Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe pamoja na Bunge lako Tukufu kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia na kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizotolewa wakati wa uwasilishaji wa bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee napenda kumshukuru Waziri wangu wa Maji Mheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso, Mbunge kwa kuwasilisha kwa umahiri hoja ya Wizara yetu ya Maji kuhusu Mpango wa Bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Maji imechangiwa na Wabunge wengi, tunashukuru sana Ni wazi kuwa muda niliopewa kikanuni hautanitosha kujibu hoja zote kwa ufasaha. Hivyo, katika muda huo mfupi, kwa kuzingatia wingi wa hoja, naomba nijikite kwenye baadhi ya hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mkoa wa Mtwara, napenda kusema kwamba Waheshimiwa Wabunge wote maelezo yote waliyoyatoa kutokana na matatizo ya maji katika Mkoa wa Mtwara, kwa uchache nichukue matamshi ya Mheshimiwa Tunza Malapo na Mheshimiwa Hokororo; waliongea kwa hisia kali sana kuhusiana na akina mama wa Mtwara kuchota maji ambayo wanasema ni maji ya kuokota. Wamekuwa wakitamka hivyo kwa sababu ni maji ambayo walikuwa wakiyatega nyakati za mvua na kuingia kwenye mashimo ambayo wanakuwa wameyaandaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa kama mama, suala hili limeniingia na kujisikia vibaya. Nitawajibika kwa nafasi yangu kuhakikisha tunaenda kutekeleza mikakati ya Wizara ambayo tumejiwekea hasa kwa kutumia Mto Ruvuma. Chanzo hiki cha Mto Ruvuma naamini kitakuwa ni suluhu ya matatizo ya maji Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia mradi wa maji Ziwa Victoria kwa Mkoa wa Simiyu. Mkoa huu upo katika hatua za mwisho kupata huu mradi wa maji na tayari tuko kwenye hatua za kuweza kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya kazi ya usimamizi. Mara baada ya kupata Mhandisi Mshauri, kazi ya kumpata mkandarasi wa ujenzi pia itafanyika. Lengo ni kuona kwamba ujenzi wa mradi huu unakwenda kuanza mara moja. Tutafanya hivi kwa kuhakikisha tunasambaza maji maeneo yote ambayo bomba kuu litapita; kilomita 12 kulia na kilomita 12 kushoto kama sera inavyotutaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mkoa wa Songwe, napenda kuwapongeza Wabunge wote; Mheshimiwa George Mwenisongole, Mheshimiwa Shonza, Mheshimiwa Hasunga, Mheshimiwa Condester na Mheshimiwa Neema. Wote wamechangia kwa uchungu, namna ambavyo maji yamekuwa ni tatizo. Kwa Mkoa wa Songwe tuna mradi mkubwa wa chanzo cha maji cha Ileje; na yenyewe tunakwenda kushughulikia mwaka ujao wa fedha. Baada ya kushughulika na chanzo hiki cha Ileje, tunaamini tunakwenda kutatua tatizo la maji Mkoa wa Songwe katika Majimbo karibia yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuhusiana na kufikisha maji katika taasisi zetu za Serikali kama vile mashule ama mahospitali na vituo vya afya, tayari Wizara ipo kwenye mchakato wa kuona tunafanya ushirikiano mzuri pamoja na Wizara ya Elimu na Wizara ya Afya ili kuhakikisha shule zetu zinapata maji na watoto wanapata maji katika mazingira rafiki. Lengo ni kuona tunakwenda kuondoa changamoto ya mimba za utotoni na vile vile kuhakikisha watoto nao wanafikia ndoto zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili tayari katika utekelezaji nimeshalifanya katika ziara zangu. Nilishakwenda Biharamulo na nikahakikisha nimeacha maagizo pale ya shule ya sekondari kupata maji; Singida vilevile na pia katika Mkoa wa Mbeya nimetoa maagizo katika Sekondari ya Lyoto na yenyewe iweze kupatiwa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekuwa nikiongea mara nyingi, kwa sasa hivi Wizara ya Maji tuko katika mageuzi makubwa. Malalamiko haya ya Waheshimiwa Wabunge tunayasikia na