Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, pamoja na kazi nzuri inayofanywa na wizara yetu ya Ujenzi, nichangie kwenye eneo la barabara ya Kibiti - Lindi, barabara hii haina muda mrefu lakini kwa sasa ina maeneo korofi kweli kweli niombe wizara ifanye kadri inavyoweza ili yapitie maeneo haya na kuyarekebisha mara moja. Maeneo haya Mbwemkuru, Malendego mpaka Nangulukuru kipande hiki ni kibovu kweli kweli na kinaweza kikasababisha ajali endapo hazijachukuliwa hatua za makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninzungumzie eneo la barabara za kutoka Nangulukuru kwenda Liwale, Liwale – Nachingwea, Nachingwea – Ruangwa, Ruangwa - Nangulukuru. Maeneo haya yamedumaa kwa sababu pamoja na mambo mengine ni hali ya barabara ya maeneo haya, tukijengewa barabara maeneo haya hata kiuchumi yatakwenda kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa masikitiko makubwa niendelee kusema tu kwamba maeneo haya tunazalisha korosho kwa wingi, tunazalisha ufuta kwa wingi, lakini barabara zake ni mahandaki. Niombe sana sana wizara iweke upendeleo maalumu kabisa. Mheshimiwa Mbunge wa Liwale hapa amezungumza, amezungumza jana tena kwa hisia kali kabisa, kwa kweli ipendeze baada ya Bunge hili au wakati Bunge linaendelea Mheshimiwa Waziri aende akatembelee haya maeneo akajionee mwenyewe. tunachokizungumza tunamaanisha watu wetu wanapata shida kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa unyenyekevu mkubwa nizungumzie kipande cha barabara kutoka Masasi kwenda Nachingwea. Wakati tunafunga kampeni za uchaguzi mwaka jana aliyekua Rais wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hayati alizungumza na wapiga kura wa Jimbo langu la Nachingwea kwa njia ya simu na kati ya vitu alivyowaahidi ni barabara hii ya Nachingwea kwenda Masasi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye kumbukumbu ya barabara hii upembuzi yakinifu umeshakamilika miaka mitano iliyopita, lakini mwaka 2016 ilitengewa shilingi bilioni moja kwa maana ya kishika kasima hakuna kilichoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumi na saba kumi na nane ilitengewa bilioni 3.5 hakuna kilichoendelea 2018/2019, 2019/ 2020 ikatengewa bilioni 1.3, 2020/2021 ikatengewa bilioni 1.4 mwaka huu imewekewa bilioni 1.5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Waziri atakapokuja kujibu hapa kwa kweli nitashika shilingi kama huna maelezo yatakayotoa matumaini ya lini barabara hii itajengwa, na kwenye hotuba yako huku nimeona Mheshimiwa Waziri amesema Serikali inaendelea na kutafuta pesa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii ya Masasi – Nachingwea.

Mheshimiwa Naibu Spika, imetafutwa kwa miaka mitano, upembuzi yakinifu na vitu vingine vimeshakamilika hebu tuchukuwe juhudi za makusudi kwa ajili ya watu wetu hawa. Watu hawa wanajuwa kujiletea maendeleo yao wenyewe lakini kama miundombinu ikiwa ni shida kwa kweli hii haikubaliki. Nitaishikilia shilingi hiyo Mheshimiwa Waziri mpaka mwisho ili nione unawatendea haki wananchi wa Jimbo langu la Nachingwea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nizungumzie pia changamoto nyingine ya kipande cha barabara nilichokizungumzia cha kutoka Nachingwea – Ruangwa. Tukumbuke Ruangwa yupo Mheshimiwa Waziri Mkuu anateremka Uwanja wa Ndege wa Nachingwea hii barabara ni mbovu. Naomba tufanye juhudi za makusudi ili kuwezesha hata viongozi wetu wakiwa wanateremka uwanja wa ndege waweze kutembea kwenye barabara ambazo kwa kweli watakuwa na usalama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara ya kutoka Masasi - Lindi ina matuta na mimi nafikiria hawa wakandarasi au wahandisi wetu walifikiria nini maana haya matuta ni makubwa kiasi ukiendesha speed hata kama ni 60 ukipita kwenye hilo tuta utapata ajali tu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsate sana, kengele imegonga.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)