Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kwake kwa kura za kishindo kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi walivyouwezesha Mkoa wetu wa Dar es Salaam. Usiposhukuru kwa kidogo basi hata ukipata kikubwa huwezi kushukuru, ni lazima niipongeze na kuishukuru Serikali kwa yale yaliyofanyika katika Mkoa wetu wa Dar es Salaam. Kwanza kupata Daraja la Kigamboni; Daraja la Mfugale TAZARA; Interchange Ubungo ya Kijazi; na ujenzi wa Daraja la Selander ambao umeanza na unaendelea vizuri ila nitaiomba Serikali waharakishe katika kulimaliza daraja hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ujenzi wa barabara ya Bagamoyo. Barabara hii imejengwa vizuri lakini ina changamoto kubwa sana. Changamoto yake kubwa ni kwamba mvua inaponyesha inajaa maji katika maeneo yote. Hatuelewi hivi upembuzi yakinifu uliofanyika katika eneo lile hawakuliona hilo? Barabara ni nzuri na tunatarajia kweli itafungua uchumi katika maeneo hayo lakini ina changamoto ya kujaa maji. Niiombe Serikali wakaangalie hiyo barabara ina matatizo gani mpaka inajaa maji tena inajaa kwa kupitiliza kama bahari, ni nini kimetokea pale? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niipongeze Serikali kwa ujenzi wa daraja au interchange nyingine ya Uhasibu Chang’ombe na pale VETA. Miradi hiyo yote yote inaendelea na kandarasi wako site, naipongeza sana Serikali kwa kutufanyia mambo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee sasa barabara za Ubungo, tuna wilaya mbili; Wilaya ya Ubungo na Wilaya ya Kigamboni ni mpya hazina mitandao mikubwa ya barabara. Kwa hiyo, naiomba Serikali izingatie kwamba wilaya hizi ni mpya na tumeweka makao makuu ya wilaya na halmashauri lakini hayafikiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije katika barabara za Ubungo. Tuna wilaya mbili; Wilaya ya Ubungo na Wilaya ya Kigamboni ni wilaya mpya, hazina mitandao mikubwa ya barabara. Kwa hiyo, naiomba Serikali izingatie kwamba Wilaya hizi ni mpya na tumeweka Makao Makuu ya Wilaya na Halmashauri, lakini Makao Makuu ya Wilaya na Halmashauri hizo hayafikiki. Kwa mfano, katika Wilaya ya Ubungo barabara ya Makabe kupitia Msakuzi hadi Mpiji, barabara hii ni muhimu sana katika kuwezesha wananchi wa maeneo haya kufika katika Ofisi zao za Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna barabara kubwa ya Kibwamba - Kibwegere mpaka Mpiji; barabara hii ni kubwa na imetupa shida sana katika kampeni zetu. Naiomba Serikali ianze ujenzi wa barabara hii angalau kwa kilometa moja, wananchi wa Kibamba waone kwamba angalau Serikali yao inawajali. Pia niombe barabara ya Kimara mwisho kwenda Segerea kupitia Bonyokwa, barabara hii ni muhimu ambayo inaunganisha wilaya mbili; Jiji la Ilala na Halmashauri ya Ubungo. Naiomba sana Serikali waiangalie barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije katika Jimbo la Kigamboni. Jimbo hili ni mtihani, hakuna barabara. Barabara ya lami ambayo ipo kuanzia Mji Mwema kwenda Pemba Mnazi, bado haijafikia kilometa hiyo, inaishia Somangira. Pia barabara hii inakubwa na changamoto kubwa ya kuharibika haribika. Mara tu inaanza kujengwa ni viraka viraka, sasa hii hali inakuwaje? Naiomba sana Serikali, kama wanajenga, basi wajenge barabara imara kulingana na uchumi wa eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ile mwanzoni Mji wa Kigamboni ulikuwa haujajengeka, lakini sasa Kigamboni imejengeka ina viwanda, ina magari makubwa. Kwa hiyo, wakijenga wasiweke lami ya mparazo, wahakikishe wanaweka uimara wa sawa sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ambayo tunaiomba toka mimi nimeanza kuwa Mbunge humu ndani mpaka leo hii, barabara ya kutoka Kibada kwenda Kisarawe II, kwenda Pemba Mnazi kupitia Kimbiji; barabara hii jamani tumeiomba mimi toka naanza Ubunge kila nikisimama naomba barabara hii. Naomba Serikali sasa waianzishe. Hii barabara ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Marehemu kwamba sasa Mji wa Kigamboni unaenda kufunguliwa na barabara ikiwepo barabara hiyo. Naomba sana Serikali waiangalie.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda umeisha Mheshimiwa.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote naipongeza sana Serikali kwa yale waliyoyafanya.