sisi tukiwa kama sehemu ya jamii, tunayafahamu. Tukwenda kutekeleza miradi yote ambayo imekuwa ikisuasua kwa muda mrefu na tutahakikisha inakwenda kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote ambayo imekuwa ikiwasumbua wananchi katika maeneo mbalimbali kwa kutokukamilika, sasa hivi RUWASA imechukua nafasi. RUWASA imekuwa ni changa, bado tu ina mwaka mmoja lakini wameshafanya ufumbuzi wa miradi mbalimbali. Kwa hiyo, tutaendelea kutumia pia wanafunzi wetu ambao tunawapata kwenye Chuo chetu cha Maji na vile vile watumishi ambao wapo ndani, tayari na wao wameendelea kuchukua kasi ya Waziri wetu Mheshimiwa Jumaa Aweso, kwa sababu yeye wakati wote anahitaji kuona matokeo ya haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi watendaji wameshabadilika, wameshaachana na kufanya kazi kwa mazoea na sasa hivi wanafanya kazi vizuri. Wakurugenzi, Mameneja wa Mikoa na Wilaya tunawashukuru sana kwa sababu maagizo tunayowaachia tukiwa katika ziara zetu, yamekuwa yakifanyiwa kazi kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mikakati ambayo tumejiwekea kama Wizara ya kuhakikisha maeneo ya vijijini ambako maji hayajawahi kutoka bombani, sasa ndiyo wakati wa maji kutoka bombani. Tunataka tuhakikishe akina mama wanaachana na kazi ngumu ya kubeba maji vichwani, tunakwenda kumtua ndoo mwanamama kichwani. Hapa nina kila sababu ya kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu mpendwa mama Samia Suluhu Hassan, katika hotuba yake ya matumaini makubwa kwa Wizara ya Maji alipokuwa akihutubia Bunge lako Tukufu aliweza kutuhakikishia kwamba atakwenda kutuongezea fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukishapata fedha, ni usimamizi; sisi tuko tayari tutakesha, tutafanya kazi usiku na mchana. Lengo ni kuona kwamba tunahakikisha akina mama wanapata maji kwa umbali ambao ni rahisi kufikika na wanaachana na shughuli za kubeba ndoo vichwani na kupoteza muda mwingi. Tunafahamu kwamba ndoa nyingi zimekuwa zikivunjika kwa akina mama hawa kukesha huko kwenye visima, vilevile tunafahamu kuna akina mama waliopata hata ulemavu kwa sababu ya kupata vipigo vikali kutoka kwa waume zao. Sisi kama Wizara tumesema kwamba suluhu sasa ya akina mama kuondokana na dhoruba hizi zote inakwenda kupatikana mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mkoa wa Mbeya kuna mradi mkubwa wa kimkakati wa Kiwira. Huu utasambaza maji katika maeneo yote ya Jiji la Mbeya, maeneo ya Chunya kwa badaye, maeneo ya Rungwe Mbeya Vijijini na maeneo ya Ileje pia yatajikuta yananufaika na mradi huu mkubwa. Huu mradi tutausimamia kwa karibu na tutaona kwamba kuanzia mwaka ujao wa fedha tumeshautengea fedha ya kutosha na tutakuwa tunautengea mara kwa mara. Lengo ni kuona kwamba unakwenda kukamilika ndani ya muda ambao unahitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwa Mkoa wa Mbeya kwa mji wa Tukuyu pale mjini, tayari tumeendelea kupeleka fedha. Hivi karibuni tumepeleka shilingi milioni 500. Lengo ni kuona kwamba tunaboresha maji katika Mji wa Tukuyu, lakini vilevile kusimamia fedha ambazo tunazipeleka kule wilayani na mikoani ili ziweze kufanya kazi na tutasimamia kuhakikisha thamani ya pesa inakwenda kuonekana katika utekelezaji wa miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mbeya pale mjini tumepeleka Ilunga Project ambayo itasaidia maeneo ya Iwambi mpaka Mbalizi. Kwa Chunya tutaangalia mradi wa Matwiga ambao sasa umekuwa ni wa muda mrefu sana toka mwaka 2012, lakini toka baada ya RUWASA kuundwa mradi ule sasa unaelekea mwishoni, unakwenda kukamilika na vijiji 16 vinakwenda kunufaika. Yote haya ni katika kuona kwamba mageuzi ndani ya Wizara ya Maji yanakwenda kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuongea haya yote, naunga mkono hoja. (Makofi)