Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja iliyopo mezani kwetu. Niungane na wenzangu kuwapongeza viongozi wa Wizara hii tukianza na Mheshimiwa Waziri Aweso na Naibu wake kwa kweli mnafanya kazi na mna kipaji cha kipekee cha kusikiliza watu na hiyo ndiyo sifa kubwa ambayo mnayo. Mnatenga muda kusikiliza watu badala ya ninyi kusema ili watu wawasikilize. Kwa hiyo, endeleeni na moyo kama huo ili mpate kushauriwa na ninyi muweza kuyatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile, nimpongeze Katibu Mkuu, Engineer Sanga lakini kipekee nimpongeze Mtendaji Mkuu wa RUWASA, Engineer Kivegalo. Ni watendaji wachache sana ambao wakifanya ziara wanatenga muda wa kukutana na wanasiasa. Engineer Kivegalo alivyofanya ziara Mkoani Mtwara alitenga muda wa kukutana na Wabunge wote wa Mkoa wa Mtwara. Watendaji wengi wana kawaida ya kusema wanasiasa wana nini hao lakini huyu alitembelea miradi, akawasiliza watendaji, jioni akatenga muda kwamba nimewasikiliza watendaji sasa nataka niwasikilize ninyi wawakilishi wa wananchi. Hongera sana Engineer na endelea na tabia kama hiyo utafanikiwa, naona future yako ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na Wabunge wenzangu wa Mtwara waliochangia kuhusu suala la maji Mkoani Mtwara. Kwa kweli suala la maji Mkoani Mtwara ni tete na hata kikao cha Kamati ya Ushauri cha Mkoa kilichopita agenda ya maji iliwekwa pembeni kwamba tuwe na kikao maalum kwa ajili ya kuzungumzia maji Mkoa wa Mtwara. Mheshimiwa Aweso nakupongeza kwa sababu tulivyofika hapa tulikutana, tukafanya kikao cha Wabunge wa Mtwara ukatusikiliza na wewe umeanza kuyafanyia kazi. Ndio maana nikakwambia kwamba una sifa ya kusikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maombi yetu makubwa yalikuwa mawili na nikushukuru kwa yote umeshayafanyia kazi. Cha kwanza, tulikwambia kwamba Mradi wa Maji wa Makonde ambao kwa bahati mbaya uliondolewa kwenye Mradi wa Vijiji 28 umeurudisha tena kwenye orodha ile, tunakupongeza sana. Mradi wa Makonde unahudumia karibu asilimia 40 ya Mkoa wa Mtwara, unahudumia halmashauri nne, Newala Mjini, Newala Vijijini, Tandahimba na Nanyamba. Kwa hiyo, mradi huu ukitekelezwa ipasavyo tutakuwa tumepunguza tatizo la maji katika Mkoa wetu wa Mtwara. Nikuombe usikilize ushauri wetu kwamba mradi wa maji wa Makonde chanzo kikubwa cha Mitema kuna maji mengi sana. Kwa hiyo, tutumie chanzo cha Mitema kupeleka maji Tandahimba na Nanyamba mtakuwa mmetatua changamoto ya maji kwa kiasi kikubwa katika Mkoa wetu wa Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi letu la pili kwenye kikao kile tulikwambia muda umefika sasa tutumie maji ya Mto Ruvuma. Mimi Jimbo langu la Nanyamba, Mheshimiwa Katani amesema kwake ni kilometa nane tu mimi ni zero distance, kwa sababu wananchi wangu wakati ule walikuwa wanalala Tanzania wanafanya kazi Msumbiji wanavuka kwa miguu Mto Ruvuma, kabla ya matatizo yale ya Msumbiji hayajaanza.

Mheshimiwa Spika, kile chanzo cha maji cha mradi wa kupelekeza maji Manispaa ya Mtwara kipo Nanyamba na maji yapo ya kutosha. Nimeona hapa tumetenga fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu kuyatoa maji Maembe Chini kwenda Nanyamba kama nilivyoshauri siku ile. Hongera sana uendelee kusikiliza hivyo, mradi huu unagusa vijiji 74 na Kata zaidi ya 13 ambazo ni za Nanyamba, Mtwara Vijijini na inawezekana mradi huu ukavuka ukaingia Jimbo la Mtama kwa sababu tumepakana. Kwa hiyo, mradi huo ukitekelezwa utatatua changamoto nyingi sana si za Nanyamba tu na maeneo mengi ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama walivyosema wenzangu kwamba muda umefika sasa kuanza utekelezaji wa mradi huu wa kutoa maji Mto Ruvuma na kupeleka Mtwara Manispaa. Nimeona shilingi bilioni sita zimetengwa maana siku za nyuma ilikuwa mradi huu unazungumzia tutatoa fidia, tutafanya upembuzi yakinifu lakini leo nikupongeze Waziri kwamba umeanza kuweka fedha. Naomba wakati wa utoaji wa fedha basi hizi fedha zitolewe ili mradi huu mkubwa uanze kutekelezwa na Manispaa ya Mtwara tuwe na maji ya uhakika kiasi kwamba hata wawekezaji wakija wajue wanawekeza Mtwara ambayo ina maji na umeme wa uhakika ambao sasa hivi upo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Nanyamba imesajiliwa kama Halmashauri ya Mji na kwa Sheria ya Maji tuna uwezo wa kuwa na mamlaka yetu. Sasa hivi tunahudumiwa na Mamlaka ya Maji ya Mtwara (MTUWASA) katika kipindi hiki cha mpito.

Kwa hiyo, naomba na hili sasa Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi, sisi tuna hadhi ya kuwa na mamlaka ya kwetu na hakuna sababu ya kuitumia ile Mamlaka ya MTUWASA. Ni muda umefika sasa kufanya taratibu zinazotakiwa ili na sisi tuwe na Mamlaka ya Maji ya Mji wa Nanyamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa mwisho ni kuhusu RUWASA. RUWASA ni mtoto mchanga anafanya kazi vizuri lakini kama walivyosema Wabunge wengine ana changamoto hebu tuiwezeshe RUWASA. Tuiwezeshe kwa vitendea kazi na rasilimali watu. Wilaya nyingine zina halmashauri zaidi ya moja, kwa mfano mimi Meneja wangu wa RUWASA anashughulikia Mtwara Vijijini na Nanyamba, lakini ana watendaji wachache. Naomba tuongeze watumishi ili mamlaka hii ambayo imeanza kufanya kazi vizuri iendelee kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)