Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii ya kuchangia katika wizara hii, kwanza kabisa nianze kwa kuipongeza wizara hii na watendaji wake wote kwa hatua hii ya utendaji ambayo imefikia lakini pili niungane na Mheshimiwa Eshi kukipongeza Chama changu Cha Mapinduzi kwa ushindi mkubwa kilichopata kule mkoa ni Kigoma katika jimbo la Mwihambwe na Bwihigwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto ya ajira tuliyonayo vijana katika nchi hii, sehemu ya kandarasi ni moja ya sehemu ambazo vijana wengi wamejikita katika kutatua changamoto hii ya ajira. Lakini bado pamoja na juhudi hii wanayoifanya kujiingiza katika sehemu hii wanachangamoto nyingi na changamoto kuu ambayo tunakutana nayo ni ukosefu wa mitaji na ujuzi wa kutosha kujiingiza katika kazi hizi za ukandarasi hasa ukandarasi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inanifanya nijiulize ni lini hasa au Serikali inadhani ni lini hasa tutaendelea kutoa asilimia zaidi ya 70 ya kazi zote ambazo zinazofanyika katika nchi hii kwenda katika makampuni ya kigeni ili hali asilimia kumi tu ya makampuni yaliyosajiliwa ndio ya kigeni hii ni aibu sana. Nadhani ni wakati sasa Serikali ijihoji kwamba tuna mkakati gani wa miaka 2, 3, 4, 5, 10 au hata 50 kwa kuhakikisha kwamba na sisi itafika wakati wakandarasi wa kitanzania watafanya kazi zetu za hapa ndani kwa asilimia 70 na wakandarasi wa nje wafanye kwa asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ilani yetu ya uchaguzi tuliyotumia kuomba kura zaidi ya asilimia 90 ya Wabunge tulioko katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 72 ni kushirikisha kikamilifu vikundi vya wanakijiiji na wananchi pamoja na makandarasi wadogo katika kazi za matengenezo madogo ya barabara kama vile kufyeka nyasi kuzibua mifereji mitaro ya barabara na kufanya usafi wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, “pili, kuendelea kuwajengea uwezo wakandarasi wazalengo ikiwemo kuwapatia kazi nyingi zaidi za fedha za mifuko ya barabara na kuwawezesha kupata mikopo ili kushiriki kikamilifu kwenye kazi kubwa za ujenzi wa barabara, madaraja na majengo.” Maana yake tuliwaahidi vijana, hasa wakandarasi, kwamba kazi yetu ndani ya miaka hii mitano itakuwa ni kuhakikisha tunawajengea uwezo wa kushiriki katika kandarasi, hasa kandarasi kubwa, lakini pia kuwasaidia ili waweze kukopesheka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika changamoto hii ya mitaji, kwa kiasi kikubwa imechangiwa na Serikali yenyewe. Tunatambua kwamba kazi hizi ni kazi ambazo zinahitaji mitaji mikubwa na labda wengi wetu hatuna, lakini Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha inatubeba sisi vijana na kutuwezesha hivyo hivyo kushiriki katika kazi hizi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi yao wamejitahidi, wametuafuta hela huku na huku ikiwemo kukopa katika benki za kibiashara kuingia katika kazi hizi, lakini shida inakuja kwenye vipaumbele vya kulipwa. Kwa vile wageni katika kampuni zao wanakuwa wana-raise invoice kila baada ya mwezi na kudai interest katika invoice zile zisipolipwa kwa muda, Serikali yetu inawalipa wao kama kipaumbele kuliko kuwalipa wazawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ndiyo imekuwa changamoto zaidi ya kuua mitaji ya vijana hawa. Huyu mtu kakopa kwenye benki ya kibiashara, anatajiwa riba kila anavyozidi kuchelewesha malipo; na imefikia hatua mikataba wanayopewa Wakandarasi wetu wa ndani haiaminiki tena kwenye benki zetu na taasisi za fedha. Mtu hawezi kupeleka mkataba ule akapewa pesa ya mkopo ili aje afanyie kazi. Kwa nini? Kwa sababu Serikali haiwalipi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta mtu hana hata pesa ya kula, lakini anakwambia anadai Serikalini shilingi milioni 500. Ni kitu cha aibu sana. Wakati makampuni ya nje tunayalipa kwa wakati, wazawa tunawaacha pembeni, inatia mashaka kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili suala la kuhakikisha kwamba tunawashirikisha…

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Engineer. Mwanaisha Ulenge.

