Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. PROF. MAKAME M. MBARAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye Wizara hii ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Awali ya yote, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujaalia kukutana hapa tukiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita hasa kwenye eneo la miundombinu kwa sababu kubwa kama tunazungumzia digital economy, kama tunazungumzia maudhui, kama tunazungumzia chochote kile kwenye sekta hii ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano jambo muhimu ni miundombinu sahihi. Ndio sababu Serikali yetu iliamua kujenga miundombinu sahihi, miundombinu mahiri, miundombinu ya uhakika kwa kuhakikisha kwamba Watanzania hawa wanapata huduma safi na salama ya mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kwanza kwenye sekta hii eneo la Mkongo wa Taifa. Kama unavyofahamu na Watanzania wote wanavyoelewa kwamba Serikali yetu imewekeza kwenye Mkongo wa Taifa mabilioni ya fedha. Mpaka sasa hivi tumejenga takriban kilometa 7,450 ambazo zimeunganisha mikoa yote ya Tanzania pamoja na nchi jirani, kwa maana inaunganisha nchi yetu na nchi za nje. Tunafanya vizuri na nchi yetu sasa imekuwa kituo mahiri kwa ajili ya muunganisho wa sekta ya mawasiliano. Pia tumeona taasisi nyingi za Serikali tunatumia Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kuna eneo ambalo bado hatujafanya vizuri. Eneo hili ni eneo la elimu mtandao, matibabu mtandao, biashara mtandao, kilimo mtandao na kadhalika. Watu wengi hapa wanazungumzia kuhusu maudhui, maudhui yanapatikana hasa kama tunakwenda kwenye elimu mtandao kwa sababu tunasomesha vijana wengi, tunawapa nafasi nyingi, matokeo yake vijana hawa wanaweza kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini hatujafanya vizuri kwenye maeneo haya, kwanza, ni kwa sababu bundle yenye kasi kubwa high speed internet bandwith ipo bei juu. Pili, kumekuwa na shida ya excess network, last mail connectivity. Maeneo mengi ya mjini yanayo internet lakini ukitoka nje ya miji kuna shida, tumefika kwenye wilaya lakini bado kuna shida ya connectivity. Tatu, kunatakiwa taasisi maalum ambayo itasimamia mkongo kwa uwezo mzuri zaidi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi tunaishauri TTCL ambayo ndiyo shirika letu la mawasiliano likishiriana na Wizara iweze kutoa bandwith hasa kwa Vyuo Vikuu na hospitali kwa bei nafuu ili kuwawezesha watu hao kufanya elimu mtandao, waweze kufanya matibabu mtandao na kadhalika. Naamini tukifanya hivyo tutaweza kutumia mkongo wetu vizuri na utaleta faida kubwa zaidi kuliko ilivyo sasa hivi. Sasa hivi wakati mwingi tunatuma mkongo kwa ajili ya simu, kupeleka meseji huku na kule, kupeleka picha huku na kule lakini hatujautumia ipasavyo hasa katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ninalotaka kuchangia ni kuhusu miundombinu ya data center. Pale Kijitonyama tumejenga mfumo wa kisasa wa data center. Data center ile ni ya kisasa, nathubutu kusema kwamba katika Afrika ya Mashariki ndio data center kubwa na ndiyo yenye uwezo wa kisasa. Ina kiwango kinachoitwa tier-3 ambayo inatambulika kimataifa. Hata hivyo, bahati mbaya sana, taasisi chache hasa sekta binafsi zimejiunga na mfumo ule. Nachukua fursa hii kuiomba Wizara itumie muda mwingi kuhamasisha watu wengi waweze kujiunga na taasisi ile au data center ile. Kwa sababu watu wengi wakijiunga na data center ile tutapata fedha zaidi, tutaweza kupata hub grade, tutaweza kufanya mambo mengi na Watanzania watafaidika zaidi na mfumo ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya data ni biashara muhimu sana duniani na kila nchi inafanya biashara ya data, lakini hapa kwetu bado hatujachangamkia sana fursa ile na Serikali imewekeza shilingi nyingi karibuni, kama sikosei Dola za Kimarekani milioni 91 zimewekezwa pale kwa ajili ya kujenga data center. Kwa hiyo naomba sana Wizara, naomba sana TTCL na wadau wote waitumie fursa ile kwa maslahi mapana ya nchi yetu. Pia ile data center iko pale tu Kijitonyama lakini ipo haja ya kujenga na maeneo mengine kwa mfano hapa Dodoma na Zanzibar kwa sababu lazima tuwe na backup. Ikitokea la kutokea leo pale Kijitonyama tutapoteza data nyingi ambalo hilo litakuwa siyo jambo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa hiyo naomba wizara ifanye jambo hili na iweze kuchangamkia, waweze kujenga data center moja hapa Dodoma, nafikiri mpango huo ulikuwepo na vile vile waweze kujenga data center nyingine huko Zanzibar. Tukifanya hivyo data zitakuwa salama na nchi yetu inaweza kufanya biashara kubwa ya data. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la PKI - Public Infrastructure, hili ni jambo kubwa sana na Wizara wanalifahamu na wamejipanga, naomba waongeze kasi ya kutengeza jambo, kwa sababu mfumo huu ni muhimu sana hasa kwenye usalama wa miala tunayofanya. Kama unavyojua sasa kila mtu sasa hivi ananunua vitu kupitia kwenye mitandao, ananunua vitu kupitia kwenye simu, lakini usalama wa miamala hiyo bado ni shida. Kwa hiyo, tukianzisha mfumo huu wa PKI, naamini kwamba sasa tutajipanga vizuri na tutaweza kufanya kazi vizuri na nchi yetu itafaidika katika teknolojia hii ya habari na utangazaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo machache, sasa naomba kuunga mkono hoja na nafikiri tunaendelea vizuri. Ahsante sana. (Makofi)