Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru sana kwa nafasi hii. Kabla sijaongea sana niseme tu naunga mkono hoja. Pia nimpongeze ndugu yangu Waziri wa Maji, Mheshimiwa Aweso na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya kwenye sekta ya maji. Wanafanya kazi nzuri ya heshima na sisi hatuwezi kuwalipa kwa maneno yetu haya lakini Mwenyezi Mungu atawalipa vile wanavyostahili. Naomba waendelee kuchapa kazi na Mungu na Watanzania wanawaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa Sumve wanalo jambo lao ambalo wameniomba nije nimwambie Mheshimiwa Waziri kuhusu mambo ya maji. Katika Jimbo la Sumve lililoko kwenye Wilaya ya Kwimba nadhani katika Mkoa wa Mwanza ambao ukilitaja Ziwa Victoria unaongelea Mkoa wa Mwanza kwa kiasi kikubwa ni jimbo pekee ambalo halijui utamu wa maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria. Mheshimiwa Naibu Waziri nikiangalia katika bajeti zilizopita kila mara mradi nafikiri namba 3403 ambao unahusisha kupeleka maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria katika Miji ya Sumve, Malya pamoja na Malampaka iliyoko kwenye Jimbo la Maswa Magharibi kwa Mheshimiwa Mashimba umekuwa unatajwa kila bajeti, unatengewa hii shilingi milioni 600 lakini haufanyiki. Mpaka umekutwa na miradi mingine, naanza kuona Busega ambaye ni mjukuu wa Kwimba tumemzaa sisi anapangiwa mabilioni ya fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Simiyu na Wilaya ya Kwimba hasa Jimbo la Sumve kijiografia, hali ya hewa inafanana. Mradi huu wa Kuokoa Mazingira wa Simiyu, unapokwenda Simiyu unaiacha Sumve inakuwa sio sawa, watu wa Sumve tuna matatizo makubwa ya maji. Tunaomba mradi huu katika bajeti hii muweke fedha ambayo watu wa Sumve na sisi tutajiona ni sehemu ya Watanzania kwa sababu tupo kwenye Wilaya ya Kwimba lakini Jimbo la Kwimba lina maji ya bomba kutoka ziwa Victoria lakini Jimbo la Sumve hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri aliwahi kuja kwenye ziara Wiayani Kwimba nikamwomba walau utengenezwe usanifu yale maji ya bomba katika tenki la lita milioni mbili waliloliweka kwenye Mji wa Ngudu yaende walau kwenye Kata za Lyoma, Malya, Wala ili kata zilizo karibu na mji wa Ngudu zipate maji kutoka Ziwa Victoria. Hata hivyo, naona bado usanifu ni wa kupeleka kata zilizo kwenye Jimbo la Kwimba lakini Jimbo la Sumve tumeachwa. Kwa niaba wa watu wa Sumve naomba kusema kwamba maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria ndiyo yatatuokoa na matatizo ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Sumve hata uchimbaji wa visima wamekuwa wakichimba wanakosa maji chini. Tuna shida visima havijawahi kutusaidia kutatua tatizo hili. Tunapata visima vichache lakini na vyenyewe havijengewi mfumo wa maji ambao utawafikia watu wote. Naomba katika jambo hili la maji kwenye Jimbo la Sumve mtuangalie kwa jicho la pekee. Naunga mkono hoja kama nilivyosema lakini nahitaji sana tupate majibu yanayoeleweka hasa kwenye mradi wa maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria kwenda kwenye Mji wa Malya, Sumve na Malampaka ambao utalisha vijiji vingi vya Jimbo la Sumve na kuwa limepunguza tatizo la maji kwa kiasi kikubwa kwa watu wa Sumve. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo la Sumve pia ipo miradi nimeona nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri miradi ya visima katika vijiji vya …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Nasisitiza maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria kwenda Jimbo la Sumve hayaepukiki, naomba mtusaidie. (Makofi)