Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii adhimu. Kwanza kabla sijazungumza naomba niunge mkono hoja ili nisije nikasahau. Siungi tu mkono hoja, ninayo sababu. Sababu ya msingi kabisa ni kwamba ile barabara ambayo nilikuwa ninasema, leo ni mara ya nne naizungumzia hapa Bungeni. Barabara inayotokea Magu – Bukwimba – Ngudu mpaka Nhungumalwa yenye urefu wa kilometa 71 sasa nimeona kwenye Vote namba 4162 imepangiwa kujengwa kilometa 10. Hiyo ndiyo sababu nimeunga mkono kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu tunaheshimiana sana, wewe ni kama kaka yangu na watu wa Kwimba wanakushukuru kwa hili. Lakini, wanao ushauri kwako. Katika Vote hii namba 4162 ambayo tumehangaika mimi na wewe mpaka naiona hapa umetupangia bilioni 1.5 nadhani mimi na wewe ni mashahidi kwamba bilioni 1.5 haiwezi kutosha kuanza kutujengea kilometa 10 kwenye hizi kilometa 71. Sisi tunataka kwa kweli tumeshaomba sana, sasa sasahivi tunataka mtujengee, msikomee kutuandikia hapa kwamba mnajenga kilometa na mmetenga bilioni 1.5 halafu ujenzi usitokee katika Mwaka huu wa Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo wazungumzaji wa mwanzo wamesema, ni lazima ifike wakati sasa vipaumbele hivi vitolewe kwa maeneo yote. Tumekuwa tukiona maeneo ya mjini ambayo yanaonekana kwa urahisi, ikitokea foleni kidogo tu naona zinajengwa ring roads, fly overs, lakini sisi watu wa vijijini inawezekana foleni zetu Mheshimiwa Waziti hauzioni, foleni zetu ni za mazao yanayoharibikia shambani kwa kushindwa kusafirishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, foleni zetu sisi ni watu wanaolala njiani siku mbili kwa barabara kuharibika. Hamyaoni haya, lakini nchi hii ili uchumi uende vizuri na watu waache kuhamia mijini wabaki vijijini wazalishe ni lazima na vijijini huduma ziende. Barabara za vijijini zipitike, kule ndiko tunakolima mazao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo la Sumve mazao yakilimwa mfano kwenye Kata kama ya Mwandu, ukilima mazao wakati wa mvua ni mpaka usubiri kiangazi uje uyasafirishe na tela ya ng’ombe. Mkokoteni ule ndiyo unasafirisha. Sasa, na sisi tunayo haki kama watu wengine wanaobanduliwa lami na kuwekewa lami mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano natoa barabara ambayo haipitiki kabisa iko kichwani tu lakini haipitiki. Yaani ukitokea Goroma unaenda Shushi, unaenda Mwakaluto, uende mpaka Ngudu kupitia Ilumba, ile barabara ni ya kichwani, haipitiki wakati wa mvua lakini kule ndiko tunakozalisha mazao mengi ya mpunga. Ukitaka kwenda kutokea kwenye mnada mkubwa kabisa kwenye Wilaya ya Kwimba Wabungurwa, unaenda Ng’undya, barabara ile haipitiki lakini kule ndiko mazao yanazalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa waziri, tufike wakati uangalie hii barabara ya kwetu ya msingi kabisa ambayo inatokea Magu kwenda Ngudu mpaka Nhungumalwa kupitia stesheni ya Bukwimba ni lazima sasa muijenge kwa kiwango cha lami. Maombi tumeomba sana. Tunaomba sasa hizi kilometa 10 zilizoandikwa kwenye bajeti tuzione. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini iko barabara ambayo ndugu yangu Mheshimiwa Flatei Massay alitaka kupiga sarakasi hapa. Barabara hii inaanzia, yeye aliishia Maswa lakini ukitoka Maswa inakwenda mpaka Malya. Kutokea Malya inaenda mpaka Nyambiti. Kutokea Nyambiti inaenda mpaka Fulo, barabara hii imeahidiwa kwenye ukurasa wa 77 wa Ilani ya CCM kwamba itafanyiwa upembuzi yakinifu na kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii itamsaidia mtu anayetoka Mwanza akapita Jimbo la Sumve akaenda mpaka Maswa – Meatu, akaenda mpaka Hydom Mbulu akasafirisha mazao yake na inarahisisha sana usafiri. Barabara hii ni ya kimkakati kwenye kuinua utalii wa Serengeti. Sasa barabara hii imekuwa ikiandikwa na kuachwa na kwenye bajeti sijaona ule upembuzi yakinifu niliuona kwenye Ilani kwenye bajeti sijaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa waziri, naomba sasa Wizara iipe kipaumbele barabara hii. Ijengwe kwa kiwango cha lami ili na sisi tupate kama wanavyopata wengine. Nakushukuru sana. (Makofi)