Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu. Lakini naomba nianze kwa kuunga hoja bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, lakini niishukuru Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa kukamilisha ujenzi wa Daraja la Mto Sibiti lililogharimu shillingi bilioni 34.5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, daraja hilo liko kwenye barabara inayotoka Kolandoto – Lalago, Mwanuzi – Sibiti, Matala mpaka Junction ya Karatu. Barabara hii ni barabara ambayo jana Mheshimiwa Flatei alitaka kuirukia sarakasi, Mheshimiwa Mbunge alikuwa na haki kwa sababu barabara hii ni ahadi ya muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini, nikushukuru na niishukuru Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza daraja hili la Sibiti na barabara unganishi yenye km 25 kwa ujenzi wa lami.

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika,taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Leah Komanya kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Flatei.

T A A R I F A

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Leah, barabara hiyo haipiti kule inapita Singida kuja Haydom kwenda Mbulu kwenda Karatu, kwa hiyo siyo hiyo anayosema.

NAIBU SPIKA: Ahsante, Mheshimiwa Leah Komanya unaipokea taarifa hiyo?

MHE. LEAH J. KONANYA: Naipokea taarifa ni hiyo hiyo niliifupisha kwa ajili ya kuokoa muda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha daraja la Mto Sibiti na barabara unganishi. Barabara hii ya km 25 ni muhimu sana, nimuombe Mheshimiwa Waziri aje kuiona kutokana na changamoto ya eneo lililopo, eneo hilo ni mbuga kali sana na ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha changarawe umechukua miaka mingi sana mpaka kukamilisha, nimuombe aje aone ili ajue ni wakati gani aanze kujenga barabara hiyo kwa sababu sasa imeanza kuliwa na mvua ambayo inaweza ikapelekea hasara nyingine kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuishukuru Serikali kwa kuanza kuonyesha nia kuijenga hii barabara niliyoitaja angalau kwa kutenga bilioni 5, angalau imeonyesha nia ni zaidi ya miaka 25 hii barabara imekuwa ikiwekwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, angalau sasa shilingi bilioni 5 zimetengwa. Mimi kama Mbunge niliomba kipaumbele kipelekwe katika ujenzi wa madaraja katika mito iliyo karibu na daraja la Sibiti ambayo ni Mto Itembe, Mto Chobe, Mto Nkoma na Mto Liusa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kujengwa kwa madaraja katika Mito hii kutaleta tija katika daraja la Mto Sibiti kwa sababu daraja hili limekuwa mara nyingi likitumika tu wakati wa kiangazi wakati limechukua shilingi bilioni 34. Na matumizi ya barabara hii ni makubwa kutokana na magari ya mizigo yanayotoka Musoma, Mwanza, Simiyu kuelekea Iguguno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali imeonyesha pia katika kipande cha kutoka Mkalama mpaka Iguguno ambayo ni barabara ya kutoka Bariadi, Kisesa, Mwandoya, Mwanuzi, Sibiti mpaka Iguguno kwamba wako kwenye hatua ya kumpata Mhandisi Mshauri wa kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wanafanya hiyo niiombe TANROADS Singida, kipande cha kutoka Mkalama hadi Nduguti, Gumanga hali ni mbaya sana, hakuna changarawe inayoweka ya kutosha na kufanya magari haya kudidimia. Ninaungana na Mbunge wa Wilaya ya Mkalama ambaye alichangia jana, magari yamekuwa yakizama kutokana na barabara hazijatengenezwa vizuri kwa kiwango cha changarawe na ili hali fedha hizi zinatoka kwenye mfuko wa TANROADS ambao sisi tunaamini TANROADS ina fedha za kutosha kuliko mfuko wa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe ombi katika jimbo langu, nitoe ombi la kuipandisha hadhi barabara ya Mwanuzi- Mwabuzo. Barabara hii inatengenezwa na TARURA na kwenye kikao cha barabara cha Mkoa niliomba nikakubaliwa, lakini tuliambiwa tusubiri Serikali iidhinishe upandishaji wa hadhi. Barabara ni muhimu ambayo itaunganisha mpaka Wilaya ya Igunga ni muhimu kiuchumi kwa sababu wafanyabiashara wa Wilaya ya Meatu, Maswa, Singida wote sasa wanaelekea Igunga kwa ajili ya kupata bidhaa hiyo, hivyo na kuchochea uchumi katika Wilaya ya Meatu na Mkoa wa Simiyu kwa ujumla. (Makofi)

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ngasa.

T A A R I F A

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mchingiaji kwamba wafanyabiashara wanaotoka Meatu, Shinyanga na Simiyu pamoja na Singida, imefikia hatua wamelipa soko la Igunga jina Kariakoo ya Igunga na kila Jumatano wanakuja pale kufanya mnada na kununua bidhaa. Kwa hiyo, kama anavyoomba Mheshimiwa taarifa kuhusu barabara yake, naomba nimpe taarifa ili aweze kupewa kipaumbele na Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge narudia tena, mmesikia taarifa aliyoitoa Mheshimiwa Massay? Mmeisikia Wabunge? Maana saa nyingine tunaongea sana kwa hiyo hatusikilizi. Taarifa inayoweza kutolewa ni kama ile, sijui kama tunaelewana vizuri! Tutumie muda wetu vizuri, wabunge wengi wanataka kuchangia hapa mbele sawa jamani, nadhani hilo limeeleweka. Mheshimiwa Leah Komanya malizia mchango wako.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuiomba Serikali kwa kuonyesha nia sasa ya kujenga daraja la Mto Simiyu upande wa Mwanza ambalo linaunganisha Mkoa wa Simiyu kwa upande wa Wilaya ya Busega. Barabara hii ni muhimu pia kwa magari yanayoteka Rwanda, Mwanza na mikoa mingine kuelekea Nairobi. Lakini kumekuwa hakuna mahali pa kupishana lakini niipongeze Serikali, imeonyesha nia kwa kutafuta fedha kwa kupitia Benki ya Dunia. (Makofi)

Mheshimwa Naibu Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)