Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nianze kwa kuungana na Wabunge wenzangu kuipongeza sana Wizara ya Maji kwa juhudi kubwa walizozifanya kusambaza maji vijijini. Vilevile napenda niwapongeze RUWASA Mkoa wa Songwe hasa Meneja Injinia Charles Pambe kwa kazi kubwa anayoifanya, ingawa nasikitika kusema kwamba RUWASA, Mkoa wa Songwe hatuna gari, wamekuwa wakifanya kazi kwa kuazimaazima gari. Vilevile nimpongeze meneja wa RUWASA, Wilaya ya Mbozi Bw. Gratius Haule kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya Wilaya ya Mbozi. (Makofi)

Mheshiniwa Naibu Spika, pamoja na juhudi hizi kubwa za Wizara ya Maji kusambaza maji huko vijijini juhudi hizi zinaweza zikawa bure kama Serikali haitaingilia gharama za kuunganisha maji vijijini. Katika ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi inasema kwamba kufika mwaka 2025 asilimia 85 ya wakazi wetu vijijini lazima wapate maji, lakini kwa gharama hizi ya shilingi laki nne laki tano kuungainishiwa maji, hivi mwananchi maskini wa kijijini hizi laki nne laki tano anapata wapi? (Makofi).

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wakulima mwananchi ataamua ni bora anunue mifuko ya mbolea kuliko kuunganishiwa maji, lakini kama gharama hizi zikishushwa zikawa sawa kama umeme wa REA ambao kuungaishiwa ni Shilingi elfu 27 tunaweza tukafikia sio tena asilimia 85 itakuwa ni asilimia 100. Ushauri wangu Mheshimiwa Waziri ni huu, wananchi waunganishiwe bure halafu wakate gharama za kuunganisha bure wanapokuja kulipia gharama za maji kila mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo kama wananchi wote wataunganishwa bure maji, halafu wakaja kuwakata mwisho wa mwezi wanapolipa bili yao ya maji, tunaweza kufika sio tena asilimia 100 hata asilimia 150, lakini bila kufanya hivyo hizi juhudi zote zitakuwa bure kama hatutaweza kushusha gharama za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine Mheshimiwa Waziri kwa masikitiko makubwa wananchi vijijini wanalazimishwa kununua vifaa vya kuunganisha maji kwenye mamlaka za maji. Sasa nataka niulize hizi mamlaka za maji zina maduka ya kununulia vifaa vya kuunganisha maji? Kama sio udalali! Kwa sababu maduka hayo hayo wananchi ambao wangeenda kununua ndio hayo hayo ambayo hao Maafisa wa Maji ndio wanakwenda kununua hivyo vifaa. Sasa kuna sababu gani ya msingi kulazimisha wananchi kununua vifaa vya kuunganisha maji kwenye mamlaka za maji, kwa nini wasiende kununua kivyao wao wa-deal tu na gharama za kuunganisha maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ushauri wangu ni huu, kama kweli tuna nia yakutaka kusambaza maji na kuhakikisha maji yanafika kwa kila mwananchi ndani ya nchi yetu ya Tanzania, ni lazima gharama za kuunganisha maji ziwe ndogo. Kwa kufanya hivyo tutaweza kabisa kumaliza tatizo la maji ndani ya nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)