Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, bajeti yake ni nzuri na naamini hii ndio bajeti ya kwanza kuwasilisha. Ninachoomba kwa Mheshimiwa Waziri, Wabunge wamekuwa wakisema kumekuwepo na upendeleo na ukweli nakiri, ukiangalia huu upendeleo umekuwepo kwa sababu kuna maeneo mengine unaona ndio yanayotajwa kila mara. Sasa tumwombe Waziri kwa sababu ni bajeti yake ya kwanza ajitahidi sana huu upendeleo usiwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumizie suala la barabara, barabara ni uchumi na ndio kila kitu. Niombe nizungumzie barabara ambazo ni za kiuchumi; niongelee barabara ya Murushaka kwenda mpaka Murongo, hii ni barabara muhimu sana kiuchumi. Kwenye Nchi ya Tanzania hakuna wilaya ambayo inalima kahawa nyingi kama Wilaya ya Kyerwa, lakini ukija kuangalia hizi barabara ndizo barabara ambazo zimeachwa kwa muda mrefu na imekuwa ni ahadi ya muda mrefu lakini hazitengenezwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine nimekuwa nikishangaa, wanasema Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa maskini. Lakini jambo ambalo linasikitisha ni kwamba hii mikoa ambayo imenyimwa miundombinu lazima itaendelea kuwa mikoa maskini lakini kwa upande mwingine ninajiuliza, Serikali hili hailioni?

Mheshimiwa Naibu Spika, hii mikoa ambayo ina uzalishaji mkubwa wa kahawa, hii mikoa ambayo ndiyo ina uzalishaji mkubwa wa ndizi, hata ukienda Ulaya watakwambia ndizi ya Bukoba. Lakini nenda uangalie barabara zake zilivyo! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo niombe, nimeona umeweka pesa kidogo, nimesema hiki ni kama kishika uchumba, hii pesa bilioni tatu ambazo umeweka, Biblia inasema kila mtu aseme kweli na Jirani yake, na ndiyo yenu iwe ndiyo na hapana iwe hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu kwako Mheshimiwa Waziri; hii bilioni tatu uliyoitenga barabara hii unanihakikishia utaanza kuijenga! Na ni ahadi ambayo Mheshimiwa Rais, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, aliahidi na akatoa maelekezo kwamba ijengwe kilometa 50 kwa kuanzia. Sasa nimeona mmeweka bilioni tatu, kwa kweli niseme hili jambo sijaridhika nalo lakini wewe nikuombe wakati unajumuisha hapa utuambie hii barabara unaijenga lini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mgakorongo kwenda mpaka Mrongo. Hii ni barabara ambayo ni muhimu, inaunganisha Nchi jirani ya Uganda. Ukiangalia upande wa wenzetu ni jambo ambalo linasikitisha, kule kwa wenzetu ni kama Ulaya lakini huku kwetu ni kama uchochoroni. Sasa hizi barabara ambazo zinaunganisha nchi na nchi lazima tuzipe kipaumbele. Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo nikuombe sana barabara hizi ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, ni jambo ambalo linasikitisha unapita kwenye barabara unaona bado ni nzuri lakini wanakwambia tunaondoa hii lami kwa sababu muda wake wa kuishi umekwisha. Kule kwetu tunatamani hata hiyo mliyoiondoa mngetupa sisi, lakini hatuipati. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri hili uliangalie sana na huu upendeleo uondoke kabisa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshalia Mheshimiwa.

MHE. INNOCENT S. BILAKATWE: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilisemeeā€¦

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ni Mwanakamati wa Miundombinuā€¦

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)