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Ng’wasi kwamba anachosema ni kitu sahihi. Siyo tu kwamba Wakandarasi hawa wazawa wa ndani wanachelewa kulipwa, lakini pia Wakandarasi wazawa wa ndani hawana jeuri ya kumwomba client interest. Ile 14.7 billion aliyoisema CAG, ile ni ya Wakandarasi wa nje. Wakandarasi wazawa wanaogopa kudai hata interest kwa sababu wanaogopa kukosa kazi kesho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ng’wasi Kamani, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo. Naomba niendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ambayo inapatikana kwenye kushirikisha hivi vikundi vidogo vidogo vya wananchi kwenye kazi hizi, hasa kazi ndogo ndogo ni kwamba, kwanza hakuna mikataba inayoeleweka wanayopewa watu hawa kabla ya kupewa kazi hizi na wengi wanaishia kukimbiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongea na baadhi ya Wabunge wa Majimbo, pesa nyingi wanaishia kulipwa wao kwa sababu wale Wakandarasi wanawapa kazi hizi ndogo ndogo, wanaishia kuwakimbia. Kwa hiyo, nashauri Serikali iangalie utaratibu wa kuweza kuvilinda vikundi hivi vidogo vidogo vinapokuwa vinapewa kazi na wakandarasi wakubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye bidding process; tunatambua kwamba tenda hizi zinatolewa kwa uwazi, watu wanakuwa na uhuru wa ku-bid freely, lakini tukiangalia Wakandarasi wetu wa ndani na wa nje, wa kwetu wako kwenye disadvantage kubwa kuliko wa nje. Kwa sababu wa nje kwanza kabisa wanapewa support kubwa sana na Serikali zao, kitu ambacho hakipo katika kandarasi zetu za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili, watu hawa wana- bid kwa bei ya chini wakiwa wameshajua kwamba upungufu wa ulipaji uliopo kwenye mifumo yetu ikoje na wanategemea faida wataitengeneza kwenye interest, kitu ambacho Mtanzania hana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiri ni wakati Serikali iangalie namna gani inafanya juhudi ya makusudi kutekeleza yale tuliyoahidi kwenye ilani yetu kwa kuwapa support, kuwawezesha Wakandarasi wa ndani, kuhakikisha wanawapa kipaumbele kwenye malipo ili waweze kukua na mwisho wa siku basi tuone asilimia za Wakandarasi wanaofanya kazi zetu za ndani ni watu wetu wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, tumeahidi kwenye ilani kwamba tutazidi kuwawezesha kuwapa kazi nyingi zaidi. Hapa kwenye hili, naomba Serikali kuangalia kwa umakini sana tunavyokwenda na hili suala. Sekta binafsi ni ya msingi sana kwenye maendeleo ya Taifa lolote lile, lakini sasa baada ya kuwa kandarasi nyingi za ndani zinasumbua kwenye ufanyaji wa kazi ikiwa ni pamoja na kazi kuishia njiani kwa sababu hawana pesa au wamecheleweshewa pesa, Serikali sasa ime-resort kwenye kutumia taasisi zake binafsi kufanya kazi hizi. Hilo ni jambo jema, kwa sababu najua Serikali haicheleweshi malipo kwenye taasisi zake zenyewe, lakini hii inakwenda kuua wakandarasi binafsi, inaua sekta binafsi ya wakandarasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, badala ya kuwanyang’anya kazi na kuzipa kazi taasisi za Serikali kama TBA, SUMA JKT, basi tuangalie namna gani ya kuwasaidia kuondoa changamoto walizonazo, ili basi tuendelee kuwakuza na sekta binafsi ikue zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kuna huu mfuko wa kudhamini Wakandarasi wadogo ambao ndiyo Serikali iliuanzisha kwa ajili ya kuwakomboa kwenye suala zima la mtaji, lakini Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mfuko huu una shilingi bilioni 3.9 pekee mpaka sasa tangu uanzishwe na Wakandarasi walio ndani yake ni 1,167. Haitoshi kabisa kuwapa mtaji Wakandarasi hawa kufanya hizo kazi. Kwa hiyo, pia tunaomba Serikali iangalie katika bajeti hii namna gani inaongeza pesa katika mfuko huu ili Wakandarasi wa ndani wengi zaidi wapate kunufaika nao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwenye hizi kazi; tunashukuru Serikali imefanya kazi nzuri ya kuhakikisha wazawa wanaajiriwa zaidi kwenye kazi hizi za ukandarasi, lakini basi tunaomba iangalie namna gani wahusika wa eneo husika waweze kuwa wanufaika wa kwanza wa zile kazi zinazofanyika kwenye maeneo yao. Kwa mfano, tuna reli ambayo sasa hivi inatakiwa kujengwa kutoka Mwanza kwenda Isaka. Basi watu wa Mwanza na wa kanda ile wawe wanufaika wa kwanza wa tenda na kazi zinazopatikana kutoka katika reli ile, sambamba na maeneo mengine yote. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na mengi ya kusema, nitayachangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho wa siku, naunga mkono hoja. (Makofi)