Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Awali ya yote, napenda niishukuru sana Serikali kwa namna ambavyo imetekeleza miradi mingi na mikubwa kwenye Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru sana Wizara kwa ulipaji wa fidia wa kupisha Uwanja wa Ndege wa Msalato, ambapo wananchi wameanza kulipwa fidia zao. Vilevile, naishukuru sana Serikali kwa sababu wameanza maandalizi ya malipo ya fidia kwa wananchi ambao wanapisha Outer Ring Road. Nashukuru sana kwa hatua hiyo. Pia naishukuru sana Serikali kwa kuwa hivi sasa ile barabara korofi ya kuanzia Ntyuka - Mvumi kuzunguka Kikombo ya kilometa 76 muda wowote zabuni itatangazwa ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na shukrani hizi, hapa Dodoma panajengwa barabara ambayo ni Outer Ring Road, Middle Ring Road na Inner Ring Road. Kwenye Inner Ring Road, wananchi wangu wamesimamishwa kuendeleza maeneo yao kwa muda wa takribani miaka miwili hivi sasa; wananchi wa maeneo ya Nzuguni, Mbuyuni, Chidachi na Nkonze. Wananchi hawa wote wanashindwa kuyaendeleza maeneo yao kwa sababu wanaambiwa kuna mradi unakuja wa Inner Ring Road.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri, kama mradi huu haupo tayari au hautekelezwi tunaomba wananchi wale wapewe taarifa kwa sababu ni muda mrefu umepita. Katika baadhi ya maeneo zoezi la urasimishaji makazi limeanza lakini wananchi hawa wanashindwa kurasimishiwa kwa sababu ya mradi huu ambao tunautengemea na bado haujafika. Hivyo, namuomba Mheshimiwa Waziri kwenye hii Inner Ring Road atuambie kama barabara hizi zipo au hazipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakati anaweka jiwe la msingi pale SGR Ihumwa aliahidi zile kilomita kadhaa kutoka barabarani pale Ihumwa kwenda mpaka kwenye stesheni kule. Namwomba Mheshimiwa Waziri pia aliangalie hili kwa sababu ni sehemu ya ahadi ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikumbushie barabara ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri alinijibu juzi ya Ihumwa - Hombolo - Mayamaya zaidi ya kilomita 57 ambayo na yenyewe pia ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi. Naomba Serikali iangalie kwa sababu mnaweza mkashughulikia hizi Outer Ring Road na mkahisi kwamba Dodoma ina barabara nyingi sana. Outer Ring Road lengo lake kubwa ni kupunguza msongamano wa magari makubwa hapa jijini lakini siyo barabara ambayo inakwenda kuwagusa wananchi moja kwa moja. Kwa hiyo, ziko barabara ambazo zinawagusa wananchi moja kwa moja ikiwemo hii ya Hombolo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri katika mipango ya Serikali muiangalie barabara hii kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu wananchi wanapata shida kubwa sana na gharama za usafiri zimekuwa kubwa sana kutoka Hombolo kuja hapa mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia iko barabara ambayo wenzangu Mheshimiwa Dkt. Chaya na Mheshimiwa Nollo wameizungumzia; barabara ya kutoka Manyoni - Bahi inatokea Mbabala na kuikuta Outer Ring Road. Barabara hii ina mchango mkubwa sana kwa wananchi wetu wanaotokea pembezoni, ikijengwa kwa kiwango cha lami itakuwa imesaidia sana kwa sababu inakuja pia kuungana na barabara ya Outer Ring Road ili tuweze kuwarahisishia wananchi wetu usafiri na hasa kwa kuwa inagusa takribani majimbo zaidi ya mawili kwa maana ya Jimbo la Manyoni lakini vilevile Jimbo la Bahi na Jimbo la Dodoma Mjini. Ni barabara muhimu sana tunaomba Serikali iweze kuiangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa kuna changamoto wananchi wengi wakikutwa kwenye barabara ambao wanapaswa kusubiri utekelezaji wa miradi ya barabara, wenyewe wanapaswa wasubiri mpaka Serikali ikiwa tayari kujenga barabara lakini tunawatesa sana wananchi kama hawa ambao nimewasema wameacha kuendeleza maeneo yao wanasubiri mpaka Serikali ikiwa tayari kutekeleza miradi hii. Hii siyo Dodoma tu ni nchi nzima, naomba Serikali iweke utaratibu ambao hautamuumiza mwananchi wa kawaida, kama bado hatuko tayari tusiwasimamishie wananchi hawa uendelezaji wa maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)