndiyo ambapo tunamtaka regulator, TCRA asikilize maoni ya sisi wadau ambao ni watumiaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa ushauri kwa Wizara hii, nianze sasa kuelezea changamoto ambazo zipo katika Jimbo langu la Kilwa Kusini lakini pia Jimbo la mwenzangu, jirani yangu ndugu yangu, Mheshimiwa Ndulane la Kilwa Kaskazini. Katika Wilaya ya Kilwa, wilaya yenye kata 23, kata 22 hazina uhakika wa mawasiliano. Nitumie fursa hii kumkumbusha rafiki yangu Mheshimiwa Dkt Ndungulile, nimefika ofisini kwake mara kadhaa kumkumbusha kwamba Likawage ambayo ni kilometa zaidi ya 110 kutoka Makao Makuu ya Wilaya hawana mawasiliano, kitu ambacho ni tishio kwa usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tukumbuke kwamba Kata hii ya Likawage na Vijiji vyake vyote vitatu vya Likawage na Inoke na Liwiti, ni kata ambayo ipo katika eneo kubwa linazungukwa na Mbuga ya Selous. Wanapata shida ya kwenda kupiga simu mbali karibu na mpakani ukielekea Njinjo kule na usalama wa maisha yao unakuwa hatarini, tunapata shida kupata taarifa za dharura ikiwemo misiba, lakini shida kubwa ni suala la mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alinipokea vizuri ofisini kwake na kupitia sasa katika mjadala wa bajeti yake, nimkumbushe ahadi yake ya kuhakikisha kwamba Wanalikawage wanapata mnara wana uhakika wa mawasiliano. Sambamba na hilo bado zipo kata zingine ambazo mawasiliano ni shida katika Wilaya ya Kilwa ikiwemo Kata ya Nanjilinji hususan Nakiu pamoja na Kigombo, lakini pia ikiwemo Kata ya Lihimalyao hususan Kisongo na maeneo ya Mabanda kule. Pia Kata ya Kandawale, Kipatimu, Miguruwe, Mitole, Kibata, Kinjumbi, Namayuni pamoja na Chumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Wizara hii inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndungulile awatendee haki Watanzania wa Wilaya ya Kilwa kuhakikisha kwamba wanapata mawasiliano ya uhakika. Mbaya zaidi hata zile sehemu ambazo mawasiliano yanapatikana, uhakika wa 4G haupo. Kwa hiyo tunaomba kwamba minara hii sasa iongezewe nguvu ili watanzania wa Kilwa nao waishi kidigitali kama maeneo mengine ya mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)