Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Miundombinu. Kwanza kabisa, nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Waziri na Manaibu wake wawili kwa uchapakazi wao mzuri wa kuhakikisha kwamba barabara zetu zinaunganika karibia Tanzania nzima. Hongereni sana kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kupoteza muda naomba niingie sasa kwenye hoja zangu za msingi. Hoja yangu ya kwanza ni kwamba pamoja na kazi nzuri ambayo Serikali inafanya kwenye miundombinu lakini kuna changamoto ya wakandarasi. Wakandarasi wanalalamika sana wanapokuwa wamefanya kazi wanacheleweshewa sana malipo yao lakini pia wakifanya kazi kabla hata hawajalipwa wanakatwa pesa zao kwenye akaunti zao na kufungiwa bila utaratibu. Kwa kweli hilo Wizara iliangalie kwa makini na ilifanyie kazi. Wakandarasi wetu ni wazalendo na ni Watanzania na wamefanya kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba barabara zetu ni nzuri pamoja na changamoto ya mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni Uwanja wa Ndege wa Mkoa wa Rukwa, Sumbawanga Mjini. Uwanja huu wa ndege umezungumziwa muda mrefu sana, zaidi ya miaka minne tunapitisha bajeti ya Uwanja wa Ndege wa Sumbawanga lakini hakuna kinachoendelea. Tunaishukuru Serikali mwaka juzi iliweza kuwalipa wananchi waliokuwa wanauzunguka uwanja ule wa zamani mdogo lakini baada ya hapo kumekuwa kimya kabisa, hakuna kinachoendelea na wakati Mkoa wa Rukwa una fursa nyingi ikiwemo na utalii wa aina mbalimbali; Kalambo Falls, mbuga za wanyama na madini ya kutosha. Pia kuna wafanyabisahara wakubwa ambao wangeweza kutumia usafiri wa ndege kuja Dar-es- Salaam na kurudi Dodoma na kwenda Sumbawanga. Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hapo atueleze Uwanja wa Ndege wa Sumbawanga Mjini utajengwa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni barabara. Kuna barabara moja ambayo ni uchumi kabisa wa Mikoa ya Rukwa, Katavi, Songwe na Mbeya. Barabara hiyo inatoka Kibaoni – Maji Moto - Muze - Iremba – Kilyamatundu - Mloo. Barabara hii nayo imezungumziwa muda mrefu sana, Serikali imekuwa ikitengeneza vipande, utakuta imetengenezwa daraja baada ya muda linaacha mto Serikali inarudi tena kutengeneza. Nachoweza kuishauri Serikali, barabara hii muarobaini wake ni kuweka lami. Barabara hii imepita kwenye Bonde la Rukwa ambapo mazao mengi yanalimwa kule. Mpunga, ufuta na mazao ya kila aina yanastawi kwenye Bonde hilo la Rukwa. Kwa hiyo, tunaiomba barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kupoteza muda niongelee tena suala la bandari. Mkoa wa Rukwa tumekuwa na bandari kama tatu lakini hazifanyi kazi yoyote. Serikali imewekeza pesa za kutosha kwenye bandari hizo lakini mpaka sasa hivi hakuna bandari hata moja inayofanya kazi. Kwa maana hiyo, naishauri Serikali iweke nguvu kwenye bandari hizi ikiwemo Bandari ya Kipili na Bandari ya Kabwe; bandari zile Serikali imeweka pesa nyingi kwa hiyo, irudi kwenda kuzifanyia kazi ziweze kufanya kazi na kuingiza pato la Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maneno haya mafupi, naomba Serikali iwakumbuke wakandarasi kwa kuwalipa pesa zao kwa wakati. Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)